Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, awali ya yote naomba kuunga mkono hoja hii ambayo imeletwa na kaka yangu Mheshimiwa Mpango, Waziri wa Fedha na Mipango. Kulikuwa na mambo kadhaa yamejitokeza yanayohusu Ofisi ya Rais, TAMISEMI na suala zima la bajeti kwa ujumla na hasa hoja kubwa iligusa suala la TARURA bajeti ni ndogo. Tulijadili hapa kwa kina na niseme wazi kwamba ni kweli, hata hivyo fedha nyingi zilizotengwa kwa ajili ya kuimarisha miundombinu zaidi shilingi bilioni 284.7 ambayo kwa imani yangu ni kwamba kwa usimamizi wetu mzuri tutahakikisha tunafanya mabadiliko makubwa.

Mheshimiwa Spika, wenzetu wa Bodi ya Mfuko wa Barabara sasa hivi wanapitia ile formula ya 30% kwa 70% kwa lengo kubwa nini kifanyike kuhakikisha kwamba mtandao wa barabara wapo katika Mamlaka za Serikali za Mitaa ambao unahudumiwa na TARURA ambao takribani kilomita 127 ziweze kuwezeshwa vizuri, zikafanye kazi vizuri. Kwa hiyo naomba niwahakikishe Waheshimiwa Wabunge kwamba, Serikali inafanya kazi hii ndiyo maana mkiona sehemu mbalimbali kazi kubwa inaendelea kufanyika.

Mheshimiwa Spika, katika upande wa elimu katika bajeti yetu niliyowasilisha hapa ni zaidi ya shilingi bilioni 58.24. Hii ni program ya EP4R kwa ajili shule za sekondari ambayo naona kwamba huko tuna mafanikio makubwa sana.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo katika pia Mradi wa Kuboresha Mpango wa Elimu ya Sekondari kupitia SEDP tumetenga zaidi ya shilingi bilioni 48.99 katika bajeti ya mwaka huu. Hali kadhalika mpango wa EP4R kwa ajili ya shule za msingi tumetenga zaidi ya shilingi bilioni 31.84 ambayo Waheshimiwa wataona ni kwa jinsi gani tunaenda kuitekeleza mipango hiyo katika mwaka wa fedha 2019/2020.

Mheshimiwa Spika, katika upande wa afya, naomba tuseme wazi kwamba tunaona juhudi kubwa ya Serikali, tumesikia hoja mbalimbali hapa lakini Serikali imefanya kazi kubwa sana. Ukiachia ujenzi wa hospitali 352 katika bajeti iliyopita, lakini mwaka huu tunaona kwamba tuna ujenzi wa vituo vya afya 352, lakini mwaka huu tuna vituo vya afya tena karibuni 52. Tunaendelea na ujenzi wa hospitali za wilaya 67, lakini hali kadhalika tuna hospitali mpya takribani 27. Kwa hiyo Waheshimiwa wataona katika mpango wa miaka miwili ujenzi wa hospitali 94 kwa mara ya kwanza ni outstanding performance kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambalo hili lazima tuna kila sababu ya kujisifu kama toka uhuru mpaka 2015 tulikuwa na hospitali 77 peke yake, lakini mpango wa miaka miwili, hospitali 94, tumevunja rekodi ambayo haijawahi kutokea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, naomba nizungumze wazi, kwa mfano unaona kwamba kila mjumbe alikuwa anazungumza kwamba bajeti hii ilikuwa inajali vitu, mimi niseme kwamba bajeti hii inajali watu. Katika hospitali tulizozijenga kila moja ilikuwa inachukua takribani wataalam ambao wameajiriwa katika eneo siyo chini ya 20. Leo hii tunapozungumza hospitali hizi 97, vituo vya afya 52, ukizizidisha mara 20 unaona jinsi gani watu huko wanaenda kuguswa katika soko la ajira, lakini hata katika utoaji wa huduma.

Mheshimiwa Spika, katika upande huu wa sekta ya elimu ambayo tuna miundombinu na tunatumia force account, unaona kwamba bajeti hii inaenda kuwagusa watu kwa kiwango kikubwa sana. Ndiyo maana nimesema kuwa bajeti hii ukisema ni ya vitu hapana, bajeti hii kwa ajili ya watu kwa sababu inaenda kutengeneza miundombinu, lakini hali kadhalika inawagusa watu katika maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba bajeti hii ambayo safari hii imekuja kujibu hasa matatizo ya Watanzania na imani yangu kubwa kwamba sisi Wabunge kwa umoja wetu tunaweka historia kwamba kutengeneza bajeti ya kihistoria ambayo haijawahi kutokea katika miaka hii ya karibuni, inawezekana. Lengo letu kubwa ni tuipe support bajeti hii, tuiunge mkono, halafu katika utekelezaji wa bajeti hii twende tukaisimamie vizuri kwa mustakabali mpana wa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, ajenda ya mwisho ilikuwa ni suala zima la vitambulisho vya wajasiriamali wadogo. Hili tumepokea changamoto mbalimbali hasa kero zinazotokea kule site, japokuwa maelekezo yalikuwa yamekuwa wazi kwamba lazima mfanyabiashara yule mdogo mauzo yake yasizidi milioni nne. Hata hivyo, katika utekelezaji wa jambo hili kila mtu alitafsiri kivyake, ndiyo maana unaona mikoa mingine imetulia, mikoa mingine ina changamoto. Jukumu letu ni kuangalia wapi kuna matatizo ili tuweze kuyarekebisha na lengo kubwa ni kwamba kila mfanyabiashara ambaye ni mdogo aweze kushiriki vizuri lakini hali kadhalika kutoa kadhia mbalimbali ambazo wananchi wetu zinawakabili.

Mheshimiwa Spika, kwa haya machache kwa sababu dakika zangu ni tano, naomba nikushukuru sana na naomba kuunga mkono bajeti hii kwa asilimia yote mia moja. Ahsante sana. (Makofi)