Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ili nami nitoe mchango wangu katika hoja hii muhimu ya Bajeti Kuu ya Serikali na Hali ya Uchumi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia afya na uzima ili kuwa miongoni mwa viumbe vyake kwa ajili ya kumuabudu na kupata nafasi ya kushiriki kutoa mchango wangu kweye hotuba hii ya muhimu kwa mustakabali na maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii pia kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha, Naibu Waziri wa Fedha, dada yangu, Mheshimiwa Dkt. Ashatu Kijaji, Katibu Mkuu Wizara ya Fedha Ndg. Dotto James na watumishi wote wa Wizara ya Fedha kwa kuchapakazi kwa bidii, uadilifu na uzalendo mkubwa na kufanikisha miradi mingi ya maendeleo mikubwa na midogo kutekelezwa katika maeneo mbalimbali nchini ikiwemo Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki.

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi hii inatekelezwa kwa sababu ya upatikanaji wa fedha kutoka Serikalini Kuu na Serikali ya Halmashauri nchini chini ya usimamizi mzuri wa Wizara hii ya Fedha kwa kusimamia makusanyo ya mapato ya Serikali vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru Serikali kwa kumpatia fedha katika Jimbo la Morogoro kwa kituo cha afya Mkuyuni, Mikese na Gwata, kila kimoja shilingi milioni 400; na pia uboreshaji wa barabara ya Bigwa – Kisaki, Mikese – Msombizi na Ubena Zomozi – Ngerengere – Tununguo – Mvuha – Kisaki Stiegler’s na Madamu – Kinole kwa kiwango cha changarawe na kuweza kupitika mwaka mzima kwa majira yote ya mvua na jua.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na uboreshaji wa barabara ya Bigwa – Kisaki kwa kiwango cha changarawe lakini bado ule umuhimu wa Serikali kuitengeneza barabara kwa kiwango cha lami uko palepale kwa sababu umuhimu wa barabara hii kwa shughuli za kiuchumi za wananchi wa Morogoro Vijijini umeongezeka, hasa shughuli za kilimo, uwekezaji wa kiwanda cha sukari cha Morogoro Sugar pamoja kuwepo kwa Makao Makuu ya Halmashauri ya Mvua.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia barabara hii ya Bigwa – Kisaki ndiyo inayotumika kufika kwenye mradi mkubwa wa kielelezo wa kufufua umeme wa Mto Rufiji (Stiegler’s). Kuwepo kwa mradi huu na Mbuga ya Selous kutaongeza wageni wa utalii na kuongeza mapato ya Serikali na uchumi wa taifa. Kwa umuhimu huo, barabara hii ina umuhimu na ulazima wa kujengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali kuweka barabara hii ya Bigwa – Kisaki katika bajeti ya mwaka 2019/ 2020 kujengwa kwa kiwango cha lami. Ombi langu kwa Serikali kuwahisha ujenzi wa barabara hiyo kwa haraka na kuongeza kiwango cha fedha za bajeti na kuzitoa kwa ajili ya utekelezaji wa ujenzi wa barabara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu wa pili ni maombi ya vituo vya afya Kata za Kinole na Tegetero kule milimani kwenye Milima ya Uluguru ambao wako mbali na Makao Makuu ya Tarafa Mkuyani Bondeni. Pia vituo vya afya katika Kata za Ngerengere, Tununguo, Kidugalo na Mkulazi katika Tarafa ya Ngerengere ambako hakuna hata kituo kimoja chenye hadhi ya kituo cha afya ilhali ni tarafa kubwa kuliko tarafa zote kwenye Wilaya ya Morogoro. Pia tuna kambi nyingi za jeshi kituo kikuu cha garimoshi ya kisasa (SGR) na ujenzi wa Kiwanda cha Sukari Mkulazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba Serikali, vituo vya afya katika Kata ya Kibuko ambayo ni kata mpya, Kata ya Kiloka na Tomondo ambazo zina watu wengi sana katika Tarafa ya Mkuyuni.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba ujenzi wa mabweni na madarasa ya vidato vya tano na sita katika Shule za Sekondari Mkuyani, Nelson Mandela na Ngerengere ili kuwa na shule za vidato vya tano na sita kwenye makao makuu ya tarafa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba Serikali kuboresha miundombinu ya Shule za Msingi za Mkunyani, Mikese na Njia Nne Ngerengere kwa sababu zina uhitaji mkubwa wa vyumba vya madarasa vya ziada kila moja zaidi ya 20 kwa kila shule.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya mchago wangu kuwasemea watu wa Morogoro Kusini Mashariki, sasa naomba kushauri Serikali katika kuongeza mapato ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Fedha ya Serikali za Mitaa ya Mwaka 1982, Sura ya 290, kifungu 7(1)(g) na kufanyiwa marekebisho kupitia Sheria ya Fedha ya Mwaka 2017 kupitia kifungu cha 32(a),(b) na (c) kuhusu produce cess na kifungu cha 13(4) kuhusu ushuru wa huduma. Sheria hizi zinainyima Serikali mapato makubwa. Ushauri wangu ni kama ifuatavyo:-

(i) Makampuni yanayolima na kuchakata mazao ya miwa na mkonge kulipa kodi ya kuzalisha mazao katika halmashauri wanazolima mazao na kusamehewa kodi ya huduma kwenye halmashauri hiyo.

(ii) Makampuni makubwa yanayolima na kuuza nje ya nchi mazao yao ambao hatuna uwezo wa kukusanya kodi ya mazao kwa wanunuzi, Sheria ya Fedha ya 2019/2020 itamke kuwa muuzaji wa mkonge akusanye kodi hiyo kwa mteja wake kwa niaba ya Serikali na asipokusanya atalipa yeye mkulima mkubwa.

(iii) Mwekezaji/mnunuzi anayenunua mazao halmashauri moja na kwenda kuchakata mazao yake katika halmashauri tofauti na aliyozalisha mazao hayo anapaswa kulipa tozo na ushuru, zote mbili, yaani produce cess na ushuru wa mazao kwa halmashauri aliyozalisha na kulipa ushuru wa huduma (service levy) katika halmashauri anakokwenda kuchakata mazao yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Serikali kuingiza mapendekezo haya katika Sheria ya Fedha ya Mwaka 2019/ 2020 ili kuongezea mapato ya Serikali na kuimarisha mapato ya halmashauri na kusukuma maendeleo ya wananchi kwa haraka katika mikoa na taifa kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, naomba Serikali kuboresha na kupanua miradi chakavu ya maji ya zamani ya Mkuyani na Kivuma pamoja na mradi wa Pangawe – Kizinga.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja.