Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Mariamu Nassoro Kisangi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja, hoja hii ya Bajeti ya Serikali. Nampongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Makatibu Wakuu na Watendaji wote wa Serikali kwa kazi nzuri na ngumu wanazozifanya kuhakikisha nchi yetu inaenda vizuri. Bajeti ya Serikali iliyosomwa ni nzuri sana na imegusa maeneo mbalimbali, lakini pia, kuondoa tozo ambazo zilikuwa kero kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakubaliana na Bajeti ya Serikali kwa jinsi ilivyowasilishwa pamoja na Mpango wa Maendeleo wa Taifa na utekelezaji wake kama inavyoonesha katika ukurasa 138. Kwa kweli, mambo mengi yaliyopo katika mpango yamefanikiwa kwa kiasi kukubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, maoni yangu kwa upande wa biashara ni kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza natoa pongezi kwa Serikali kwa kutoa muda wa miezi sita kwa wafanyabisahara wanaoanza biashara na kulipa kodi kwa muda huo. Kwa kweli, hii ilikuwa ni shida kubwa kwa wafanyabiashara wenye mitaji midogo. Shukrani sana kwa kulitekeleza hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, naomba kwanza kuweka maslahi yangu wazi kuwa, mimi ni mdau wa sekta ya mafuta. Tatizo kubwa la wawekezaji wa mafuta na gesi na hata wawekezaji wengine ni vibali vya kuanzisha ujenzi wa biashara ambavyo, lazima ufike EWURA, NEMC, OSHA, Bodi ya Majengo, Bodi ya Architect, TRA, Halmashauri/ Manispaa, Ardhi, Bonde la Mto/Visima. Kwa kweli kazi hiyo ni kubwa sana mara nyingine unatamani kuacha kuwekeza. Ushauri wangu, kwenye One Stop Centre ya uwekezaji kuwepo na wahusika hao wote ili wananchi wanapotaka kuanzisha biashara wanawaona. Ni bora kulipa gharama kubwa wakati mmoja kuliko usumbufu usiokuwa na mwisho.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, biashara ya mafuta kwa maoni yangu naona ilikuwa imekaa vizuri, tatizo ni wale mawakala ambao wanalipwa Sh.2,830,000/= kwa mwaka, lakini mashine zinapoharibiwa wanakuwa wazito kuja kurekebisha, ndio tatizo. Kwa maoni yangu naona mfumo wa EFD za vituo vya mafuta ukiboreshwa hali itakuwa nzuri zaidi kwa kuwa, sekta ya mafuta ilikuwa na ubabaishaji mkubwa sana, lakini kwa kutumia mashine hizi Serikali imepata kodi zake na hali imezoeleka tusibadilishe kwa haraka mfumo uliopo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Bandari; naungana na Serikali kwa kuruhusu watu kuingia bandarini kutoa mizigo yao, lakini ulinzi uboreshwe kwa kuwa, mizigo ni mingi. Tukiingia wote inaweza kuwa ni vurumai ndani ya bandari japo kwa upande mwingine wataamsha na kuleta uhai wa bandari.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa kupongeza Serikali kwa kudhibiti mfumo wa bei na hasa katika kipindi cha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani. Nazi iliuzwa mpaka 500/= na vitu vyote bei ilishuka ghafla na kuwa chini, haijawahi kutokea kwa miaka zaidi ya 10, sijawahi kuona hali hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.