Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Muhammed Amour Muhammed

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Bumbwini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. MUHAMMED AMOUR MUHAMMED: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nakushukuru kunipatia fursa ya kuchangia bajeti ya Serikali ya mwaka 2019/2020. Kwanza nitoe pongezi kwa hotuba nzuri sana kutoka Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni jinsi ilivyosheheni ushauri mzuri sana kwa Serikali. Pia kabla sijaendelea na mchango wangu naomba niikumbushe Serikali ile ahadi tuliyotoa kwamba tutawapatia wana vijiji wetu milioni 50 kila kijiji katika Tanzania hii ule wakati wa kutoa ndiyo huu. Watanzania wana msemo wao wanasema, ahadi ni deni kwa muungwana na muungwana ni kitendo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo nianze rasmi, kwanza nitaanza na elimu, elimu ndiyo mwanzo kuliko kila kitu na hapa nataka kuzungumzia Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu. Kwa kipindi kirefu sasa kumekuwa na ucheleweshwaji mkubwa sana wanaopatiwa vijana wetu hawa wanaoanza chuo. Wale vijana wanaomba mikopo baada ya kuomba na kupata uhakika wa kujiunga na vyuo. Wanapoomba mikopo kwenye Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu nao wanaarifiwa kwamba mkopo umepata lakini inafika wakati wanaenda chuo ile mikopo bado hawajapata. Wanakaa wiki tatu, mwezi mmoja; sasa je, muda ule wote watapata wapi fedha ya kujikimu?

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni hatari kwa maslahi ya hao vijana wetu, mimi niiombe Serikali kwa heshima zote ifikirie tena wale vijana once wakiripoti tu pale chuoni basi siku ya kwanza, ya pili, sana sana ya siku ya tatu basi zile akaunti zao ziseme. Ile mikopo yao wapewe ili waweze kuwa na utulivu wasome vizuri pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeangalia vizuri sana kitabu cha bajeti lakini bajeti ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano siyo sensitive kwa Zanzibar, haitaji kabisa Zanzibar. Naomba uniongeze dakika mbili, tatu labda turudi kwenye historia tuangalie kwani hii Tanzania ni nini? Na Tanzania ni akina nani hasa? Kwa kipindi kirefu hakukuwa na Taifa linaloitwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni two Independent Sovereign State ndizo zilizokuja kwenye shirikisho zikaunda Tanzania United Republic of. Jamhuri ya watu wa Tanganyika na Jamhuri ya watu wa Tanganyika wakaungana pamoja wakatengeneza Jamhuri ya watu wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mbele ya hii Jamhuri ya watu wa Tanzania kuna Mamlaka tatu hapa separately. Kwanza Zanzibar na Tanganyika walikubali kusalimisha baadhi ya mamlaka yao wakayaweka pamoja wakasema haya ndiyo mambo tutakayoshirikiana katika Muungano, Nataka kuzungumzia haya. Pia kuna mambo mengine yakabaki Tanganyika, wao watafanya peke yao lakini still yatasimamiwa na Serikali ya Muungano, hayo ni ya kwao peke yao Tanganyika. Kwa upande wa Zanzibar wao watasimamia yale mambo yaliyokuwa si ya Muungano kwa upande wa Zanzibar yatasimamiwa na SMZ. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nataka kuzungumza hiki kikapu cha pamoja hiki, hapa ndiyo bajeti haiku sensitive na Zanzibar. Ukienda bandarini pale Zanzibar, nianzie hapa Dar es Salaam kwanza, ukienda pale kuna maboresho mengi sana kabisa ya bandari yanafanywa, ni Union meter ile. Ni jambo jema, zuri nalipongeza kwa kweli, tulikuwa tunapendelea tuone kwamba na Zanzibar mambo kama yale yanafanywa. Ukienda uwanja wa ndege Dar es Salaam the reserve holl room, ukienda uwanja wa ndege Zanzibar umeachwa kama kwamba wenyewe hawapo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa wapi tunakwenda watanzania, Baba wa Taifa alisema hapa, umoja na nguvu na utengano ni udhaifu. Kwa hivyo mnatutenga, narudia kusema hapa miradi mingi sana ya kimaendeleo hata yale ya Muungano yanafanywa upande mmoja tu wa muungano na upande wa pili unaachwa kama kwamba wao siyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, juzi tu Waziri wa fedha kule Zanzibar anawasilisha bajeti yake kwenye Baraza la Wawakilishi kalitamka hili, kwamba wenzetu wametukalia pabaya kwenye uchumi, tunapotaka kuomba mikopo wanakataa kutupa loan guarantee. Juzi hapa kuna Mbunge mmoja alichangia akakuletea hii document ambayo Waziri wa Fedha Mheshimiwa Dkt. Mpango alikataa kusaini na akamwambia yule mjumbe hapa, Mheshimiwa Dkt. Mpango una roho mbaya sana alimwambia hivyo. Sasa siweze kusema hivyo lakini kama utaratibu utakuwa ndiyo huu na nyingine tunayo hapa kama hiyo ya mwaka 2014. Wakati ule sijui Waziri wa Fedha alikuwa nani, naye alikataa kusaini, sasa kama trend itakuwa ndiyo hii hata ile sifa ya kuambiwa Waziri Mpango una roho mbaya itakuwa haikutoshi, labda tufikirie msamiati mwingine tukupatie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo niseme naiomba Serikali kwa heshima zote, kwa heshima zote, kwa heshima zote. Najua Mheshimia Waziri Dkt. Mpango wala huna roho mbaya ni mtu mzuri, kule Zanzibar kuna ndugu zako kule na wewe unaelewa hilo. Kwa hivyo nikuombe ukae na Waziri mwenzako wa SMZ mfikirie namna gani itapatikana mikopo ya namna kama hii mnakaa pamoja, mnazungumza ili ile mikopo Zanzibar nayo ipate. Au mtataka wale watu kule wafe? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niende 4.5 ambayo Zanzibar inapata kutoka Serikali ya Muungano. Wakati East Africa Currency Board inavunjika Zanzibar ilikuwa inachangia karibu asilimia 11, tukatengeneza BoT, BoT kule sisi kuna mtaji wetu Zanzibar, tukakubaliana tupewe 4.5 siyo mbaya. Kwa hiyo, wakati ule ilikuwa inatosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivi sasa demand ni kubwa sana, population inaongezeka kwa kiasi kikubwa sana kule Zanzibar nadhani na hata huku Bara viwanda vya kutengeneza watoto Alhamdulillah. Sasa watu wanaongezeka kwa kiasi kikubwa sana sana kabisa. Kwa hivyo 4.5 haitoshe kwa mahitaji hayo ya sasa ya Zanzibar. Sasa niiombe Serikali kwa heshima zote kabisa, mkae tena mjadili angalau tutoke kwenye 4.5% tuende 9% angalau Zanzibar nayo ikaweze kujitutumua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kauli ya Serikali kwamba uchumi wa Taifa umepanda kwa asilimia 7. Hapa napa pana matatizo kidogo ila sitaki kupingana na Serikali wala sitaki niishutumu vibaya Serikali kwa sababu wao ndiyo wenye mandate ya kuweka hizi data na kuzitangaza kwa watu wote nchini. Hii 7.5 tunaweza kui-transform vipi hii from the digital form kwenye paper in to our everyday life, hili swali sasa, how we can verify this? Siyo tunasema tu kwamba 7.1%, Je, tunajenga Standard Gauge? Ukiangalia uchumi katika nchi yetu sasa katika yearly practice ni vigumu mtanzania wa kawaida kukubali hili hakubali kirahisi. Mifuko kidogo imetoboka, korosho ndiyo hivyo Nchi is going a stun

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda uwekezaji umeshuka nearly 40%, uzalishaji nao mtihani mtupu, wafanyakazi na watumishi wengine Serikalini hawaongezwi mishahara. Sasa kama uchumi umepanda, wapi unasema? Kwa sababu inabidi mfanye mipango tuone maana yake ni kweli huu uchumi umepanda really practice. Kuna watu wakati fulani walikuwa wanaishi kwa milo miwili, hivi sasa hata huo mmoja kidogo ni mtihani. Sasa niombe sana sana sana kwa heshima zote, Serikali jaribuni ku-transform hii data 7.1 muilete in to our everyday life tuone kwamba ni kweli uchumi sasa umepanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho nije kwenye Mfuko wa Jimbo, hapa kwa kweli kuna matatizo makubwa. Nia njema ya Serikali kutoa Mfuko wa Jimbo kwa Wabunge wote wa Majimbo Tanzania nzima is a good approach, kwa kweli naipongeza. Sasa swali langu liko hapa; mnapohakiki, mnafanya uhakiki, mnahakikisha vipi kwamba hii fedha imewakuta walengwa na wameitumia kama vile inavyotakiwa. Naheshimu uwepo wa Waziri Kiongozi wa zamani wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Mheshimiwa Shams Vuai Nahodha na naheshimu uwepo wa Waziri Mkuu ambaye ni Mtendaji Mkuu wa Shughuli za Serikali Bungeni.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Amour Kengele ya pili imeshagonga, ahsante sana shukrani sana. Ahsante Mheshimiwa. (Kicheko)

MHE. MUHAMMED AMOUR MUHAMMED: Mheshimiwa Naibu Spika, dakika mbili naomba.

NAIBU SPIKA: Dakika moja!

MHE. MUHAMMED AMOUR MUHAMMED: Haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mbunge wako sijapata Mfuko wa Jimbo wa mwaka uliopita. Sasa kama Serikali kuna watu mliwapa waje watupe, mimi bado. Ni hilo sasa, ahsante. (Makofi)