Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Neema William Mgaya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi kuweza kuchangia hotuba hii ya Wizara ya fedha na Mipango.

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya ya kuweza kusimama ndani ya Bunge hili Tukufu na kuweza kuchangia hotuba hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli wka kazi kubwa anayoifanya ya kutekeleza miradi mikubwa ambayo itakuja kuleta tija na kujenga uchumi endelevu wa nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza pia Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na timu nzima ya Wizara hii ya Fedha kwa kuona umuhimu wa kutumia malighafi za kilimo, mifugo, uvuvi, madini katika kuzalisha bidhaa mbalimbali kwa ajili ya soko la ndani ya nchi yetu na ziada kwa ajili soko la nje na vilevile na kuongeza ajira kwa vijana.

Mheshimiwa Naibu Spika, dira yetu ni ya kujenga nchi ya viwanda; ni vyema basi tukajenga viwanda ambavyo vitatumia malighafi inayopatikana ndani ya nchi yetu kama hizo malighafi za kilimo, mifugo, uvuvi, madini n.k.

Mheshimiwa naibu Spika, nchi yetu imejaaliwa sana kuwa na malighafi hizi ndani ya maeneo mbalimbali ya nchi yetu. Ukiangalia kule Ludewa, nchi yetu imejaaliwa kuwa na madini ya chuma katika mradi wa Liganga na Mchuchuma. Kule kwenye mradi wa Liganga na Mchuchuma kuna takribani tani 128 za chuma ambazo zimechanganyika na madini mengine. Haya madini yanaweza kutusaidia kujenga uchumi wetu kama tukiamua kuyachimba na kuyatumia katika viwanda vya kutengeneza nondo, mabati, viwanda vya kutengeneza vifaa vya ujenzi wa madaraja na reli. Kwa kuweza kuzalisha chuma hiki tutaweza kuokoa pesa bilioni 640 kila mwaka kwa muda wa miaka 30 ya uhai wa mgodi huu wa Liganga na Mchuchuma, sambamba na kutengeneza ajira 35,000 zitakazotokana na mgodi huu wa Liganga na Mchuchuma.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la malighafi ya misitu. Mkoa wa Njombe, Songwe, Mbeya, Iringa, Katavi, Rukwa, Tanga na mingineyo ndani ya nchi yetu ya Tanzania ina malighafi nyingi sana za misitu lakini vilevile misitu hii tuna kila aina ya mbao; tuna soft wood, tuna hard wood, tuna mianzi tuna mpaka nta ya kuweza kutengenezea furniture. Nilikuwa naiomba Serikali ihamasishe wawekezaji ambao watatumia malighafi hizi za mbao kuwekeza katika viwanda vya kutengeneza karatasi kwa wingi. Kwa kufanya hivi tutakwenda kutumia karatasi zetu za ndani ya Nchi bila kuagiza nje ya Nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile niishauri Serikali ihamasishe wawekezaji wa viwanda vya furniture ili waweze kuwekeza kwa wingi ndani ya nchi yetu na tuendelee kununua furniture ambazo zitakuwa zinatengenezwa ndani ya nchi yetu ambazo zina ubora zaidi ukilinganisha na zile ambazo zinatoka nje ya nchi. nyingi ambazo zinatoka nje ya nchi zinakuwani mavumbi tu ya mbao, siyo mbao halisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile ni wakati muafaka wa kujiuliza hivi kwa nini Serikali inaendelea kununua samani nje ya nchi ilhali tuna JKT, tuna Magareza, tuna viwanda vya watu binafsi ambavyo vinatengeneza mbao ndani ya nchi yetu. Na kwa hili niiombe sana Serikali iangalie namna bora ya kusaidia viwanda hivi vya furniture ambavyo viko ndani ya nchi yetu lakini vilevile na kuhamasiaha zaid wawekezaji wapya wa kuweza kuwekeza katika vianda hivi vya furniture na kuwatolea tozo na kodi ambazo si za lazima katika ufanisi wa viwanda hivi vya furniture. Vilevile wawaondolee kodi katika vile vifaa ambavyo vinatumika kurembea furniture zetu. Kwa mfano, vitasa, kuna vile vimishikio, msasa, vanish, vyote hivyo viondolewe kodi ili kuweza kuhamasisha ufunguaji wa viwanda vingi ndani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nilikuwa naiomba Serikali iongeze kodi kwa furniture zile ambazo zinatoka nje ya nchi ili kuweza kulinda viwanda vya furnitures ambavyo viko ndani ya nchi na ambavyo vitakavyoendelea kufunguliwa ndani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukiwa bado katika suala zima la utengenezwaji wa samani bado kuna hii mlaighafi ya ngozi. Namini kabisa Tanzania tuna malighafi nyingi ya ngozi, tukiachilia mbali kutengeneza tu mikoba na viatu tuangalie namna bora ya kuweza kuwekeza zaidi katika viwanda vitakavyoweza kutumia malighafi ya ngozi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kule Ethiopia wenzetu wameingia mkataba na Kampuni ya Mercedes Benz. Nchi ya Ethiopia ina-supply ngozi ambayo inatengeneza viti ambavyo vinatumika katika magari ya Mercedes Benz. Nilikuwanaishauri Serikali ifanye utafiti na uwezekano wa kuingia mikataba kama hiyo ambayo Ethiopia wenzetu wameingia ili kuweza kutumia malighafi ya ngozi yetu lakini vilevile na kuweza kuongeza uchumi wa taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sitoridhika kama nitamaliza kuchangia hotuba hii bila kuzungumzia malighafi ya mazao ya kilimo na hususani katika zao la parachichi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Njombe, Songwe, Rukwa, Mbeya, Iringa na Mikoa mingine ndani ya Tanzania inalima sana parachichi; na tunaishukuru Serikali kwa mikakati mbalimbali ambayo imefanya ya kuweza kuwasaidia wakulim wa parachichi kusafirisha nje ya nchi parachichi hiyo ikiwa ghafi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo bado, Serikali itafute namna ya kuhakikisha kwamba inahamasisha wawekezaji ambao watakuja kutumia malighafi hii ya parachichi ndani ya nchi yetu kuweza kufungua viwanda mbalimbali ambavyo vitatumia malighafi ya parachichi hii vikiwemo viwanda vya cosmetics kama mafuta ya nywele, lotion, conditioner kwa ajili ya nywele. Vile vile malighafi hii ya parachichi tunaweza kufungua viwanda vya kutengeneza asali pamoja na dawa ambazo zinatokana na majani ya parachichi. Kwa kufanya hivyo, tutaweza kukuza uchumi wa nchi yetu na kuweza kuendelea mbele. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kuishauri Serikali, kule bandarini nilikuwa naishauri Serikali iweze kuanzisha, iweke ile single receiving point ya mafuta. Kwa kuweka single receiving point ya mafuta, faida kubwa itasaidia katika kupunguza zile demurrage charges ambazo zinakwenda kumsaidia mfanyabiashara wa mafuta kumpunguzia mzigo. Halikadhalika itaenda ku...

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa, kengele ya pili ilishagonga.