Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushuru sana kunipa nafasi ili nami niweze kutoa mchango wangu kuhusiana na hoja hii iliyo mbele yetu ya Waziri wa Fedha na Mipango.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango pamoja na Naibu Waziri wake kwa sababu ya nguvu na akili walizoweka kwenye kuandaa bajeti ya mwaka huu. Kusema ukweli wameweka nguvu na akili kubwa, lakini pia wametoka na kitu ambacho ni cha manufaa na kina leta matumaini kwa Watanzania wengi sana. Kwa hiyo niwapongeze sana Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri Mheshimiwa Katibu Mkuu pamoja na watendaji wote wa Wizara hii, kwa kuja na bajeti ambayo inatoa matumaini makubwa kwa Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, mapinduzi ya viwanda ya nchi ya Uingereza yalisababishwa na mambo mawili tu. Cha kwanza ni nishati, na hiyo ilikuwa ni nishati ya makaa ya mawe. Halafu cha pili mapinduzi kwenye usafiri na uchukuzi, na njia kubwa iliyokuwapo ni njia ya reli. Mambo hayo mawili yalisababisa Waingereza wakafanya mapinduzi ya viwanda na wakaanza kuzalisha bidhaa nyingi. Mpaka ilipofika mwaka wa 1884 na kuendelea wakaanza kutafuta masoko ya bidhaa zilizokuwa zikilizalishwa kwenye viwanda vyao.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakaanzia Ulaya wakafika mpaka kwetu Afrika na huku wakaona ili waunze bidhaa zao vizuri lazima watutawale; lakini chanzo ilikuwa ni nishati ya umeme walioyoipata kwa njia iliyokuwa rahisi lakini pia mambo ya usafiri, uchukuzi na mambo mengine. Kwa hiyo tunaponzungumza nchini kwetu juu ya kuzalisha umeme wa kutosha bado tupo sahihi. Nchi yetu tunapozungumza reli ya kisasa na kuboresha njia za usafiri nyingine zote, barabara na viwanja vya ndege pamoja nakuwa na ndege zetu bado tupo sahihi. Mheshimiwa Rais yupo sahihi, wasaidizi wake wanaomshauri, Makamu wa Rais Mheshimiwa Waziri Mkuu na Mawaziri wengine wote tupo sahihi na tupo kwenye njia sahihi. Kwa hiyo ninaamini baada ya miaka michache hawa wanaopotosha na kubeza watakuja kukubali ya kwamba tulipata kiongozi kwenye miaka hii ambaye alitupeleka mahali kulipokuwa sahihi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kutoa ushauri kwa mambo mawili au matatu. La kwanza ni kuhusu Shirika letu la TPDS. Shirika hili limeboreshwa sana sasa hivi, limeunda kampuni mbili zingine, yaani kampuni inayoshughulika na gesi na kampuni nyingine inashughulika na mafuta. Shirika hili limepewa majukumu mbalimbali lakini jukumu mojawapo ni kuhakikisha kwamba linaendeleza matumizi ya gesi kwenye nchi yetu. Kwa kutimiza jukumu hilo, shirika hili limeweza kupeleka gesi kwenye viwanda 41 na lipo mbioni kupeleka gesi kwenye viwanda vingine 14.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini si hivyo tu shirika hili pia limeweza kuunganisha kwenye magari zaidi ya 200 ili yaweze kutumia gesi pamoja na petrol; sasa magari haya ni mengi sana. Pamoja na mambo hayo shirika hili limeweza pia kuunganisha gesi kwenye baadhi ya kaya katika jiji la Dar es Salaam ili gesi hiyo iweze kutumika majumbani.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naomba sana Serikali ijaribu kuangalia kulipa nguvu shirika hili ili liweze kuendelea na mpango wake hasa ule wa kutumia gesi kwenye magari kwa sababu mpango huu una faida kubwa kwa nchi yetu. Kwa mfano magari haya 200 kama yangekuwa ni ya serikali. Serikali ingeweza kuokoa pesa nyingi kwa sababu kwa mujibu wa maelezo yao kutoka Dar es Salaam kuja hapa Dodoma mtungi unaoweza kutumika kwa gari linalotumia petrol ni mtungi wa kil 15 ambao unagharimu kama shilingi 40,000 au na kidogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa maana yake kutoka Dar es Salaam kuja hapa Dodoma unaweza kufika kwa shilingi sana nyingi 50,000 balada ya shilingi 150,000 mpaka shilingi 200,000. Kwa hiyo ikiwa shirika hili litawezeshwa likajenga vituo vya kuweka gesi hapa Dodoma na pengine Manyoni au Singida na mahali pengine Shinyanga au Mwanza, mtu anaweza akatoka Dar es Salaam mpaka Mwanza akatumia gesi, kitu ambacho kitamgharimu hela kidogo mpaka kufika Mwanza. Na kwa maana hiyo nchi inaweza ikaokoa hela nyingi sana za kigeni ambazo tunatumia kununua mafuta petrol na diesel.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nchi inaweza ikaokoa hali zetu za mazingira kwa sababu gesi ni rafiki ya mazingira. Kwa hiyo nilikuwa nashauri kwamba shirika hili liwezeshwe na liweze kugharimia au liweze kutoa gesi kwenye magari mengi zaidi. Mimi nilikuwa nashauri pengine Serikali ingefikiria sasa kuleta magari yake yanayotumia njia mbili, njia mojawapo iwe ya gesi ili kwamba magari hayo mengi ya Serikali yatumie gesi badala ya kutumia petrol au diesel, hilo ni jambo la kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ambalo nataka kushauri; sasa hivi dunia yetu inaendeshwa kimtandao. Kuna kitu ambacho kinaitwa Digital Economy, na duania yote sasa mwelekeo ni huo. Sasa ukijaribu kuangalia sisi tunatumia mifumo hii kwa uchache sana. Naelewa serikali imeweka mifumo ya TEHAMA mbalimbali, inayo, lakini bado hatujamia fursa hii kwa ukamilifu wake. Kuna mambo mengi ambayo yanatumiwa kwenye uchumi huu wa ki-dijitali. Kwa mfano siku hizi kuna mikopo unaweza ukapata kwa kupitia simu yako ya mkononi, lakini pia kuna namna nyingi zinatumika kuanzisha mitandao mbalimbali ambayo kupitia mitandao hiyo watu wanalipa pesa na wanapata bidhaa zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nilikuwa nashauri kwamba sisi kama nchi hebu tunanze kufikiria kuchukua hii fursa ambayo iko wazi sasa hivi kwanza kwa kuwa na sera ya TEHAMA. Kwa sababu sera ya TEHAMA pia hatuna; tuwe na sera ya ICT halafu baada ya hapa tuwe na sheria zitakazotu-guide namna ya uwendeshaji wa uchumi huo ambao dunia inakimbia haraka kuelekea huko.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nilikuwa nashauri kwamba sasa sisi kama nchi tunapopanga mipango yetu ya uchumi tuanze kufikiria jambo hili ambalo hatuwezi kuliepuka.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie jambo la tatu kuhusiana na masoko ya mazao yetu; jambo ambalo limezungumza na Wabunge wengine. Mwaka jana Serikali ilifanya uamuzi mzuri, Wizara ya Kilimo ikanunua korosho kutoka kwa wa kulima kwa bei nzuri lakini korosho ile hatujaweza kuiuza kwa sababu shida ni masoko. Pia sasa hivi tupo kwenye msimu wa kuuza pamba, pamba yetu sasa hivi inapelekwa tu kwenye magodauni ya vyama vya mashirika lakini hakuna mnunuziā€¦

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mashimba Ndaki kengere ya pili imeshagonga.

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na naunga mkono hoja.