Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Joseph Roman Selasini

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Rombo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nichangie kwenye bajeti hii ya Serikali. Ningetaka niseme tu tangu mwanzo kwamba hii siyo bajeti ya Mheshimiwa Dkt. Mpango na mtani wangu Mheshimiwa Naibu Waziri Dkt. Ashatu, hii ni bajeti ya Serikali. Bahati mbaya sana Mheshimiwa Dkt. Mpango kwa sababu ni Waziri anapokea hayo madongo na namjua ni mtu mnyenyekevu anayapokea pia kwa shukrani, kwa hiyo, mzee pokea tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, niseme ninaunga mkono sera ya Serikali ya viwanda na kama Mheshimiwa Mlinga angekuwepo aoneshe Ilani ya CHADEMA angeona kwamba vilevile hiyo sera ipo. Kwa sababu ni mapinduzi ya viwanda yatakayotusaidia kusonga mbele katika nchi hii. Ningependa nitoe ushauri kuhusiana na jambo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ningesema kwamba basi Serikali ijitahidi kabla haijahamasisha au sambamba na uhamasishaji wa viwanda vipya, ifufue vile viwanda vya zamani vilivyojengwa na Serikali ya Awamu ya Kwanza chini ya Mwalimu Nyerere na kama mtakumbuka, Mwalimu alijenga viwanda karibu katika kila mkoa, kanda na alijenga viwanda kwa ajili ya kuyapa mazao yetu thamani. Tanga alijenga viwanda vya nyuzi, nguo, katani na viwanda vya magunia na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, viwanda hivi vilikuwa vimesambaa maeneo mengi katika nchi yetu, kwa mfano, pale Moshi kulikuwa na Kiwanda cha Machine Tools, Kiwanda cha Magunia, Kiwanda cha Plywood, Kibo Match, Coffee Curing, Moshi Textile, Kiwanda cha Pipi, Kiwanda cha Dawa za Mimea, Pharmaceutical Industry, Plastic Court, ICC Meal Café, Kiwanda cha Bidhaa za Misitu na Kibo Paper, vyote hivi vimekufa. Sasa tunahangaika kufungua viwanda vingine lakini viwanda hivi ambavyo vilianzishwa vingine kwa kodi za wananchi na utaalam na wataalam wenyewe wapo tunaviacha tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nashauri hivi kwamba Serikali iamue kwa makusudi mazima kama ilivyoamua kuchukua mashamba pori vile viwanda ambavyo vilibinafsishwa na wale wawekezaji hawakuviendeleza kadri ya mkataba, Serikali ichukue vile viwanda, itafutie Vyama vya Ushirika au labda wananchi ambao wana uwezo wa kuendesha hivi viwanda waendeshe hivi viwanda kwa sababu hivi viwanda ni mali yetu na vilianzishwa kwa kodi zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, halafu vilevile napendekeza sambamba na hili tuhakikishe kwamba tunarejesha imani ya wawekezaji kwa sababu ni kujidanganya kusema kwamba sisi wenyewe tuna uwezo wa kuanzisha viwanda wenyewe tu hapa ndani. Sisi tuko katika dunia ambayo imegeuka kuwa kijiji. Sasa katika hilo ningependekeza sasa Waziri Mheshimiwa Dkt. Mpango hapa pamoja na timu yake waangalie kodi zetu katika mambo mbalimbali. Wizara ya Ardhi iangalie namna ambavyo wawekezaji wanakuja hapa kupata maeneo ya kuanzisha viwanda kwa urahisi. Halafu na hawa viongozi wetu watu wazima, waangalie namna ya kuongea, kuwapa semina hawa viongozi vijana ili waangalie lugha ya kuongea na wawekezaji, vinginevyo mwekezaji mmoja akisumbuliwa hapa, akienda nje matokeo yake anaenda kuharibu image ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu, ningesema haiwezekani suala la uanzishaji wa viwanda likabaki kwenye Wizara ya Viwanda peke yake, vinginevyo mtawatumbua Mawaziri wa Viwanda kila uchao. Ningeshauri iundwe timu, Wizara ya Fedha, Wizara ya Viwanda, Wizara ya Uwekezaji, Wizara ya Kilimo, Wizara ya Ardhi na Wizara ya Mambo ya Nje kuangalia namna bora ya kuhamasisha wawekezaji kuja kuwekeza. Wizara ya Mambo ya Nje ina mchango mkubwa sana kwa sababu yenyewe ndiyo inayoliuza Taifa nje. Sasa kama Wizara ya Mambo ya Nje haitachukua lead, tukasema tunaachia Wizara ya Viwanda, kuna mahali tutashindwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kilimo sitazungumza mengi. Naomba ushauri unaotolewa na Wabunge kuhusu kilimo ufuatwe kwa sababu wananchi katika maeneo yote wanahangaika. Kilimanjaro ilikuwa mzalishaji mzuri sana wa kahawa aina ya arabica lakini sasa hivi imekwenda na maji. Wakulima wanang’oa kahawa, wanapanda vitu vingine. Sasa tujiulize tumekosea wapi, tuwasaidie, kama ni pembejeo, kama ni masoko, kama ni utafiti tuwasaidie kwa sababu asilimia 75 ya Watanzania ni wazi wamejiajiri katika kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo ningependa kulizungumza ni hili la pads. Nashangaa akisimama Mbunge mwanamke katika Bunge hili kuunga mkono hili pendekezo la Serikali halafu hatoi solution, nashangaa sana kwa sababu ni TWPG pamoja na wanawake wote humu ndani walileta hilo pendekezo katika Bunge lililopita. Sasa ni kweli hilo pendekezo halikuweza kuzaa matunda, lakini tuache hivi hivi na kama kuna mtu ana watoto wa kike na yuko karibu naye anafuatilia, atagundua mtoto wa kike akipewa mtihani wakati wa zile siku lazima atayumba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nasema hivi; sisi katika Kamati yetu ya Utawala tulishatoa agizo kwa Halmashauri zote kwamba hatuwezi tukaongea nao katika bajeti ijayo kama Mkurugenzi hatatuambia kwamba amenunua hizo pedi na kugawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tuliwapa utaratibu, tulisema kwamba ni lazima kila shule iwe na choo kizuri, iwe na chumba ambacho kitakuwa na sehemu ya kuhifadhi hizo pedi, iwe na dustbin ya kutupia na kadhalika. Sasa Wabunge wanawake nendeni kwa mtindo huo, kwa sababu sisi hatuwezi, wale watoto wanateseka. Watoto katika karne hii wa Kitanzania wanatembea na makanga machafu, wanajihifadhi kwa majani na kadhalika, halafu mtu anasimama hapa anasema hakuna cha bure! Sisi hatusemi mtoto wa Selasini apewe, sisi tunasema watoto wa maskini wapewe na kwa sababu wote wapo kwenye shule moja, basi watoto wanazipata pale shuleni na wala sio nyumbani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeshangaa mtu anasema kwamba anaweza akapewa akampelekea mama yake, kwanza akimpelekea mama yake so what? Si amesaidia, lakini vinginevyo, hili sio suala la kuzungumza. Naomba Mheshimiwa Waziri akae na Mwenyekiti wa Kamati ya TAMISEMI, sisi hili agizo tulishalitoa na katika Kamati yetu walipokuja katika Bunge hili kuna Halmashauri zilikuwa zinatupa ripoti kwamba sisi tumeshatekeleza by half, sisi tumeshatekeleza asilimia 100. Kwa hiyo kama hili la kodi linawashinda, tuchukue hili lingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo ningetaka niliseme kwa haraka haraka ni kuhusu TARURA, uamuzi tuliofanya wa TARURA ulikuwa uamuzi mzuri, lakini TARURA haina pesa na kwa sababu hiyo haiwezi kutekelezea miradi yake vizuri. Mwaka 2018/2019 katika Jimbo langu bajeti ilikuwa shilingi milioni 850, zimeenda shilingi milioni 550, wameweza kufanya miradi minne tu. Safari hii wamewaambia ceiling ni shilingi milioni 700. Wameniambia hawawezi kumaliza miradi viporo na wakafanya hata mradi mmoja.

Kwa hiyo, pamoja na kwamba najua kuna mikoa ambayo haijaunganishwa bado na lami kwa mfano Mkoa wa Kigoma na Mkoa wa Katavi, hilo jambo linaweza likafanyika, lakini kwenye bajeti ijayo waangalie namna ile Road Fund kuigawa labda TARURA half na TANROADS half baada ya kumaliza kuunganisha ile mikoa mingine ambayo bado haijaunganishwa, kwa sababu kwa mfano jimbo langu, ukanda wa juu wote ambao una volcanic soil, una mawe makubwa sana, TARURA hawawezi kufanya hiyo kazi. Kwa hiyo naomba hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hizi barabara ni muhimu sana, tunaweza tukajenga reli, tukajenga barabara za lami, sasa hizi feeder roads kama hazitajengwa ni shida na tulishawaaminisha wananchi wetu kwamba halmashauri inajenga. Kwa hiyo Madiwani na Wabunge wanalalamikiwa kumbe kuna chombo kinaitwa TARURA ambacho kinajenga…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)