Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kunipa nafasi ya kuchangia Wizara hii muhimu na bajeti ambayo kwa kweli kila mmoja ambaye ameisoma bajeti hii kwa kweli inagusa maisha ya Watanzania na imekuwa bajeti ya mfano.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru Mwenyenzi Mungu kwa kunipa afya na nguvu lakini pia nimpongeze Waziri Dkt. Mpango kwa kazi nzuri unayoifanya na tunakuombea kwa Mwenyezi Mungu azidi kukupa afya nikutie moyo kelele hizi unazozisikia kutoka kwa wenzetu usitegemee zitaisha, wewe unaposikia kelele ujue mambo yanakuwa mazuri songa mbele uendelee kuwatumikia Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti hii kwa jinsi ambavyo imeletwa kama tutaisimamia vizuri ninaamini uchumi wa Taifa letu unaenda kuinuka na tunaenda kuona mambo makubwa ambayo hatujawahi kuyaona katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, niiongelee kwa upande wa kilimo, pamoja na jitihada za Serikali bado hatuja wekeza nguvu kubwa ya kutosha kwenye kilimo. Nasema hivi kwa sababu tunataka kuingia kwenye uchumi wa viwanda ili viwanda vyetu viweze kupata nguvu kubwa lazima tuwe na malighafi ambazo zinapatikana katika nchi yetu, tusitegemee kupata malighafi ambazo zitatoka nje kuendeleza viwanda vyetu. Kwa hiyo, tujikite kwenye kilimo ambacho kitainua kwanza kipato cha Mtanzania na asilimia kubwa zaidi ya 80 ni wakulima, tukiwekeza kwenye kilimo kwa mfano wakapata mbegu bora wakawa na masoko ya uhakika, dawa na pembejeo ninaamini tunaweza uchumi wa Taifa letu ukainuka.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano Serikali imejikita kwenye mazao ya kimkakati ambayo ni korosho, pamba, chai, kahawa mazao haya tukiyasimamia ninaamini yanaweza yakainua kipato cha nchi yetu pia kipato cha mkulima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee suala la zao la kahawa ambalo tukilisimamia vizuri linaweza kuingiiza pesa nzuri na nyingi kwenye Taifa letu, lakini pamoja na kuondoa zile tozo ambazo zilikuwepo bado kahawa haijaweza kumnufaisha mkulima. Zao la kahawa siyo linalimwa Kagera tu zao la kahawa linalimwa maeneo mengi katika nchi yetu, niiombe sana Serikali ilisimamie.

Mheshimiwa Naibu Spika, hiki ni kitu cha kushangaza pale kwangu Kyerwa ukivuka tu mpaka hata ukiita wanasikia, ukivuka tu mpaka ukienda Uganda kahawa ni shilingi 2000 lakini ukija kwetu ni shilingi 1100. Ukienda kwenye nchi ya Rwanda kahawa ni shilingi 3000. Ninaiomba sana Serikali hawa wenzetu hii kahawa wanaiuza wapi tuangalie huko wanakouza kahawa na njia wanazotumia ili tuweze kuinua kipato cha mkulima lakini kipato cha Serikali yetu ninaamini hili litasimamiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye suala la kahawa kuna watu ambao mimi ninaamini bila kuingilia kati, Serikali ikaingilia na Waziri wa Kilimo angekuwepo hili akalisikia, kuna Bodi ya Kahawa, unasema unaunda Bodi ya Kahawa hii angelisikia kuna Bodi ya Kahawa, wewe unasema unaunda Bodi ya kahawa hii bodi inawakilisha wafanyabiashara hakuna mkulima hata mmoja ambaye anawakilishwa mnategemea hawa wakulima ni nani atakayewasemea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na vikwanzo vingi kwa mfano mwaka jana tulipata KDCU ambao ni Chama cha Ushirika walipata mteja kwa kununua kahawa lakini ilichukua siku 28 kutoa kibali, hii ndiyo bodi ya kahawa na ofisi ya Mrajisi. Mwaka huu tunatangaza msimu wa kahawa mwezi wa Tano mpaka sasa hivi bado kibali hakijatolewa na Benki ya Kilimo ipo tayari kutoa pesa imetenga zaidi ya bilioni 40, lakini bado ofisi ya Mrajisi haitoi kibali.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi ni vikwazo ambavyo haviwezi vikainua kilimo kwa sababu huyu mkulima anakata tamaa, lakini kama tukiondoa hivi vikwazo ambavyo vipo kwenye Tume ya Ushirika vipo kwenye Bodi ya Kahawa na vipo kwenye ofisi ya Mrajisi, nanaamini mkulima ataongeza kilimo na pato la Taifa litaongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine nnaipongeza sana Serikali kwa kuwekeza katika mradi mkubwa huu wa umeme, tunasema tunaingia kwenye uchumi wa viwanda hatuwezi tukaingia kwenye uchumi wa viwanda kama hatuna umeme wa uhakika. Hatuwezi tukawakaribisha wawekezaji kuja kuwekeza kwenye nchi yetu kama hatuna umeme wa uhakika. Kwa hiyo, naipongeza Serikali kwa maamuzi makubwa na mazito ambayo imeendelea kuyachukua.

Mheshimiwa Naibu Spika, mara nyingi Wabunge tulikuwa tunalalamika tunasema Serikali inashika huku, inashika huku haileti miradi ambayo inaweza ikasimamia sasa Serikali imekuja na miradi hii mikubwa nilitegemea kama Wabunge wote tuungane kwa pamoja tuiunge mkono
Serikali kuona hii miradi inakamilika, sasa hivi tunashauri, sasa Serikali ikifaya wenyewe tunageuka! Kwa kweli huu niseme ni kama uwendawazimu au ni kama uigizaji, tufanye mambo ambayo tunashauri Serikali, Serikali hii ya Chama cha Mapinduzi ni Serikali sikivu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kitu kingine watu walikuwa wanalalamika wanasema tumewekeza kwenye mradi wa Stigler’s Gorge. Huu mradi ninaamini tumekuwa tukilalamika Wabunge tunasema barabara zetu zinaharibika kwa sababu ya mizigo, huu mradi utakapokuwa umekamilika tunaamini barabara zetu zitakuwa salama na usafirishaji utakuwa mzuri kuongeza kipato cha Taifa. Tunaboresha bandari, bandari tunapoiboresha tunategemea mzigo tena ije ipite barabarani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niendelee kuipongeza sana Serikali kwa kazi hii inayofanyika, tusitegemee wenzetu kuwa watasifia kwa sababu yale ambayo walikuwa wanashauri ndiyo leo tunayoyafanya, kwa hiyo wamekosa hoja hawana jambo jingine ambalo wanaweza kuja nalo jipya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niipongeze sana Serikali na niiombe sana Serikali Mheshimiwa Waziri Dkt. Mpango bajeti hii kama ulivyoileta Mungu akuwezeshe uweze kuisimamia vizuri na ninaamini tunakoenda tunaenda kuzuri, Tanzania tunavyopiga hatua siyo kama Tanzania ya miaka 20 iliyopita na mtakuja kujionea wenyewe kwenye Uchaguzi Mkuu unaokuja uchaguzi wa Serikali za Mitaa na Uchaguzi Mkuu mtaona mambo makubwa ambayo Watanzania wanayaona wakati mwingine mnaweza mkafikiri Watanzania hawasikii, Watanzania wanasikia na wanaona mambo makubwa yanayofanyika katika Taifa hili na ndio maana kila kona tunakoenda Mheshimiwa Rais anaungwa mkono na Serikali yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya ninakushuru, ahsante sana.(Makofi)