Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi jioni hii ya leo na mimi kuchangia Bajeti Kuu ya Serikali. Kwanza niipongeze Serikali yetu kwa mambo makubwa ambayo imeyafanya, lakini nitatoa pongezi za kipekee kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Tunduru kwa ujumla kwa Serikali pamoja na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kutuokoa katika janga la korosho. Nitashukuru kwa sababu wakulima karibu asilimia 80 wamelipwa wamebaki asilimia 20; lakini nilitegemea katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri wakati amekuja angalau angezungumza jambo kidogo kuhusu suala la korosho, lakini bahati mbaya sikuiona, naomba nimkumbushe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, korosho ni zao la biashara upande wa Kanda ya Kusini, lakini ndio tegemeo kubwa kwa wananchi wa Kusini, nilikuwa naomba kati ya tozo ambazo umeziona zitolewe ningeomba na export levy kwenye korosho nayo iondolewe ili iweze kusaidia wakulima kwa sababu kwa sasa imeonekana export levy ni gharama kwa mnunuzi halafu ni mzigo kwa mkulima ambapo bei yake ya korosho inapungua. Tukiangalia kwa sasa hali tuliyokuwa nayo korosho kuwepo maghalani madhara ya kuwepo maghalani hapo mbele itakuwa ni makubwa, lakini kama tungeweza kutoa export levy ninaamini kuna wanunuzi ambao wangeweza kujitokeza kuweza kununua korosho zile kwa bei ambayo ingeweza kusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa kuwa gharama zetu ni kubwa ukiongeza mzigo wa export levy korosho zile mpaka sasa hivi wanunuzi waliokuwa wengi wanaziogopa na athari zake zitakuwa ni kubwa kwa sababu msimu ujao wa korosho unakaribia kuanza hapo mwezi wa nane jambo ambalo kutakuwa na madhara makuu mawili. La kwanza tutakosa mahala pa kuhifadhia korosho kwa sababu korosho nyingi zimejaa kwenye maghala ambayo ndio tunayoyategemea, kwa hiyo nilidhani katika mkakati wa Serikali wa awamu ijayo, moja ya mkakati ingekuwa ni kuongeza maghala katika maeneo ambayo yanazalisha korosho; lakini madhara ya pili wanunuzi wetu ni wale wa kila siku ambao ni Wahindi wa Vietnam ukweli wanajua tuna tani 224,000 kwenye maghala yetu, kwa hiyo, wataogopa kuja katika msimu ujao kununua korosho zetu kwa sababu wanajua kwamba korosho zikikaa zaidi ya miezi sita ubora unaendelea kushuka siku hadi siku. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba naongea hili kwa uzoefu nimekuwa General Manager zaidi ya miaka nane kwenye sekta ya korosho. Ninaijua korosho, naombeni sana Serikali kwa kuangalia hali ilivyo sasa basi tukubali bei itakayojitokeza tuuze zile korosho isije yakatokea yaliyotokea mwaka 2013/2014; jambo hili lilijitokeza na korosho tuliuza nusu bei, naomba sana Serikali iliangalie hili kwa kuangalia gharama zake ambazo zitasaidia korosho zile ziuzwe ili kunusuru msimu ujao korosho ziuzike kwa urahisi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo nilikuwa ninaomba kuna wananchi ambao wanadai mpaka leo, waliobaki walio wengi ni wale ambao ni wakulima wakubwa vijijini kwetu, hawana namna ya kuhudumia mikorosho, hawana namna ya kupulizia, basi kwa kuwa wanadai na Bodi ya Korosho wana pembejeo ambazo zipo kwenye maghala basi uwekwe utaratibu wa kuwakopesha wale wananchi pembejeo pindi Serikali itakapopata fedha basi waje kupunguza kwenye hayo mapato yao ili na wao waweze kuhudumia mashamba yao ili angalau mwakani nao waweze kuvuna zaidi. Jambo hili ni muhimu sana kwa sababu hawana namna kilio kimekuwa ni kikubwa sana, naomba sana Mheshimiwa Waziri uliangalie hili kwa upande wa huruma sana wale wakulima hawana namna yoyote ya kuweza kuwasaidia zaidi ya kuwakopesha pembejeo ili waweze kupalilia na kupulizia mikorosho yao.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine napenda niishukuru sana Serikali na kuipongeza kwa sheria ile ya mwaka 2005 ya mfumo wa stakabadhi gharani na ndio iliyoifanya korosho iongezeke uzalishaji mpaka mwaka 2017/ 2018 ukafikisha tani 3,13,000; lakini bahati mbaya yale yaliyojitokeza mwaka jana ambayo tuliyayalalamikia kwa muda mrefu uzalishaji umeshuka mpaka tani 224,000 na hii ilitokana na namna ambavyo tuli-handle pembejeo kwa wakulima wetu ambazo jambo tulilokuwa tumelilalamikia kwa muda mrefu, lakini halikutilia maanani.

Kwa hiyo, ninaomba sana ili kuongeza uzalishaji basi tupunguze gharama na miaka ya nyuma Serikali ilikuwa inatoa ruzuku kwenye pembejeo, nimesema nimekuwa kwenye korosho miaka nane, miaka ile Serikali ilikuwa inatoa ruzuku kwenye sulphur, ilikuwa inatoa ruzuku kwenye mbolea, lakini jambo lile limesitishwa naomba ile ruzuku irudie tena kwa wakulima ili waweze kununua pembejeo kwa bei rahisi na waweze kununua kwa wingi waweze kuzalisha zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mfumo ule wa Stakabadhi gharani tulisema tunaanza kwa mfano katika kanda ya korosho mafanikio yameonekana na hata sasa hivi upande ule tumeamua ufutwe kutumia mfumo wa stakabadhi gharani. Matokeo yake yamekuwa mazuri, bei imekuwa nzuri. naomba Serikali kwa kuwahurumia wakulima wa Tanzania ule mfumo ni mzuri uendelee kwenye maeneo mengine ya kahawa, pamba na tumbaku ili wakulima waweze kufaidika kama wenzao wa ufuta na korosho walivyoweza kufaidika miaka miwili, mitatu iliyopita. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Kengele ya pili imegonga Mheshimiwa.

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)