Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Saed Ahmed Kubenea

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Ubungo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii muhimu ya kuchangia hotuba ya Waziri wa Fedha ya Mapendekezo ya Bajeti ya Serikali. Kwanza niseme masikitiko yangu kwamba Mheshimiwa Waziri wa Fedha wakati anawasilisha hotuba yake hapa Bungeni, aliacha jukumu lake la msingi la kusimamia sera za Serikali juu ya bajeti akajikita kwenye ushabiki wa kushabikia Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Taifa letu ni Taifa changa sana na sisi wengine hatuna mahali popote pa kwenda, tumezaliwa hapa, tumekulia hapa, tumeishi hapa. Hatujawahi kwenda hata nchi za watu kuishi miaka mitano, miaka kumi, kwa hiyo hatuna mahali pa kwenda, bila kuheshimu utulivu wetu, amani yetu na busara zetu hakika Taifa hili tunaweza tukalipeleka mahali pabaya sana. Kwa hiyo Mheshimiwa Mpango jukumu lako kubwa ni kuisimamia Serikali juu ya mapato na kututoa hapa tulipo na kuachana kabisa na huu ushabiki wa kisiasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka huu wa fedha Serikali imetenga kwa mujibu wa hotuba ya Mheshimiwa Dkt. Mpango kwenye ukurasa wa 87 na 88 anasema; fedha ambazo zimetengwa kwa ajili ya maendeleo ni shilingi trilioni 12.25 ambayo ni sawa karibu na asilimia 37 ya bajeti. Ukiangalia kwenye hiki kitabu fedha karibu zote zimekwenda kwenye miradi isiyozidi minne,

wametaja hapa reli ya kati (standard gauge), umeme wa Mto Rufiji, REA na maji. Ili uchumi wetu uweze kukua tungewekeza katika kilimo, tungewekeza katika viwanda, tungewekeza katika umwagiliaji, lakini bajeti za Wizara hizo zote ziko chini ya asilimia tano ya bajeti yote. Sasa unajiuliza tunapojenga reli kutoka Dar es Salaam mpaka Dodoma, tumewezaje kuunganisha uchumi wa nchi na kule Congo - Lubumbashi ambapo Waheshimiwa Wabunge wa Kigoma wanapigania kwamba reli yetu iende? Unajiuliza hiyo mizigo tunaibebaje ikifika Dodoma tunaunganishaji uchumi wetu na nchi za nje? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nashangaa sana, nashangaa kwa sababu Mheshimiwa Dkt. Mpango kabla hajawa Waziri wa fedha alikuwa Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango na huu mpango wa miaka ishirini pengine umeandaliwa akiwa ofisini au alishiriki kuuandaa, miaka 25. Sasa leo anakuja na mpango mwingine kabisa wa umeme, na mimi najua kwamba nchi hii kipaumbele chake kikubwa ulikuwa umeme wa makaa ya mawe wa Linganga na chuma cha Mchuchuma, lakini kwenye bajeti nzima Serikali haizungumzi lolote juu ya Mchuchuma, haizungumzi lolote juu ya Liganga, haizungumzi lolote juu ya umeme wa gesi ya Mtwara haina kitu kabisa. Wanakuja na miradi mipya kila siku kitu kipya, kila siku kitu kipya, tunakwenda wapi! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nafikiri ni vizuri sana Serikali ikaangalia kwamba miradi ambayo tumeanza nayo mwanzo kama kipaumbele ifanyiwe kazi vizuri ili tusije tukawa tunakwenda kila mtu anakuja na kitu chake. Mheshimiwa Kikwete alikuja na umeme wa gesi hatujamaliza, hata gesi yenyewe hatujazalisha, hata deni hatujalipa leo tumeachana kabisa na gesi tunakuja na umeme wa maji. Huu umeme wa maji tuliuacha kwa sababu tulipata matatizo makubwa kwenye Kihansi, kwenye Nyumba ya Mungu, kwenye Mtera na Hale. Mabwawa yalikauka na Serikali ikalazimika kuingia kwenye mikataba na makampuni ya kufua umeme wa dharura, nchi ikaingia kwenye matatizo makubwa. Huu umeme wa Rufiji tunaofua hatuna uhakika kama mabadiliko ya tabia nchi hayataweza kutuathiri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nafikiri Serikali badala ya kuangalia miradi kwa pupa pupa, ifanye uchambuzi yakinifu kwa kila mradi ili tunapoenda kwenye mradi, tunapoingiza fedha za walipa kodi wa nchi hii kwenye miradi mikubwa lazima tuitekeleze. Hii bajeti ukiisoma yote, fedha za maendeleo zinategemea fedha nyingi kutoka nje na fedha za nje hazina uhakika wa kuzipata. Tayari wafadhili kwa mujibu wa Kamati ya Bajeti imesema haiweze tena kuchangia bajeti ya Serikali, inakwenda kujenga miradi moja kwa moja, ni kwa sababu hatuaminiki tena. Usimamizi wetu siyo mzuri wa miradi ya watu na tunakuja hapa baada ya kuwashukuru hawa wanaotupa fedha, tunawakebehi na kuwaita mabeberu, siyo jambo jema hata kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti inazungumzia uchaguzi mkuu ujao, bajeti inazungumzia uchaguzi wa Serikali za Mitaa. Hapa ni mahali pazuri kabisa muhimu pa kurejesha heshima ya nchi yetu na utulivu wa nchi yetu. Nchi yetu hii imewahi kuingia kwenye matatizo makubwa katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2000; mamia ya wananchi wa Zanzibar, wa Pemba walilazimika kuwa wakimbizi katika nchi yao. Nchi hii ambayo ilikuwa kimbilio la wakimbizi ikaacha ikazalisha wakimbizi kutokana na misingi mibaya ya kusimamia chaguzi zetu. Hata leo ukisoma matokeo ya uchaguzi yaliyotangazwa na Tume ya Uchaguzi mwaka 2015 ukachukua kura zote zilizotangazwa kwamba zimepigwa, ukachukua kura halali, ukachukua na kura ambazo siyo halali ukijumlisha kwa pamoja hazifungamani kabisa, ni mbingu na ardhi, na hata idadi ya iliyoandikishwa katika uchaguzi wa mwaka 2010 na waliopiga kura ni tofauti kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni muhimu Serikali ikaiboresha Tume ya Taifa ya Uchaguzi na ikaachana na hii biashara ya kukata rufaa kwa ajili ya Wakurugenzi wa Halmashauri walioondolewa na mahakama kusimamia uchaguzi. Kitendo cha kukata rufaa peke yake kimeonesha hila, kinaonesha nia mbaya iliyopo, kwa hiyo, ili tuondoke huko watu waweze kuaminiana, yaliyotokea Zanzibar katika uchaguzi wa mwaka 2015 yasijirudie tena katika uchaguzi ujao wa 2020. Tuipe uwezo Tume ya Uchaguzi ya kusimamia uchaguzi ulio huru na haki ili anayeshindwa huo uchaguzi aseme ahsante sana. Watu wapeane mikono, waache uhasama wa kisiasa, lakini kwa hii tabia ambayo Mheshimiwa Dkt. Mpango ameionesha humu Bungeni nachelea kusema nina hofu na uchaguzi ujao kwamba unaweza ukawa huru na haki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Taifa letu hili limejengwa na wazazi wetu kwa misingi imara kabisa ya demokrasia ya hali ya juu sana, na hili Bunge ndiyo chombo kikubwa kabisa katika Jamhuri ya Muungano cha kuonesha umahiri wetu katika demokrasia. Tusiposimama hapa tukataka Tume yetu ya Uchaguzi ikaendesha chaguzi yetu vizuri na haki, yaliyotokea kwenye nchi za wenzetu yalitokana na mambo haya haya ya kufanya uchaguzi kuwa usanii fulani na wananchi baadae wakakataa uchaguzi huo, tusifike huko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baadhi ya nchi za wenzetu za Afrika ziliingia kwenye matatizo makubwa baada ya Tume zao za Uchaguzi kufanya kazi za kisanii, leo Tume yetu ya Uchaguzi haiaminiki katika macho ya dunia. Wanatokea wenzetu wanatuambia boresheni haki za binadamu, boresheni demokrasia, utawala bora, tunawabazaza. Wakati hao wanaotuambia baadhi yetu tumeishi kwenye nchi zao miaka kumi, tumesoma huko, tumeishi huko, wametupa scholarship za kusoma kwao na kuishi kwao tunakuja tunawatukana, siyo haki hata kidogo. Uhusiano wetu na mataifa ya nje ungekuwa ndiyo huo unaombiwa hapa ndani ya Bunge hili hakika isingekuwepo miradi ya SIDA, isingekuwapo JICA, isingekuwa miradi ya Wajapani wala miradi ya Waingereza hapa nchi hii isingekuwepo, lakini imekuwepo kwa sababu tulisahau yaliyopita tukaganga yajayo na ndivyo nchi zote zinavyojengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda South Africa leo, kama Afrika Kusini wangekubali kurudishwa nyumba kwenye ubaguzi wa rangi nchi yao isingeenda pale. Ukienda Rwanda, kama Wanyarwanda wangekuwa wanakubali mauaji ya halaiki ya mwaka 1994 yawe kumbukumbu kwenye kichwa chao nchi yao isingefika hapo ilipoenda, lakini walisahau. Hata kama walitufanya watumwa, walitutawala, tuachene na hivyo vitu tusonge mbele kwa manufaa ya nchi yetu ili kile walichokichukua waweze kukirudisha hapa, kiweze kutusaidia kwenye maendeleo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo jambo la mwisho kabisa ni juu ya kodi ya pad ya kina mama ambayo Mheshimiwa Waziri wa Fedha ameiondoa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika,...

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa Kubenea, sekunde thelathini.

MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa utafiti uliofanywa na Shirika la UNICEF kati ya wanafunzi 10 wanaosoma shuleni mmoja ameacha shule kwa sababu ya kukosa taulo ya kujihifadhi. Badala ya Serikali ku-deal na wafanyabiashara ambao wananufaika na huo msamaha, wanakuja kuondoa kodi kwa watu wote, hili jambo sio sahihi na ninalipinga kwa nguvu zote. (Makofi)