Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Jerome Dismas Bwanausi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lulindi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. JEROME D. BWANAUSI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikushukuru kunipa nafasi na mimi nichangie kwenye bajeti yetu ambayo imewasilishwa kwa umakini mkubwa sana na Waziri wetu wa Fedha Mheshimiwa Dkt. Mpango na kwa kuanza tu niwatoe mashaka juu ya utendaji wenu wa kazi Dkt. Mpango na Naibu Waziri na mimi nataka niwape moyo kwamba ukiona watu wa upande wa pili wanawashambulia basi mjue mnafanya kazi nzuri, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba ya Mheshimiwa Waziri imejaa hali ya matarajio makubwa sana kwa Watanzania na sisi wote tunaunga mkono juhudi ambazo Serikali inazifanya chini ya uongozi wa Rais wetu Jemedari Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. Kwa hakika wananchi wengi wamekuwa na imani kubwa na bajeti ya mwaka huu hasa pale ambapo mlijikita sana katika kuhakikisha kwamba mnapunguza kodi mbalimbali, lakini kuweka utaratibu mzuri wa wafanyabiashara kutozwa pale TRA, kwa hiyo, mwaka huu mmeweka maelekezo mazuri ambayo wafanyabiashara wengi wameunga mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nijikite kwenye Serikali kwanza Serikali za Mitaa. Uongozi wa Serikali unaanzia kwenye kijiji na pia kwenye mtaa. Mimi niiombe Serikali, Wabunge wengi wamekuwa wakilalamikia juu ya kutoona umuhimu kwa sasa wa kuwalipa walau kifuta machozi Wenyeviti wa Vijiji, Vitongoji na Mitaa. (Makofi)

Mimi nataka niseme ni-declare interest kwamba ni nafasi ambayo niliitumikia niliwahi kuwa Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa pale Dar es Salaam, nimekuwa Diwani, nimekuwa Meya, hadi sasa nimekuwa Mbunge, hakuna nafasi ngumu kuiongoza kama ya kuwa Mwenyekiti wa Kijiji au Mwenyekiti wa Mtaa. Kwa hiyo kwa kweli ningeomba sana kama haiwezekani kuwapa hizo posho kila mwezi basi tunapofika mwisho wa kipindi cha miaka mitano nafasi hii ifikiriwe kama wanavyofikiriwa Madiwani na wanavyofikiriwa Wabunge walau wanapata chochote kutokana na kazi waliyofanya katika miaka mitano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nije pia katika suala zima la umuhimu wa afya ya Watanzania; kwanza niipongeze Serikali ya Awamu ya Tano ya Dkt. John Pombe Magufuli kwa jinsi ambavyo imesaidia sana kwenye sekta ya afya. Tumejenga vituo vya afya zaidi ya 350, tumejenga hospitali zaidi ya 67 sasa hivi na bado mahitaji yapo ni makubwa. Mimi niiombe tu Serikali sasa pia ielekeze katika maeneo mahususi ambayo huduma hii ya afya inahitajika sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikienda kwenda jimbo langu pale Jimbo la Lulindi Wilaya ya Masasi kuna maeneo mawili ambayo yanahitaji kwa kiasi kikubwa sana Serikali itazame macho kuwapelekea kituo cha afya na maeneo hayo ni Mnavira pamoja na Kata ya Lipumburu. Kata ya Mnavira iko mpakani mwa Tanzania na Msumbiji, eneo hili limekuwa likikubwa na matukio mbalimbali ya wananchi kupoteza maisha, lakini kupoteza viungo kutokana na wimbi kubwa la mamba ambao mara nyingi nimekuwa nikilisema ndani ya Bunge. Hivyo wakipata majeraha wengi wanapoteza maisha kwa sababu kutoka Mnavira hadi kufika kwenye Hospitali ya Wilaya ni kiometa 50 kufika Masasi Mjini, kwa hiyo, pale panahitajika na bahat nzuri wananchi wa pale pamoja na Halmashauri imejitolea kujenga Jengo la OPD. Kwa hiyo, majengo mengine tu yaliyobaki ili pale pawe na kituo cha afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hali kadhalika kwenye ile Kata ya Lipumburu ambayo pia ndio kata ambayo Mheshimiwa Rais Mstaafu Benjamin Mkapa anatoka kwa kweli lile eneo linahitaji kuwa na kituo cha afya ambacho kitahudumia kata ile ya Lupaso pia na Kata ya Lipumburu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni suala la ukusanyaji wa mapato ya property tax. Bahati nzuri mimi nilishuhudia wakati nilipokuwa kwenye ngazi hizi zingine za Serikali za Mitaa jinsi ambavyo Halmashauri tulikuwa tunafanya vizuri katika ukusanyaji wa property tax. Lakini baada ya kuchukua TRA naona kama kuna hali ya kushuka kwa kiwango cha ukusanyaji wa kodi hii. Mimi niseme tu wananchi wapo tayari kabisa kulipa lakini mamlaka zinazopewa kazi hii ya ukusanyaji haziko makini katika kuhakikisha zinafuatilia suala hili la kodi ya majengo, ni sehemu ambayo likizingatiwa tutapata kipato kikubwa na kuisaidia Serikali kutimiza wajibu wake katika maeneo mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo nilitaka niliseme ni juu ya suala zima la umuhimu wa mitandao na ujenzi wa minara katika maeneo yetu. Serikali kwa muda mrefu imekuwa ikisema kwamba kama kuna maeneo muhimu ya kuhakikisha minara inajengwa ni mipakani yaani kati ya nchi na nchi na mimi jimbo langu linapakana na Msumbiji. Lakini hadi sasa hivi ninavyosema wananchi wa maeneo yangu ya Nanyemyo, Mnavira, Chipolopola, Sindano wanatumia mitandao kutoka Msumbiji. Kwa hiyo, mimi ningeomba sana Serikali kwamba badala ya wananchi kwenda kununua vocha za mitandao ya Msumbiji basi fedha zile zingetumika kununua mitandao ya hapa nchini na kuiingizia mapato Serikali yetu. Kwa hiyo, naomba sana Serikali ihakikishe kwamba maeneo haya ya mipakani ambayo Serikali ilishaeleza umuhimu wa kujenga minara hiyo iweze kujengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo ningeomba sana ni kwamba bahati nzuri tuna Daraja la Umoja kati ya Tanzania na Msumbiji, lakini eneo kubwa la kiuchumi ambalo linafanya biashara kati ya Msumbiji na Tanzania halipo kwenye eneo lile ambalo daraja limejengwa. Ningeomba sana Serikali tunapoteza mapato mengi sana kutokana na jinsi ambavyo hatuzingatii suala la ukusanyaji mapato katika nchi ya Tanzania na Msumbiji. Vifaa vingi vinatoka Msumbiji kuingia hapa lakini hakuna ushuru wowote uliotolewa. Pia Serikali iangalie kwamba uwepo uwezekano wa kujenga daraja lingine pale Mtwara maeneo ya pale Chilambo ambapo tukijenga daraja lile pale tutaweza kudhibiti kwa kiasi kikubwa sana mapato kati ya Tanzania na Msumbiji. (Makofi)

Kwa hiyo, hili jambo ningeomba sana sana Serikali ilitazame kwa macho mawili kuhakikisha kwamba tunapata mapato kutoka Msumbiji kama tulivyopata mapato kutoka nchi zingine zinazopakana na Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nilikuwa na mchango huo na najua muda ni mfupi kwa hiyo naunga mkono bajeti hii kwa asilimia mia moja. (Makofi)