Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kupata fursa hii ili niweze kutoa mchango wangu kwenye hotuba ya bajeti iliyosomwa na Waziri Dkt. Mpango. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuanza nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote katika Wizara hii kwa kutuletea hotuba nzuri inayoonesha muelekeo mzuri wa nchi yetu kiuchumi na kazi kubwa inayofanywa na Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hotuba hii imezingatia mambo mengi ambayo tumekuwa tunashauri, mambo mengi ambayo yamekuwa yanaleta kero kwenye jamii hotuba hii imezingatia kwa hiyo kwa moyo wa dhati kabisa nimpongeze Mheshimiwa Waziri na timu yake kwa kazi kubwa sana ya kuandaa hotuba hii nzuri. Jukumu letu sasa nikushauri maeneo machache ambayo tunafikiri yanatakiwa yafanyiwe marekebisho au yaongezwe kwa ajili ya kuboresha kile kilichowasilishwa kwetu. Kwangu mimi nitajikita kwenye maeneo makuu mawili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri, uchumi wetu unaonesha kupanda na kwa mujibu wa takwimu hizi, uchumi wetu sasa umekuwa kwa asilimia saba na asilimia saba hizi zimetokana na sekta mbalimbali za kiuchumi ambazo zimekuwa zinafanya vizuri.

Mheshimiwa Spika, katika sekta zilizofanya vizuri ni sekta ya kilimo ambayo kwa ukuaji wake ni sekta ya nne kwa kukua, lakini kwenye eneo hili, sekta hii ya kilimo kama inavyoonekana imekua kwa asilimia 5.3 na tunatambua sekta ya kilimo ni sekta inayojumuisha watu wengi, inaajiri watu wengi na kama tutaiwekea mkazo inaweza kuongeza kwa kiwango kikubwa sana ukuaji wa uchumi wetu kama Taifa na kwenye eneo hili la kilimo likijumuisha uvuvi, mifugo na kilimo chenyewe bado hatujawekeza sana kwenye sekta hii ya kilimo. Kwa mfano, tukiangalia kwenye sekta hi, tukijumuisha uvuvi, mifugo na kilimo chenyewe kwa ujumla wake aukiangalia sehemu ya uvuvi ndiyo imechangia sehemu kubwa sana karibu asilimia tisa, lakini eneo hili la uvuvi ambalo linaajiri watu wengi sana bado kuna vikwazo vingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeona kwa mujibu wa hotuba kuna maeneo mengi hasa kwenye eneo la uvuvi ambako tozo nyingi zimeondolewa, lakini bado kwenye sekta ya uvuvi yenyewe bado kuna tozo nyingi sana ambazo zinawafanya wanaoshiriki kwenye shughuli za uvuvi wasiweze kufanya vizuri sana na kuchangia pato la Taifa. Kwa hiyo, bado ni muhimu sana Serikali iliangalie hili. Niombe Mheshimiwa Mpango uangalie namna gani tunaweza tukaifanya sekta ya uvuvi ikachangia sehemu kubwa sana ya pato letu na tukiangalia kwa mfano kwenye mazao ya kilimo, kwenye bidhaa tulizouza nje kutoka bilioni 790 mwaka huu tumeuza zaidi ya trilioni moja ya mazao, lakini tunaweza tukafanya vizuri zaidi kama tutaboresha sekta ya uvuvi na wakafanya kazi vizuri, bila vikwazo vingi na tukaweza kuuza mazao mengi nje.

Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri niombe sekta ya uvuvi vilevile iangaliwe, tozo wanazokutana nazo wavuvi ni nyingi sana ziweze kuangaliwa kama zilivyopunguzwa kwenye eneo la mifugo, sekta ya uvuvi vilevile zipunguzwe kwa sababu kama tunavyojua vijana wengi wanaajiriwa kupitia sekta hii ya uvuvi kwahiyo kakam tozo hizi zitapungua wataweza kujiajiri, watafanya shughuli zao lakini uzalishaji utakuwa mkubwa zaidi na kuwezesha Taifa letu kuweza kuuza kwa ukubwa snaa mazoa ya uvuvi nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini niongelee eneo la kilimo; kwa mujibu wa tafiti mbalimbali, kilimo kinaajiri zaidi ya nusu ya wananchi wa Tanzania na sehemu kubwa tunayouza nje yanatokana na kilimo. Tunaelekea kwenye uchumi wa viwanda, bila kuboresha eneo la kilimo hatutaweza kufikia kwa ufanisi kwenye uchumi wa viwanda, kwa hiyo, ni lazima tuwekeze wka kiwango kikubwa sana na kwa dhati kwenye kilimo hasa kilimo cha kisasa, kilimo cha umwagiliaji. Bahati mbaya sana tuna eneo zuri sana, eneo kubwa tukilinganisha na mataifa mengine yanayotuzunguka. Juzi tumemuona Mheshimiwa Rais amefanya ziara nje, watu wengi sana wanaotuzunguka wanahitaji chakula kutoka nchini kwetu. Sawa, tunaweza tukawapelekea chakula, lakini tuna uwezo wa kuzalisha zaidi na zaidi tukaweza kuza chakula kingi sana na tukaipatia nchi yetu pesa za kutosha sana za kigeni, lakini kilimo tunachokifanya bado ni kilimo cha kawaida sana cha mazoea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninachoweza kushauri ni muhimu tuangalie, tuangalie comparatively maeneo tuliyonayo. Kwa mfano, Kanda ya Ziwa inalimwa pamba, Nyanda za Juu Kusini wanalima mahindi, kuna eneo wanalima mpunga, tunaweza tukatenga kwa mfano, eneo la Kilombero ihawa hub ya kuzalisha mazao kwa mfano ya mpunga, eneo la Nyanda za Juu Kusini ikawa eneo maalum kwa ajili ya kuzalisha mahindi, eneo la Kanda ya Ziwa ikawa eneo maalum kwa ajili ya kuzalisha pamba, Serikali ikaangalia ni watu gani ambao wanaweza wakatusaidia kuzalisha mazao haya, tukawekeza kwenye maeneo haya tukiamini kwamba namba kadhaa ya watu Serikali ichukue jukumu la kuwawezesha kimkakati na kuweka malengo kwamba watu hawa Serikali inawawezesha wazalishe kiasi fulani cha mazao ili sasa mazao haya na wati huo Serikali ikiwaandalia masoko waweze kuzalisha mazao haya na vilevile wakiwa na uhakika wa masoko yao. Tukifanya hivyo kwa miaka miwili, mwaka mmoja, miaka mitatu tunaweza tukawa na uzalishaji mkubwa sana wa mazao mbalimbali ya kimkakati na Taifa letu likaweza kuuza mazao mengi nje na kuweza kuisaidia Nchi yetu kiuchumi.

Mheshimiwa Spika, tuynatambua kwamba kupanda kwa uchumi wetu kumechangiw ana stabilization ya bei ya mazao ya chakula lakini vilevile inflation rate kuwa stable, lakini yote haya yanawezekana tu kama tunaweza kuwa na chakula cha kujitoseheleza ndiyo tunaweza tukafikia hapa.

Kwa hiyo ningeomba sana Serikali iangalie na hasa Mheshimiwa Waziri tuone namna gani tunaweza tukafanya kilimo cha kimkakati badala ya kulima kilimo cha kawaida tu kila mmoja analima jinsi anavyojisikia hatutaweza kufikia malengo yale tunayoyatarajia.

Mheshimiwa Spika, lakini eneo lingine ambalo nilitaka nichangie…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa Joseph bahati mbaya ni kengele ya pili.

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)