Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia Bajeti hii ya Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nataka kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kuwa hapa kujadili suala hili muhimu sana, lakini vilevile napenda sana kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha - Dkt. Mpango na Naibu wake - Dkt. Kijaji, lakini vilevile Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara ya Fedha na wadau wote waliotufikisha katika kupata bajeti kama hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti hii kwa kweli ni nzuri sana, naipongeza sana kwa sababu kama walivyosema wenzangu imezingatia maoni mengi ambayo Wabunge na wananchi wamekuwa wakiyatoa kwa muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii bajeti moja kwa moja inaenda kusaidia sana yale masuala mazima ya mazingira ya kufanya biashara au ya uwekezaji katika Taifa letu. Tozo nyingi zilizokuwa kero na ambazo zimesababisha wafanyabiashara kushindwa kufanya kazi vizuri kwa ufanisi zimepunguzwa na zingine zimeondolewa kabisa, tunapongeza sana kwa hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kuanza kuzungumzia suala moja ambalo limekuwa kama lina chukuliwa kwa upotoshwaji wa kiasi kikubwa sana nalo ni lile la kusema kuwa Awamu ya Tano Serikali imekuwa ikifanya miradi nje ya utaratibu, nje ya bajeti, nje ya mipango, hiyo si kweli na nafikiri wanaofanya hivi aidha wana nia ovu au hawaelewi! (Makofi)

MBUNGE FULANI: Hawaelewi.

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Naibu Spika, tumekuwa tuna dira ya maendeleo ya 2025 ambayo imeanza kutumika tangu mwaka 2000, kwa bahati nzuri mimi mmoja wapo kati ya watu ambao tulikuwa tunahusika moja kwa moja katika kuitayarisha nikiwa Umoja wa Mataifa na wako wengine humu ndani, hata Dkt. Mpango mwenyewe alikuwa anahusika nafikiri akiwa aidha World Bank au akiwa Tume ya Mipango sikumbuki vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hiyo dira imeainisha malengo makuu ya maendeleo yetu tunavyotaka kuyapeleka tangu wakati huo mwaka 2000, kati ya malengo matano makuu ambayo ndiyo hayo sasa yameletelezea kutengeneza mipango yetu ya maendeleo ya miaka mitano mitano hadi 2025, wa kwanza ilikuwa kuboresha hali ya maisha ya Watanzania kwa maana ya kuondoa umaskini; ya pili ilikuwa ni kuwepo kwa mazingira ya amani, usalama na umoja; ya tatu ilikuwa kujenga utawala bora; ya nne ni kuwepo jamii iliyoelimika vyema na inayojifunza na ya tano ilikuwa kujenga uchumi imara unaoweza kukabiliana na ushindani kutoka nchi nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nataka kuuliza katika mipango yote hii inayofanywa Awamu kwa Awamu ni upi ambao uko nje ya mikakati hii ya malengo haya? Hakuna na zaidi ya hapo pamoja ya kuweka malengo haya, tuliweka vilevile utekelezaji wake utakuwaje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tulipanga kabisa tutaanza na nini, tutamaliza na nini, na systematically tumekuwa tukifanya hivyo, tumeweka kwanza mikakati ile ambayo itawezesha malengo haya kutekelezwa, tukaweka namna ya kufikia mikakati hiyo, tukaweka jinsi ya kutathmini tumefikia wapi na tunaendelea kurekebisha kadri tunavyokwenda. Sasa kwenda kuwaambia wananchi kuwa oooh, Stiegler’s Gorge sijui imetoka wapi, haijulikani hata ilikotokea, ooohh sijuii hii, hii Strategic Railway imetokea wapi siyo kweli, nendeni kwenye documents za Serikali hii miradi yote ipo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunachoweza kusema sasa nakushauri Serikali ni kuwa kwanza itekelezwe kwa wakati, kwa sababu tunachelewa, kama nchi tunachelewa, tumeambiwa tunatakiwa tushindane na nchi nyingine, hatuwezi kushindana bila kuwa na miundombinu ya kimkakati kama hii, hatuwezi kushindana kama hatuna sera zinazoweza kuongoza biashara zetu zifanyike vizuri, hatuwezi kushindana kama hatuwezi kuboresha mazao yetu na kuyauza katika masoko ya ndani na ya nje, sasa hivi vyote ni vitu ambavyo vinafanywa na Serikali kwa ajili tu ya kuhakikisha kuwa tunafika kule tunakokwenda kufuatana na dira yetu ya maendeleo ya 2000/2025. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nataka kusema tu wananchi wetu wa Tanzania wapuuze upotoshwaji huu unaofanywa, aidha, ni kwa makusudi au kwa kutokuelewa, lakini baada ya kusema hayo naomba sasa niingie katika suala zima la bajeti yenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naipongeza Serikali kwa kuangalia sasa yale mambo ambayo sisi tumekuwa tukiyalalamikia sana hasa yale ambayo yanahusu uendeshwaji wa biashara au uwekezaji nchini. Ni kweli Serikali imetambua kama kuna mambo mengi ambayo yamekuwa hayaendi vizuri na wakachukua hatua za kurekebisha. Kuna suala ambalo limezungumzwa hapa la tozo, tunafurahi sana kwa tozo nyingine zimeongezwa ili kulinda viwanda vya ndani, tozo nyingine zimeondolewa ili kuhakikisha kuwa ufanisi unapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa ninaomba Serikali iende mbali zaidi, unaweza ukatoa tozo au ukaongeza tozo ya mali inayoagizwa kutoka nje ili kiwanda cha ndani kichangamke au kifanye vizuri zaidi. Lakini bila kuangalia vile vikwazo na changamoto ambazo vinaathiri vile viwanda vya ndani kukua au kufanya kazi kwa ufanisi, tukajikuta sasa tumesababisha upungufu wa bidhaa kwa sababu bidhaa za ndani hazizalishwi. Je, Serikali imetazama hayo? Tunapozungumzia bidhaa kwa mfano za kilimo na uchakataji mazao, tumeangalia sasa uwezo wa viwanda vya ndani kuchakata mazao ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kutoa mfano mdogo tu kwa Mkoa wangu wa Songwe, tunazalisha sana mazao mengi ya kila aina na hivi karibuni tulituma ujumbe DRC Congo kutafuta soko. Wakatuhakikishia kuwa wao wanaweza kununua unga mwingi sana kutoka kwetu, unga wa mahindi na mchele. Tulivyorudi Mkoa wa Songwe tukajikuta kuwa hatuna viwanda vya kutosheleza ile order ambayo watu wa Congo wanaitaka, sasa hiyo ni changamoto. Kwa hiyo, unaposema labda unaondoa hivi kurahisisha viwanda vya ndani na bila kuangalia kama viwanda vya ndani vimewezeshwa ipasavyo tunaweza tukajikuta tumekwama.

Mheshimiwa Naibu Spika, hali kadhalika tukija hata kwenye hata hizi taulo za kike, tunaipongeza Serikali kuwa imegundua kuwa ile tozo lililokuwa limeondolewa ilikuja kunufaisha wafanyabiashara lakini taulo zile ziliendelea kuuzwa kwa bei ile ile ya zamani. Dawa kweli ni kuhakikisha kuwa tozo inarudi, lakini tozo inarudi, viwanda vya ndani vitaweza kuzalisha taulo zile za kutosha ili kufidia pale ambapo tunakosa na vilevile kwa bei ambayo itakuwa nafuu? Kwa sababu ilionekana pamoja na hayo bado bei ya zinazoagizwa kutoka nje ilikuwa ni bei ya juu.

Kwa hiyo, tulikuwa tunataka sana tuangalie zile malighafi zinazoingia katika kutengeneza zile taulo za kike zinaweza kuwa siyo pamba peke yake, kuna kile kitambaa cha kuhifadhia ambacho ndiyo kinasababishia ile taulo kuwa taulo jinsi inavyoitwa, tunacho sisi hapa Tanzania? Kama kinaagizwa, je, Serikali iko tayari kuondoa sasa tozo kwenye hiyo kwa ajili ya viwanda vinavyotengeneza hizo taulo za kike ili mwisho wa siku watoto wetu waweze kupata hizo taulo kama wanavyohitaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakwenda mbio, hiyo ni kwa bidhaa nyingine zote ambazo zimewekewa tozo. Kwa mfano viberiti, dawa za meno, chuma kwa ajili ya misumari, sausage, peremende, chewing gum, chocolate, biscuits, maji. Kwa nini tumeongeza ushuru kwenye maji ya kunywa ilhali tunajua maji tuliyonayo Tanzania bado hatuna uhakika wa usalama wake kutokana na miundombinu ya maji bado haijatengemaa. Kwa hiyo, tulitaka Serikali itusaidie kuangalia hizi tozo ambazo nyingine zimeongezwa nyingine zimetolewa, je, zinatosheleza kKuhakikisha kuwa viwanda vyetu sasa vitaweza kuzalisha ili tupate bidhaa ndani ya nchi zinazotokana na viwanda vyetu kwa uhakika, kwa wakati na zenye ubora unaohitajika?

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala zima la kilimo, hili litaendelea kujirudia kwa sababu ndiyo uti wa mgongo. Tunapozungumzia uti wa mgongo, kweli kilimo ni uti wa mgongo. Hebu Serikali iangalie sasa jinsi ambavyo itaruhusu kilimo cha kisasa, kilimo cha kibiashara, cha wakulima wakubwa, kwa kuweka urahisi kwao kuwekeza katika nchi yetu. Tuna ardhi nzuri sana, tuna mvua nyingi sana lakini wawekezaji wakubwa wa kilimo hawaji, kwa nini? Ni kwa sababu bado hatujaweka mifumo mizuri ya kuwapa uhakika wao kuwekeza na bila kusumbuliwa baada ya kuwa wamewekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna mabonde mengi ambayo tunaweza tukalima mpunga, tunaweza tukalima ngano kwenye maeneo ambayo yanalima ngano, tuna maeneo mengi ya kilimo cha kila aina mboga mboga, lakini kwa nini hatuwekezi vya kutosha. Kwa sababu bado kuna changamoto...

NAIBU SPIKA: Muda wako umekwisha Mheshimiwa, ahsante sana.