Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. George Boniface Simbachawene

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibakwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. GEORGE B. SIMBACHAWENE: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali na nimpongeze sana Waziri wa Fedha na Mipango na Naibu wake, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na watendaji wote wa taasisi zote zilizopo chini ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa kazi nzuri wanayoifanyia taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, unapojenga uchumi wa nchi kama ya kwetu, ambayo zipo falsafa tofauti, wengine wanaona tunakimbia, wengine wanaona tunachelewa, wengine wanaona tunakosea na wengine wanaona tunapatia, ni lazima uwe na msimamo ili kuweza kufanya unayofikiria kufanya na hasa kama umepewa dhamana ya haki na halali ya kuongoza nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Chama cha Mapinduzi kimepewa dhamana hii kwa kushinda uchaguzi na Chama cha Mapinduzi ndicho kinachoshika historia ya nchi hii kwa sababu ndicho kilichoongoza nchi hii toka tulivyopata uhuru. Tunafahamu wapi tulipotembea tukaona mabonde, tunafahamu wapi tulioona kuna miteremko mikali na tunajua namna ya kushika brake au kuongeza mwendo. Niwasihi na niwaombe wenzetu waliopo humu na Watanzania kwa ujumla waunge mkono jitihada hizi nzuri zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunajaribu kutekeleza miradi ambayo ilikuwa haijaweza kutekelezwa tangu katika mipango ya kwanza kabisa tulipopata uhuru, leo inafanyika. Tunafanya miradi mikubwa ambayo inajenga msingi wa uchumi wa nchi kwa ajili ya vizazi vyetu vijavyo, siyo kwa ajili ya sisi. Ukijenga reli, haujengi kwa ajili ya sisi leo na kwa hiyo, hata ukikopa hatukopi kwa ajili yetu sisi, tunakopa kwa ajili ya watoto na wajukuu zetu na kukopa si dhambi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo tunajenga mradi mkubwa wa kuzalisha umeme wa Stiegler’s Gorge ambao hata tukikopa si kwa ajili ya sisi tu tunaoishi leo, ni kwa ajili ya vizazi vijavyo. Ni muhimu katika kuangalia hii mikubwa ikiwemo ya ufufuaji wa Shirika la Ndege kwa sababu ipo miundombinu muhimu ikiwemo barabara, ujenzi na huduma za afya, haya yote yanafanyika kwa gharama kubwa lakini pia uwekezaji kwa watoto wetu katika kutoa elimu bure ni mambo makubwa ambayo yakifanyika leo yana maana sana kwa kizazi kijacho kuliko sisi tunaoishi leo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, limezungumzwa hapa suala la kukopa na pengine nianze na hili ambalo Mheshimiwa Zitto amelisema juu ya masuala ya mamlaka ya fedha.

Mheshimiwa Zitto ukiisoma Katiba Ibara ya 99 unayaona mamlaka ya Rais katika masuala ya fedha pia. Sasa lazima usome zote mbili na kwa sisi wanasheria huwa tunazisoma ili tuweze kujua kama sheria hizi zinasomeka kwa pamoja au zinaenda mutatis mutandis au zinaenda kwa kupingana. Ninachokiona hapa ni kwamba hiyo uliyoisoma lazima uisome pia na Ibara ya 99. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Ibara ya 99 inasema hivi; “Bunge litashughulikia jambo lolote kati ya mambo yanayohusika na ibara hii isipokuwa kama Rais amependekeza kwamba jambo hilo lishughulikiwe na Bunge na pendekezo hilo la Rais liwe limewasilishwa kwenye Bunge na Waziri. Na mambo yanayohusika na Ibara hii ni haya yafuatayo; Muswada wa Sheria kwa ajili ya lolote kati ya mambo yafuatayo; kutoza kodi au kubadilisha kodi kwa namna nyingine yoyote isipokuwa kupunguza.”

Sasa katika madaraka haya na ukisoma na hizi nyingine ni lazima uisome na hiyo. kwa hiyo, kuamua kuwatambua Watanzania wakajulikana kwa shughuli wanazozifanya ili waweze kupata msaada wa Serikali labda lingehojiwa msaada wa Serikali uko wapi dhidi ya hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mimi nasema…

MHE. KABWE Z. R. ZITTO:Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Simbachawene pokea taarifa.

T A A R I F A

MHE. KABWE Z. R. ZITTO:Mheshimiwa Spika, naomba Mheshimiwa George Simbachawene, Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti aangalie taarifa ya Kamati ambayo yeye mwenyewe ameiongoza ambayo imesomwa hapa Bungeni ukurasa wa 27 aya ya 4.1 kuhusu namna ambavyo mamlaka zinajiamulia kukusanyakusanya mapato bila consultation ya Wizara ya Fedha na Bunge hili kuleta sheria, arejee katika hilo kabla hajanijibu mimi ndiyo atajua kwamba nilichokuwa nakiongea mimi ni kile ambacho kamati imeleta hapa.

SPIKA: Mheshimiwa Simbachawene unapokea hiyo taarifa?

MHE. GEORGE B. SIMBACHAWENE: Mheshimiwa Spika, anavyoitafsiri ni tofauti, tumezitaja kabisa; tumesema Wizara, taasisi/mamlaka ya mikoa na wilaya. Ni kwa sababu ya vile vikodi/vitozo vidogo vidogo ambavyo vinahitajika kwa mujibu wa sheria Serikali i-coordinate siyo kila mamlaka itoke na kodi/ tozo yake, zinaleta shida na kero kwa wananchi na huu ndiyo ulikuwa ushauri kwa Serikali na bahati nzuri Serikali ilishaupokea ushauri huu kutoka kwenye Kamati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa nini tunakopa leo? Lakini pia lazima nieleze ipo tofauti kati ya Deni la Taifa na Deni la Serikali; hapa tunachanganya mambo. Deni la Serikali ni lile ambalo Serikali imekopa kwa mujibu wa Sheria ya Mikopo, Misaada na Dhamana na lina utaratibu wake. Haiwezekani ikasemekana eti halieleweki, sheria ipo inakuwaje deni liwe halieleweki? Deni la Serikali linaeleweka vizuri kabisa ingawa Serikali pia ina udhibiti wa Deni la Taifa lakini Deni la Taifa linahusisha pia mikopo ya sekta binafsi. Kwa hiyo, lazima kuelewa namna ya ku-balance, isijeikachukuliwa yote kwa ujumla wake halafu ikawachanganya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, inadaiwa hapa kwamba eti sisi tunakopa sana na pengine deni hili limeongezeka. Madeni tunayolipa leo kama nchi yalikopwa toka awamu ya kwanza ya uongozi wa nchi hii, kwenye ule mkeka yapo madeni na Kamati yako iko well informed. Vipo vitu tunavipata kule na mimi namshukuru Mungu kuwepo kwenye Kamati hii nimejifunza mambo makubwa ambayo nilikuwa siyajui. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, madeni tunayolipa leo ni ya miaka ya 1980, 1990 yaani ya siku za nyuma ndiyo tunalipa leo na haya tunayokopa sisi yatalipwa huko mbele, lakini lazima tuhakikishe tunakopa kwa ajili ya kitu gani. Sasa tunapokopa kwa ajili ya reli ambayo watoto wetu wataikuta kwa miaka 100 ijayo, tunapokopa kwa ajili ya kuzalisha umeme ambao wajukuu zetu wataukuta, kuna ubaya gani! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukopaji una uwiano wake na uwiano muhimu ni kipimo cha debt to GDP ratio. Deni ukilinganisha na GDP (Pato la Taifa), kwa mfano Tanzania nilishanishe tu kidogo, Marekani debt to GDP ni asilimia 106.1; Kenya debt to GDP ni asilimia 52; Zambia debt to GDP ni asilimia 54; Ugiriki debt to GDP ni asilimia 179 yaani GDP yao inaingia kama mara mbili na zaidi, lakini Tanzania debt to GDP yetu ni asilimia 32, tupo chini ya wengine wote. Kwa hiyo deni letu ni himilivu, tena bado tuna nafasi ya kukopa ili tuweze kuwekeza, cha msingi ni kuwekeza kwa ajili ya watoto wetu na wajukuu zetu na vizazi vijavyo, hicho ndicho cha msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yamesemwa mambo hapa…

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. DAVID E. SILINDE: Achana nae unapoteza muda.

SPIKA: Mwakajoka nini tena? Maana yake hiyo shule…

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Spika, unajua amejisahau…

SPIKA: Ngoja kidogo, subiri, hujaruhusiwa bado.

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Unasikia mzee amejisahau anasema kwamba…

SPIKA: Hujaruhusiwa kwanza, nitakupa nafasi.

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Aah sorry.

SPIKA: Usiwe unaongea kabla hujapewa nafasi. Nilikuwa nasema kwamba shule hii inayotolewa na lawyer kwa Zitto economist ilitakiwa...; Mheshimiwa Zitto ni Mwakajoka amesimama kwa hiyo…, Mwakajoka nakupa dakika moja. (Makofi/Kicheko)

T A A R I F A

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Spika,mimi nampa taarifa Mheshimiwa Mbunge anayezungumza kwamba anazungumza kama Waziri, ajue kabisa kwamba sasa hivi ni Mbunge wa kawaida, kwa hiyo, anatakiwa kutoa michango yake. (Makofi)

SPIKA: Aah! Yaani kwa kweli umechezea wakati wangu, hapa wanaongea professionals na Mwakajoka hujawahi kuniandikia professional yako ni nini hasa? Mheshimiwa Simbachawene endelea. (Kicheko)

MBUNGE FULANI: Darasa la nne huyo.

MHE. GEORGE B. SIMBACHAWENE: Mheshimiwa Spika, nataka Mwakajoka afahamu kwamba kila Mbunge wa CCM ni Waziri mtarajiwa. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, ni vizuri wakati mwingine tukafahamu historia ya uchumi wa nchi yetu na namna tunavyoujenga. Tulipopata uhuru tulijenga uchumi wa kijamaa na mpaka leo misingi ya kijamaa hatujaiondoa kwenye Katiba hii. Ukisoma Ibara ya 9 inaeleza vizuri namna ya kujenga uchumi wetu, kwa sababu ya muda sitainukuu, lakini nataka wafahamu kwamba ni tofauti na baada tulipofika mwaka 1967 tukajenga uchumi mwingine, lakini pia tumejenga uchumi wa aina tofauti katika kipindi cha kila awamu ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, leo hii tunajikuta tunasahihisha makosa ya uchumi wa soko huria ambao ulikuwa ni fashion na sera ya mashirika ya fedha duniani including World Bank. Tumefika tulipofikana inadaiwa kwamba hatujapiga hatua kubwa ukilinganisha na wenzetu kwa sababu ya aina ya uchumi tulioujenga. Mataifa ya Asia ambayo yali-harmonize ujamaa na ubepari na ndiyo maana Wachina wanasema wanajenga scientific socialism leo, ndiye aliyefanikiwa kupiga hatua.

Mheshimiwa Spika, kwa ninavyoona mimi, ninaona kama Serikali ya Awamu ya Tano inaenda kwenye aina ya ujenzi wa uchumi wa scientific socialism. Mwelekeo huu ni sahihi, ndiyo uliofanya nchi za Asia, Malaysia, Singapore, Bangladesh na zingine kupiga hatua kubwa kiuchumi including China yenyewe na nchi zingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tupewe nafasi kama Chama cha Mapinduzi, tuipeleke hii nje, tufike mahali tuje tupimwe kwa kura za wananchi na nataka niwaambie Watanzania kwamba leo hii ukitaka kujenga nyumba, lazima ujinyime kabisa, ni lazima tujinyime kidogo ili tuweze kujenga nchi yetu, haiwezekani tukawa tunafanya sherehe huku tunafanya maendeleo, haiwezekani. Ni lazima tukubali, tusikilizane, tulete utulivu tuone nchi inavyojengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Watanzania ni mashahidi, kila mahali nchi hii inajengwa, katika kila sekta nchi inajengwa, sasa ni lazima tujenge nchi, haya mambo mengine yatakuja tu. The highest good in life is happiness, Plato alisema, we will be happy kama tumejenga misingi ya uchumi imara. Tumefika tulipofika leo kwa sababu hatukuweka misingi imara sana ingawa awamu zilizopita zilifanya kazi nzuri, lakini kila regime ina fashion yake, let’s follow this fashion. Twende tumuunge mkono Rais, tujenge misingi ya uchumi na mimi naamini ndani ya miaka 10 na kama tutaendelea kumchagua Magufuli kuwa Rais wa nchi hii, tutayaona makubwa ambayo hatukuwahi kuyafikiria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na ninaunga mkono hoja. (Makofi/Vigelegele)