Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Dr. John Danielson Pallangyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Arumeru-Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi nichangie kidogo kwenye hii hoja ambayo iko mezani. Nianze kwa kumshukuru Mungu mwingi wa rehema ambaye ndiye ametuweka hapa, lakini pia niwashukuru sana wananchi wa Arumeru Mashariki ambao waliniamini wakanichagua kwa kura nyingi na kunifanya niwepo hapa leo hii. Waungwana wanasema kwamba ukiaminika unakuwa ni mdeni; kwa hiyo niseme tu kwamba mimi ni mdeni wao kwa hiyo ninawahakikishia kwamba nitajitahidi kuwatumikia kwa kadiri Mungu atakavyoniwezesha.

Mheshimiwa Spika, kipekee sana nichukue nafasi hii kumpongeza sana Rais wetu Dkt. John Joseph Pombe Magufuli ambaye anafanya kazi nzuri sana na ya heshima kwa nchi hii. Anatekeleza ilani ya uchaguzi kwa umahiri mkubwa, na niseme kwamba anaziishi ahadi zake alizozitoa majukwaani mwaka 2015. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende Wizarani. Mheshimiwa Lukuvi nakupongeza sana Ndugu yangu. Nakupongeza wewe na Naibu wako, Makatibu Wakuu na watumishi wote wa Wizara hiyo, mnafanya kazi nzuri na ya heshima. Wenzangu wanakuita kinara wa kutatua migogoro, ni kweli nakubaliananao. Nilikuwa nakufuatilia kwa karibu, mara leo uko Bukoba, kesho Kilombero, kesho kwetu, Jumapili Kilimanjaro; hakika umefanya kazi nzuri unastahili pongezi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali yetu ni Serikali makini sana, inajali Watanzania na ndiyo maana tuliamua kwa makusudi kutenga asilimia nne za ecosystem ya Selou ili tuweze kujenga kinu cha kuzalisha umeme unaotumia nguvu ya maji ili Watanzania waondokane na giza na pia wapate nyenzo muhimu ya kuzalishia bidhaa kwa kuanzisha viwanda vidogovidogo na vikubwa.

Mheshimiwa Spika, ardhi ni rasilimali muhimu sana kwa wananchi, naamini Mheshimiwa Lukuvi analijua hilo. Ninamuomba, wiki iliyopita lilizungumzwa jambo la Kata ya Ngarenanyuki, Kijiji cha Olkung’wado, kwamba kuna tatizo, lakini Waziri wa Maliasili akasema pale hakuna tatizo. Baada ya pale nilipata ujumbe kwamba kweli bado tatizo linaendelea, na nimefuatilia nikakuta wananchi kuna ardhi walikuwa wanaitumia kwa ajili ya maisha yao, ekari 960, zilikuja zikachukuliwa kihalali na Arusha National Park, kisheria, lakini badaye wakakaa chini wakakubaliana wakapunguza pale wakawapa wananchi ekari 360. Nilivyozungumza nao wakasema bado kuna tatizo, na watu wanateseka wamenyang’anywa uhai wao.

Mheshimiwa Spika, sasa nikuombe Mheshimiwa Waziri, nikusihi sana, tulia kidogo uzungumze na Waziri wa Maliasili na Utalii ili muone ni namna gani kwa spirit ileile ambayo tumetenga four percent ya ecosystem kwa ajili ya manufaa ya wananchi, uende pale Momela uzungumze na wananchi uchukue lile eneo ambalo limechukuliwa na TANAPA, ekari zote 960 zirudishwe kwa wananchi ili wakawage na waweze kuishi. Ardhi ni rasilimali ya msingi sana na ndio utajiri mkubwa.

Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana kwa muda huu mfupi. Naunga mkono hoja percent 100. (Makofi).