Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Joseph Roman Selasini

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Rombo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naona tofauti kubwa sana ya kazi zilizofanywa na Wizara hii katika kipindi hiki na kipindi kilichopita. Kwa hiyo si jambo baya kupongeza juhudi na kazi kubwa iliyofanywa na Wizara hii. Pamoja na hayo ni vyema Wizara ikapokea upungufu mchache ambao tunauleta ili ufanyiwe kazi ili kazi ya Wizara iwe bora zaidi ya hapa ilipofikia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka niseme mambo matatu tu. Jambo la kwanza, mdogo wangu Mheshimiwa Mnzava amezungumza habari ya Sera ya Nyumba na huu Wakala wa Taifa wa Utafiti wa Nyumba Bora lazima utusaidie, ni aibu kwa Taifa kuwa na nyumba za tembe. Ukiangalia wananchi sio kwamba wanashindwa kujenga, lakini wakipewa aina fulani ya mjengo wanaweza wakaujenga taratibu wakamaliza na vilevile katika miji yetu sasa hivi kuna kujengwa holela tu.

Mheshimiwa Spika, ukienda miji ya wenzetu, najua Mheshimiwa Lukuvi ametembea sana, unakuta kuna eneo mtaa fulani ni marufuku kujenga aina fulani ya nyumba, aina hii ya nyumba ijengwe mahali Fulani. Sasa ni lazima tu miji yetu tuiboreshe vinginevyo tukiachia kila mtu ana plan ramani yake anabuni kitu chake, matokeo yake makazi yetu yatakuwa hovyo hovyo. Kwa hiyo huu Wakala ufanye kazi yake sawasawa kuishauri Serikali kuhusu nyumba ambazo kwa wananchi zinaweza kuwa affordable na vilevile bei na vifaa kwa ajili ya ujenzi wa nyumba hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine tumesema hapa na nataka nirudie Kambi Rasmi ya Upinzani haipingani na uchukuaji wa mashamba pori, yaani lazima hili lieleweke, sisi tunaunga mkono mashamba ambayo hayajaendelezwa yachukuliwe, tunachosema Serikali sikivu ikikutana na mwananchi mmoja anayelalamika imsikilize kwa sababu kuna baadhi ya wananchi wanalalamika kwamba mashamba yetu yamechukuliwa, lakini ndani yake kuna nyumba, kuna mifugo, kuna mashine na kadhalika. Si jambo baya Serikali ikakaa na watu hawa, ikawasikiliza wakaridhika tu, manung’uniko yakaondoka ndani ya mioyo yao.

Mheshimiwa Spika, lingine…

SPIKA: Mheshimiwa Selasini kwani jamaa si ameenda mahakamani au, endelea kuchangia tu.

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Spika, simjui huyo jamaa. Lingine Mheshimiwa Lukuvi akiwa Moshi alitushauri sisi watu wa Kilimanjaro tuache kuzika kwenye mashamba yetu na tulipiga kelele sana kwa sababu sisi kwa mila zetu na desturi zetu hatuwezi kuacha, lakini mimi ningesema hivi watusaidie katika yale maeneo ambayo huo utaratibu bado haujaanzishwa ili yale maeneo yabaki salama kwa sababu najua eneo ambalo limezikiwa thamani yake inapungua. Sasa kuna maeneo mengine kwa mfano kule wilayani, kwenye miji ile ambayo inakua sasa hivi watusaidie ili watu wasije wakapeleka tena huko makaburi, halafu tukapata shida. Sisi hatuna ardhi na kama nilivyosema huu Wakala wa Utafiti wa Nyumba Bora ingetusaidia sana sisi kwa maana sasa hivi hata shule tunajenga za kwenda juu maghorofa lakini tupewe ramani ili ziweze kutusaidia. Kwa hiyo Mheshimiwa Lukuvi hili zoezi sijui kama tutaliacha, lakini anaweza kuendela kuzungumza labda wazee wa kimila tutamsikia.

Mheshimiwa Spika, lingine ni hili la upimaji; upimaji umekuwa ni tatizo kubwa na hizi halmashauri sijui kama zitaweza. Zamani kulikuwa na utaratibu halmashauri zinakopa Wizarani halafu zinalipa kidogo. Nina maeneo pale Holili watu wanatafuta viwanja tumeshindwa kupima, lakini kwa nini Serikali wasirudishe ule utaratibu wa kuzikopesha halmashauri, zikafanya upimaji, zikauza viwanja halafu ile pesa ya kuuza vile viwanja ikarejeshwa kwa kutokana na mkopo ambao watakuwa wamekopa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie tu kwa kusema Mheshimiwa Lukuvi comment aliyotoa mwenzangu Mheshimiwa Devota Minja…

SPIKA: Malizia kwa dakika moja.

MHE. JOSEPH R. SELASINI: …aliyotoa Mheshimiwa Devota Minja ilikuwa na kusudio la kusema tujenge taasisi, Mheshimiwa Waziri anafanya kazi nzuri, lakini lazima wale wa chini yake wajengwe ili hata akiondoka pale Wizarani, Wizara iendelee na kazi ambayo tunaona anafanya ni pamoja na restructuring na kuhakikisha wale ambao hawafanyi kazi sawasawa wameondoka, lakini ifike mahali hata akiwa hayupo capacity building, Wizara iendelee kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. (Makofi)