Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

Hon. Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilosa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa heshima, naomba nichukue fursa hii kukushukuru tena wewe binafsi kwa kunipa nafasi ya kuwasilisha mpango na makadirio ya bajeti ya Wizara muda wa asubuhi na sasa kuniruhusu kufanya majumuisho ya mjadala.

Nakushukuru kwa kuongoza mjadala wa bajeti yetu kwa umahiri na kwa msingi huo, maoni na michango iliyotolewa yameiwezesha Wizara kupata maoni na ushauri utakaotusaidia kwenye kutekeleza majukumu yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ulivyoendesha kikao leo mimi nimefurahi sana, kwamba leo Mabalozi ambao kwao Bunge lao huwa ni zogo na fujo, wameona jinsi ambavyo Bunge hili ni la kistaarabu pamoja na kelele chache. Sisi ambao tumepata bahati nadra sana kuishi huko, tumeona Mabunge yao, viroja vyao, vituko vyao, wale waliodhani leo watafanya viroja ili Wazungu watuone hatufai, sasa tumewadhihirishia hao Wazungu kwamba sisi tuko mbali sana. (Makofi)

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda niwaambie na natamani wawepo; Ujerumani Spika mwanamke alikuwa haruhusiwi na walipoamua kuwa na Spika mwanamke, anaitwa Clara Zetkin, ilibidi wamtungie sheria kumtangaza kuwa mwanaume ili aweze kuwa Spika. (Makofi)

WABUNGE FULANI: Ahaa.

WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu anavaa suruali ilibidi wapitishe sheria ya kumruhusu kuvaa suruali. Sasa sisi tumeishi huko tumeyaona hayo tunayafahamu hayo sisi hapa hakuna suala la mwanamke kuwa Spika kule bado ni issue tena kubwa sana. Kwa hiyo, nimefurahi sana leo tumeonyesha umahiri wetu na uungwana wetu kwa kiasi kikubwa na kwa namna hiyo nakupongeza sana ulivyoendesha kikao cha leo, ulivyosimamia kanuni na ulivyozitafsiri. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya kipekee naishukuru kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nje ya Ulinzi na Usalama chini ya uongozi mahiri wa Mheshimiwa Mussa Azan Zungu, na wajumbe wote wa Kamati kwa ushirikiano mkubwa waliotupatia wakati wa maandalizi ya bajeti na kwa hotuba nzuri waliyoitoa. Tunashukuru kwa maelekezo, maoni na ushauri ambao kamati hii imekuwa ikiupata na nataka niahidi yale yote ambayo leo wametushauri Wizara itayazingatia na itayatekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimshukuru sana Mheshimiwa Salome Wickliffe Makamba nina mwendi labda nitoe siri leo. Salome Wickliffe Makamba marehemu baba yake Wickliffe Makamba na mama yangu Patricia Mwendi ni mabinamu na ndiyo maana mtoto wake anajina la babu yangu Mwendi, kwa hiyo mfahamu nafurahi sana mimi niko huku yeye yuko huko tumetoa hotuba leo na leo Gairo, Mamboya, Berega, Magubike wamefurahi sana kwa hiyo tumepokea maoni na ushauri ulioutoa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya pekee namshukuru sana Mheshimiwa Balozi Dkt. Augustine Phillip Mahiga, Waziri wa Katiba na Sheria ambaye hapo awali alikuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mheshimiwa Mahiga aliweka msingi mzuri katika Wizara hii ambayo inaniwezesha kutekeleza majukumu yangu kwa ufanisi namshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Mahiga kwa ushirikiano mkubwa alionipa mara mbili Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Joseph Magufuli alinituma niende pamoja na Mheshimiwa Dkt. Mahiga nje na nilijifunza mengi sana kwake katika mikutano hiyo nje na leo hii namshukuru hakuwa mchoyo wakati huo kuniandaa leo kuchukua na kuvaa viatu vyake ingawa dhahiri ni vikubwa lakini namshukuru sana pia anavyoendesha Wizara ya Katiba na Sheria nilikotoka. Mwalimu na mwanafunzi wanapopokezana vijiti ni jambo la fahari na ni nchi chache kitu kama hicho kinatokea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho lakini siyo kwa umuhimu naomba kumshukuru Dkt Damas Ndumbaro Naibu Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, kwa kazi kubwa anayoifanya katika Wizara hii kwa kipindi cha miezi takriban miwili na toka niingie kwenye Wizara hii amekuwa na mchango mkubwa katika utendaji kazi wangu na ufanisi wa Wizara. Yeye amesafiri mara nyingi nje ya Nchi kuliko mimi na huko ametuwakilisha vizuri sana nichukue fursa hii kumpongeza sana alivyotuwakilisha vizuri Argentina, alivyotuwakilisha vizuri Brussels, Pretoria, Kigali, Uganda amefanya kazi nzuri na mimi najivunia sana kazi yake. (Makofi)

Mheshiiwa Naibu Spika, pia nimshukuru Katibu Mkuu Dkt. Faraji Mnyepe, Naibu Katibu Mkuu Mheshimiwa Balozi Muombwa Mwinyi, Mabalozi wote wote Wakurugenzi Wakuu wa vitengo na watumishi kwa kujituma ni imani yangu kuwa ushirikiano huu na kujituma kwenu kutaimarika wakati mnatekeleza bajeti ya mwaka 2019/2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mjadala wa bajeti yetu jumla ya Waheshimiwa Wabunge 13 wamechangia kwa maandishi na jumla ya Wabunge wanne wamechangia kwa kuongea kwa namna ya pekee nawashukuru Wabunge waliochangia kwa kuongea na maandishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote kwa michango yao mizuri waliyoitoa wakati wa majadiliano hapa Bungeni, tumepokea maoni mazuri ambayo yamelenga kuboresha utendaji wa kazi wa Wizara na Sera ya Kidiplomasia ya kiuchumi ni dhahiri Waheshimiwa Wabunge wote wanatamani kuona mchango wa Wizara hii katika maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue fursa hii kuwahakikishia kuwa chini ya uongozi wangu na viongozi wengine wa Wizara tutahakikisha kuwa mfumo wa utendaji kazi wa Wizara unabadilika na Wizara inatoa mchango stahiki na kwa ujumla maoni na ushauri uliotolewa na Waheshimiwa Wabunge wakati wakichangia bajeti hii ni ushahidi kwamba Bunge hili linatambua umuhimu wa mapendekezo ya kujenga hoja. Kwa hiyo, ningependa niangalie nifafanue baadhi ya hoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, moja, ningependa nieleze msingi wa sera yetu ya mambo ya Nje umewekwa bayana na Baba wa Taifa letu Mwalimu Julius Kambarage Nyerere katika waraka aliotoa kwa watumishi wote wa Wizara ya Mambo ya Nje unaitwa argue don’t shout na inasema an official guide on foreign policy by the President na katika Waraka huu wa argue but don’t shout mwalimu ameweka wazi baadhi ya mambo.

Mheshimiwa Naibu Spika, moja, aliloliweka wazi ni kututaka tujue dunia inabadilika lakini pamoja na dunia kubadilika mambo ya msingi tuyashikilie lakini tujue kuna wakati itabidi tubadilishe mbinu na mikakati ya kufikia lengo tunalolitaka. Mwalimu hakutuambia tushikilie misingi tu na kuacha kuangalia hali halisi ya dunia alitutaka tuangalie hali halisi ya dunia bila kupoteza misingi. Na wengi siku hizi wanamzungumza Mwalimu bila kuwa na uhakika wa yale wanasema.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mwalimu hakuwa ni mtu ambaye alikuwa anakubali nchi hii iburuzwe. Kuna nyakati Mwalimu alichukua maamuzi katika sera ya Mambo ya Nchi za Nje ambao wengi hawakuyatazamia mwaka 1964 Tanganyika na Zanzibar zilipoungana. Tanganyika palikuwa na Ubalozi wa Ujerumani Magharibi, Zanzibar palikuwa na Ubalozi wa Ujerumani Mashariki, mara baada ya Muungano huo Ujerumani Magharibi ilitaka kumlazimisha Mwalimu kuiondoa Ujerumani Mashariki.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mwalimu aliwaomba muda ili jambo hilo lishughulikiwe kwa utaratibu Wajerumani kwa sababu ndio waliokuwa wanaipa Tanzania misaada mingi kuliko nchi yoyote walidhani wanaweza kumburuza akubali maoni yao. Wale wote wenye umri mkubwa kuliko mimi wanajua, Mwalimu alichukua hatua ambayo hawakuitarajia. Moja aliwafukuza wataalam wote wa Kijerumani isipokuwa Wamissionari, pili aliwarudishia Wajerumani fedha yao doch mark milioni 40 na Jengo la Nkurumah Hall Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ambalo sasa halijamaliziwa Mwalimu alisema limaliziwe.

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Kuhusu Utaratibu.

WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Lakini pia Mwalimu alichukua hatua nyingine kubwa mwaka 1965 Wazungu wabaguzi...

NAIBU SPIKA: Naomba ukae Mheshimiwa ukiniona nakuongelesha hivyo ni kwa sababu sitaki kukukumbusha kanuni zinasemaje huyu aliyesimama hapa ni Waziri mtoa hoja. Kanuni yako inasemaje? Naomba ukae Mheshimiwa Mwakajoka. Mheshimiwa Waziri.

WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Na wakati huo wale Wazungu wachache wa Arodesia walipojitangazia uhuru Umoja wa Nchi za Afrika ulitoa maazimio kwamba Uingereza iwaondoa Wazungu walowezi wachache Rodessia katika utawala na wasipofanya hivyo nchi za Afrika zivunje uhusiano wa Kibalozi na Uingereza.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni nchi mbili tu zilifanya hivyo ni Ghana na Tanzania, na matokeo ya Ghana kuvunja uhusiano wa kibalozi na Uingereza marehemu Kwame Nkurumah alipinduliwa na wanajeshi wakiongozwa na Achiempong aliesoma San Hast nchi ya pili kufanya hivyo ilikuwa na Tanzania ilivunja uhusiano wa Kibalozi na Uingereza kuanzia mwaka 1965 mpaka mwaka 1972 Kerbado Mwalimu aliwarudishia Waingereza msaada waliokuwa wameuleta wa paundi milioni tano, huyo ndiyo Julius Kambarage Nyerere. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hoja za leo ninazozisikia watu watatamani tupate misaada hiyo na tuvunje misingi. Watu watatamani tupige magoti ili tupate misaada. Nasema hivi chini ya utawala huu wa Chama cha Mapinduzi nchi hii haitapiga magoti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kamwe nchi hii haitapiga magoti wamethubutu wameshindwa hii ndiyo nchi pekee katika Bara la Afrika haijashindwa vita hatukushindwa Uganda, hatukushindwa Sychelles, hatukushindwa Comoro hii ndiyo nchi pekee imewapeleka wapigania uhuru kwao tumewapeleka Zimbabwe, tumewapeleka Msumbiji, tumewapeleka Namibia hii ndiyo nchi iliyopokea watu wenye shida wengi kuliko wote na kwa kufanya hivyo Mwalimu alilipa gharama kubwa ambayo Dkt. Magufuli atailipa sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mwalimu kwa kusaidia nchi hizo aliitwa M-communist na mimi nilishangaa kwa mara ya kwanza tunamkatoliti m-communist na hila hizo hizo husuda hiyo hiyo wivu huo huo upo sasa kwa sababu nchi hii chini ya Dkt. Magufuli tumeamua kujitegemea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na mara nchi ya Afrika inapoamua kujitegemea maadui wanatumia vibaraka ndani ya nchi, mabaraka ndani ya nchi…

WABUNGE FULANI: Wako humu, wako humu ndaniii!

WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, huo ni usaliti kwa nchi yetu tusikubali kuwa mabarakara wa mabeberu tusikubali kutumiwa hii nchi ni yetu. Niwakumbushe mara baada ya hali ngumu ya uchumi mwaka 1985 Benki ya Dunia na Benki ya IMF walipozilazimisha nchi zote kutuacha na nchi za mwisho kutuacha ilikuwa ni nchi za Nordic. Bado nchi hii ilisimama haikupiga magoti haiwezi kupiga leo magoti wakati tuna foreign reserve ya miezi mitano hatukupiga magoti wakati hatuna foreign reserve wakati mzee Mwinyi anaingia hatuwezi kupiga magoti leo tuna foreign reserve ya miezi mitano aslan kamwe halitatokea hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na ndiyo maana Mwalimu kwenye hii argue don’t shout anatutahadharisha anasema wale wa nje ni opponents hawa wa ndani wanaokuchimba ndiyo enemies kwa hiyo, we are facing enemies internally but we are facing opponent outside our enemies are eternal outside are opponents. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba nijibu hoija mbalimbali. Ya kwanza ni hoja kuhusu Tanzania kuwa na kigugumizi kuridhia mkataba wa makubaliano ya eneo huru la biashara Barani Afrika – AFTA. Serikali ieleze Bunge ni lini itatuletea mkataba huo Bungeni ili uridhiwe. Ningependa kusema hivi, mkataba huu tumekwisha usaini Tanzania imeusaini mkataba huu na saa hizi tuko katika mchakato wa kuupitia ili tuone faida zake na…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mbilinyi, Mheshimiwa Prof. Kabudi naomba unyamaze kidogo Mheshimiwa Mbilinyi na Mheshimiwa Salome na Mheshimiwa Mwakajoka tafadhalini sana. Mheshimiwa Mwakajoka tafadhali, Mheshimiwa Mbilinyi tafadhali na Mheshimiwa Makamba nimewataja hii ni mara ya mwisho hii ni mara ya mwisho Chief Whip wa opposition nimewataja Wabunge wako watatu mara ya mwisho. Mheshimiwa Prof. Kabudi.

Naomba ukae Mheshimiwa Selasini kwa sababu unaufahamu utaratibu nimekuambia nimewataja Wabunge wako kwa sababu we ndiyo kiongozi wako na uwambie watulie wamekaa hapo karibu na wewe. Mheshimiwa Kabudi naomba uendelee.

MHE JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa mimi ni Chief Whip.

NAIBU SPIKA: Chief Whip hausimami akiwa amesimama Waziri Chief Whip huwezi kusimama akiwa amesimama Waziri hata yeye angekuwa amesimama wakati Waziri amesimama hawezi kusimama naomba ukae, naomba ukae Mheshimiwa Selasini. Naomba uendelee Prof. Kabudi

WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala kwamba hakuna takwimu za Kitaifa zinazoonyesha idadi kamili ya Watanzania wanaoishi Nje ya Nchi, na kile wanachokifanya huko. Na kwamba Serikali inapaswa kuhakikisha inaanzisha kanzi data ningependa kueleza kwamba hivi sasa Wizara inaendelea na maandalizi ya Sera ya Taifa ya Diaspora na yapo katika hatua nzuri. Mara baada ya kukamilisha sera hiyo tutaingia katika hatua ya kuwaandikisha Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la Watanzania kuandikishwa ni la hiari kwa hiyo tunawaomba watanzania wote wanaoishi Nje ya Nchi wasikose kwenda kujiandikisha kwenye balozi zetu ili tuweze kuwatambua na kuwafahamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la uraia wa Tanzania ningependa kueleza kwamba suala la uraia linasimamiwa na Sheria ya Uraia Namba 6 ya mwaka 1995 ambayo imebainisha kuwa uraia wa Tanzania upo katika makundi matatu uraia wa kuzaliwa, uraia wa kurithi na uraia wa tajinisi (kuandikishwa) kwa mujibu wa sheria hiyo, aina ya uraia wa kuandikishwa uraia wa pacha haupo katika sheria za Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la kubadili msimamo kwamba Tanzania imebadili msimamo wake kuhusu ushirikiano na nchi za Morocco na Israel na je mabadiliko hayo ya msimamo wa nchi yanalindwa na yaliridhiwa na Bunge? Na nini msimamo wetu kama Taifa juu ya tabia za kidikteta, ukiukwaji wa haki za kibinadamu, unyanyasaji na uonevu zinazoanza kuibuka na kujionyesha wazi miongoni mwa baadhi ya viongozi wa Mataifa mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ningependa nieleze kwamba Tanzania haikuvunja uhusiano na Israel mwaka 1973 kwa sababu ya suala la Palestina. Tanzania ilivunja uhusiano wa kibalozi na Israel mwaka 1973 kwa sababu baada ya Israel kuzishambulia nchi za Kiarabu na kuteka maeneo ya Sinai kwa upande wa Misri na kuteka maeneo ya Golan kwa upande wa Syria hiyo ndiyo ilikuwa sababu iliyoifanya Tanzania wakati huo kuvunja ushirikiano wa Kibalozi na Israel.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hapo nchi mbalimbali ikiwemo nchi ya Misri yenyewe na nchi nyingi za Kiarabu zimeanzisha uhusiano wa kibalozi na Israel. Hatuoni sababu sisi kutokuanzisha uhusiano wa ubalozi na Israel. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo kuanzisha uhusiano wa kibalozi na Israel na kufungua ubalozi hakujatuondoa katika msimamo wetu wa kuunga mkono harakati za Wananchi wa Palestina. Na msimamo wetu uko wazi wala hauna kigugumizi, wala hauna tashwishwi tunasema tuwe na Israel iliyo salama na tuwe na Palestina iliyohuru katika hilo hatubadiliki na ndiyo maana mpaka leo tunavyozungumza miongoni mwa nchi ambazo zimeitambua Palestina na zina ubalozi wake hapa nchini ni Tanzania Palestina wana ubalozi wao Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo uhusiano wetu wa kibalozi na Israel hata kidogo hautatuondoa sisi kusimama kwa upande wa Palestina. Na ndiyo maana kama kuna nchi ambayo tumepiga kura kuunga mkono maazimio yake katika Umoja wa Mataifa, ni Palestina. Nina orodha ya maazimio 23 ambayo Tanzania imepiga kura in favour of Palestine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ningependa kuwahakikishia kwamba hatujatetereka lakini ni ukweli leo hii huwezi kuacha kuwa na mahusiano na Israel wakati nchi zote za Kiarabu zinamahusiano na Israel na yako mambo ambayo tunayahitaji kutoka Israel katika upande wa uchumi, upande wa kilimo, upande wa IT. Lakini hilo halitatuondoa katika kusema kwamba Palestina iwepo na iwe huru lakini pia Israel iwepo na iwe salama na maazimio hayo yapo mtu ambaye anapenda kuyapata atayapata jinsi ambavyo Tanzania imepiga kura kuunga mkono Palestina katika mambo yake mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la Morocco na Saharawe na mgogoro wa Morocco Saharawi kwenye eneo la Sahara Magharibi. Tanzania inaunga mkono juhudi za Umoja wa Mataifa na Umoja wa Afrika katika usuluhisho wa mgogoro huo, Tanzania inaendelea kuzisihi pande zote kukaa kwenye meza ya mazungumzo ili kupata suluhu ya kudumu ya mgogoro huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, na ndiyo maana kutokuegemea upande wowote tumekuwa tunahudhuria mikutano yote inayohusu Saharawi, tunahudhuria mikutano yote inayohusu Morocco. Na niseme hivi hata nchi hizo zenyewe ambazo zinawahisani watu wa Saharawi zinauhusiano wa kibalozi na Morocco mfano wa nchi hiyo ni Algeria na nchi ya Morocco kufungua ubalozi wake hapa nchini haukuifanya sisi tuiambie Saharawi ifunge ubalozi wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo leo Tanzania Saharawi ina ubalozi wake Morocco inaubalozi wake na sisi tunashirikiana na wote bila kuwabagua na tunawahimiza wamalize matatizo yao kwa kufuata maazimio ya Umoja wa Mataifa. Na tunaishukuru Algeria ambayo pamoja na mvutano wote haijavunja uhusiano wa kibalozi na Morocco hata wakati nchi nyingine zilipovunja uhusiano wa kibalozi na Morocco. Kwa hiyo hatuoni sababu ya kufanya hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nije kwa hoja alizozitoa Mheshimiwa Suzan Anselem Jerome Lyimo Mbunge wa Viti Maalum CHADEMA ambaye ameishauri Serikali kufanyia kazi changamoto za kupandishwa vyeo watumishi wa Wizara ambao wamekaa kwenye cheo kimoja kwa muda mrefu. Na kutaka kujua Serikali inampango gani wa kupeleka mbadala wa watumishi waliorudi Makao Makuu kwenye Balozi zetu na kuishauri Wizara kutoa mafunzo ya Kideplomasia kwa mabalozi wetu wanaoenda kuhudumu kwenye Balozi zetu nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kulifahamisha Bunge lako tukufu kwamba tayari katika mwaka huu wa fedha tunaoumaliza jumla ya wafanyakazi 87 wamepandishwa vyeo, 66 wamepandishwa vyeo na 21 Wizara imependekeza wapandishwe vyeo vya huo msereleko. Tunayo barua kuotoka Ofisi ya Rais, Manajimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora yenye Kumb. Na. BC.46194/03D/44 ya tarehe 16 Aprili 2019 na barua yenye Kumb. Na. BC.46/97/03D/45 ya tarehe 30 Aprili, 2019. Barua hizi zimetoa kibali cha kuwapandisha vyeo jumla ya watumishi 66 na kuwabadilisha kazi recategorization jumla ya watumishi watatu. Jitihada hiyo itaendelea kama ambavyo tumekuwa tunafanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala kutoa mafunzo ya kidiplomasia kwa Mabalozi wetu wanaoenda kuhudumu kwenye Balozi zetu. Ningependa kulihakikishia Bunge lako tukufu kwamba hicho ndicho kinachofanyika, hakuna Balozi anayepelekwa nje bila kufanyiwa mafunzo katika Chuo cha Diplomasia. Sio Mabalozi tu hata Watanzania ambao wanaochaguliwa kwenda kufanya kazi kwenye Mashirika ya Kimataifa ambao Serikali imeawaidhinisha waende, nao pia wanafanyiwa mafunzo haya na ninakubaliana na yeye kabisa kwamba kuna umuhimu wa sisi wote kujifunza etiquette za Kibalozi na Kidiplomasia ikiwa ni pamoja na Wabunge ili tuweze kuelewa hizi etiquette za kidiplomasia zinatakiwa ziwe namna gani.

Mheshimiwa etiquette Spika, kuhusu Mheshimiwa Riziki Said Lulida wa Lindi ambaye ameulizia suala la mjusi toka Tendaguru, Lindi au kwa jina la kiingereza Dinosaur. Ningependa nieleze kwamba ni kweli ukienda kwenye Jumba la Makumbusho ya Elimu ya Viumbe yaani Museum for Natural History ya ...yako masalia ya Dinosaur wa sita kutoka Tanzania ambayo wakati huo ilikuwa chini ya utawala wa Wajerumani na kwa kweli masalia hayo yalitolewa Tendaguru na ukifika pale wameeandika yametolewa Tendaguru, Lindi.

Mheshimiwa Naibu Spika, masalia hayo ni mchanganyiko wa mifupa halisi mjusi mkubwa Dinosaur na cas, cas ni maeneo ambayo mifupa haikupatikana walitengeneza ili kukamilisha umbo la wanyama hawa. Masalia yalichukuliwa kutoka kilima cha Tendaguru kuanzia mwaka 1909 mpaka mwaka 1913 wakati wa ukoloni wa Mjerumani.

Mheshimiwa Naibu Spika, takribani tani 250 za masalia pamoja na mimea silichukuliwa na kupeleka Ujerumani. Majina ya kitaalamu ya Dinosaur hao ni Brachiosaurus, Branchai, Kentrosaurus, Diastosaurus, Digasaurus, Erliphosaurus, Bambegi na Arosaurus na huyu Brachiosaurus Branchai ni mrefu na anachukua urefu wa ghorofa tatu. Na mimi kwa miaka tisana na siku nne nilizoishi pale Berlin hakuna Watanzania waliokuja kunitembelea sikuwapeleka kwenda kuyaona hayo masalia ya Dinosaur ni makubwa na bado ipo mifupa mingine ambao ipo kwenye sera ipo kwenye maghala ambayo bado hayajaunganishwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo upo umuhimu wa Serikali ya Tanzania na Serikali ya Ujerumani kuzungumza kuhusu suala hilo. Kabla ya Ujerumani Mgharibi na Ujerumani Mashariki kuungana, Ujerumani Mashariki ambapo ndipo yalipokuwa hayo masalia kwenye Chuo Kikuu cha Berlin walikuwa wameanza utaratibu wa kujenga Makumbusho ya Elimu ya Viumbe hai Arusha ili waweze kuleta leprechaun mfano wa hao Dinosaur. Kuna umuhimu tena wa kufufua mazungumzo na Serikali ya Ujerumani ili tuchukue hiyo hatua ya kwanza kabla ya kuingia kwenye hiyo hatua ya pili ya kuomba masalia haya yarudi. Kwa sababu yanahitaji utaalamu wa hali ya juu kuyatunza na tunadhani hali ya hewa ya Arusha inafaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu ombi lake kwamba watu wa Tendaguru waweze kufaidika na mijusi hawa ambao wapo Berlin, wazo hili tumelichukuka na sisi tutazungumza na Serikali ya Ujerumani kuona ni kwa kiasi gani Wajerumani na hasa wanaohusika na mambo ya utafiti wataikumbuka Tendaguru ambapo hao mijusi walichukuliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Timotheo Mnzava, Mbunge wa Korogwe Vijijini kwa maelezo aliyoyatoa kuhusu hali ya haki za binadamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwezi Machi tulipata nafasi ya kwenda kwenye Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Kimataifa na tulipofika palikuwa tayari taarifa zimepelekwa nyingi sana kwamba Tanzania hali ya haki za binadamu haiko sawasawa. Tulitoa maelezo na maelezo yale yaliwaridhisha na kwa maana hiyo Kamishna wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa aliiondoa Tanzania katika ripoti yake ya nchi zinazovunja haki za binadamu, aliiondoa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuliwaeleza bayana wenzetu kwamba moja hakuna haki ambazo hazina mipaka, haki zote zina mipaka. Mipaka hiyo imewekwa ndani ya Katiba wazi kabisa, hakuna uhuru wa yoyote kuingilia uhuru wa mtu mwingine. Kwa hiyo, mpaka wa kwanza wa haki za binadamu ni pale haki ya mtu mwingine inapoanza. Kwa hiyo, hakuna haki ambayo haina mpaka na Katiba yetu imeweka wazi kabisa katika Ibara ya 30 ni mipaka gani imewekwa kuhusu haki za bindamu nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na kama iliyoelezwa sisi mahakama zetu na tatizo kubwa tulionalo sisi na hapo wa kulaumia ni mimi na Dkt. Mwakyembe. Kosa kubwa tulilolifanya mimi na Dkt. Mwakyembe ni kutokuandika commentary ya Katiba yetu. Kwa hiyo, watu wengi wanaposoma haki za binadamu wanasizoma silivyo ndani ya Katiba bila kuwa na commentary ya kuwaonesha ibara hii ya Katiba tayari Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufaa imetoa tafsiri hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwahakikishe sisi ndio nchi inayoongoza katika hukumu zetu za haki za bindamu kuwa cited na Mahakama za nchi nyingine za Commonwealth. Kesi ya kwanza iliyoamuliwa na Mahakama Kuu iliyotupa umaarufu mkubwa kabisa na kunukuliwa na mahakama zaidi ya 56 ni kesi ya Horaria vs Pastory. Horaria binti wa Kihaya ambaye alizuiwa kurithi mali kwa sababu ni mwanamke.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mahakama Kuu ya Tanzania kuhumu ya Jaji Mwalusanya ilisema haki hiyo, sheria hiyo ya mila inavunja Katiba na baada ya hapo hiyo ndio imekuwa reference ya nchi nyingi kuhusu haki za wanawake zinapovunjwa na sheria za kimila. Kwa hiyo sisi Tanzania tumepiga hatua kwamba hata sheria za kimila zimewekewa mpaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hivi majuzi zimetoka kesi mbili maamuzi ya Mahakama ya Rufaa kwenye kesi ya Mheshimiwa Freeman Mbowe na Mheshimiwa Esther Matiko, kabla ya hizo kesi kuamuliwa nilifuatwa na watu wa nje wengi sana wakati huo nikiwa Waziri wa Katiba na Sheria wakinisihi niiambie mahakama hizo kesi zifutwe, jibu langu lilikuwa we are not a banana republic allow the court to do their job. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma leo hukumu hizo mbili zimeweka misingi mizuri sana tisa ya jinsi gani mahakama zishughulikie suala bail (suala la dhamana). Ningeshawishika ili kuwafurahisha na labda wanisifie na wanipambe hao watu wa nje ningeimbia mahakama bwana hii kesi iacheni, tungekuwa tumekosa judgement nzuri kabisa ya Jaji Rumanyika ambaye ameweka sasa misingi mizuri tisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nina imani hukumu hiyo sasa itakuwa ni precedent ingawa sio binding katika nchi nyingine za Commonwealth. Kwa hiyo mahakama zetu zinafanya kazi kubwa sana na ndani ya ile hukumu kuna mstari watu wengi hawausemi. Sasa hivi hawa Wabunge wawili hawawezi kusafiri nje ya nchi bila permission of the court kwa sababu wali-jump bail, lakini kikubwa kwenye judgement hiyo ni ile misingi tisa ambao sasa mahakimu wote ni lazima waizingatie wanapotaka kumnyima mtu dhamana na ni misingi imewekwa vizuri na itawasaidia sana walio chini yake na sana itakuwa binding to all subordinate courts.

Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi baada ya hukumu hiyo Mheshimiwa Naibu Spika niliwaita baadhi ya hao waliokuja kunisii nifanya hivyo, nikawambia hii misingi tungeipata wapi? Kwa sababu kuna tabia ya hawa wenzetu wa nchi za Magharibi na nchi za Magharibi hazina moral authority za kutufundisha haki za binadamu. Naawaambia na uzuri nimekaa nao miaka tisa, nimesoma nao wajinga pia kule wengi na nimefaulu nikawashinda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi nchi hizi za Afrika we have never enslaved anybody, we have never colonized anybody, we have never plundered property of anyone, wao wametu- enslave, wametu- colonize na wame-plunder our resources, hawawezi kuwa na moral authority. Nchi za Magharibi sisi hatujawahi kusababisha vita yoyote, wao wamesababisha vita kuu mbili, na vita zote kuu mbili zimekuwa na madhara kwa nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Vita ya Kwanza ya Dunia ilipokwisha makoloni yote ya Wajerumani yaliwekwa chini ya league of nations yaligawanywa, Tanganyika huku, Rwanda na Urundi kule. Na nchi hii kwa miaka mitatu ilikuwa na haina jina, haina mwenyewe, Cameroon ikagawanywa, Togo ikagawanya, waliacha ... West Africa ambayo leo ni Nambia. Na matokeo yake we became the cinderella of West Africa, the British did nothing, the British did nothing for this country. The biggest university we have tumeijenga wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Waingereza hawajatuachia University they did nothing. Hata reli ile ile aliyoacha Mjerumani na sasa tunajenga nyingine. Vita Kuu ya Pili ya Dunia wamechinjana Warusi peke yao walikufa milioni 20. Sisi hatukumkamata shoga kumtia kwenye gas chamber kama walivyofanya Wajerumani, sisi hatukumkamata chotara tukamtia kwenye gas chamber, sisi hatukumkamata Myahudi na kumtia kwenye gas chamber, sisi hatukukamata mashoga na kuwatia kwenye gas chamber. Wao wamefanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, so they have no moral authority of telling us anything, tutaendelea kuheshimu haki za binadamu kwa sababu ni muhimu kuziheshimu, tutaendelea kuheshimu Katiba yetu kwa sababu ni muhimu kuiheshimu. Lakini sio kwa sababu kuna mtu anayetuambia tuiheshimu na tuchukue jitihada zote kulinda haki za binadamu kwa sababu binadamu wote ni sawa, huo ndio msingi wa Katiba ya TANU, huyo ndio msingi wa Katiba ya CCM na huo ndio msingi wa Katiba yetu. Binadamu wote ni sawa na wanastahili heshima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini wao hawakutuheshimu na wao hawakutuchukulia kuwa sawa. Nchi hii imewahi kuingizwa katika ushauri wa ajabu kina Mzee Mkuchika wapo hapa mwaka 1958 tulilazimshwa kufanya uchaguzi na ninasema hivi kwa sababu wanafunzi wapo waelewe. Tukaambiwa ili mjiandae kupata uhuru lazima tuwafundishe kupiga kura, tukaambiwa kila jimbo la uchaguzi tuchangue Wabunge watatu Mzungu, Mhindi na Mwafrika.

Mheshimiwa Naibu Spika, wanachama wengi wa TANU walikataa ikiwa ni pamoja na Katibu Mkuu wa TANU wa wakati huo Zuberi Mtemvu ambaye alijitoa akaunda chama chake cha African National Congress. Tulivuka huo mtihani, tumevuka mitihani mingi na huu mtihani tutauvuka tena kwa ushindi mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 1985 benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa lilitupigisha magoti kwa sababu tulikuwa hatuna uwezo wa kiuchumi. Sasa tunajenga Stiegler’s Gorge itatupa umeme tunajenga Standard Gauge Railway tutasafirisha mizigo. Baada ya hapo huduma zetu za kijamii katika elimu, afya na maji haitategemea tena fedha kutoka nje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tuwe ndio kizazi cha mwisho cha kutegemea misaada, wajukuu zetu na vitukuu vyetu wasiishi fedheha hii tena. Fedheha hii iishe na sisi, tunavuna haya kwa sababu bado hatujafikia mahali pa kujitegemea na mimi nashukuru sana Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kuchukua hii miradi ya kimkakati ambayo baadaye italifanya Taifa hili lijitegemee liwe lenye nguvu, na mimi nimefarijika sana na ningependa kuwaambia Watanzania wote Mheshimiwa Rais leo amemaliza ziara ya Zimbabwe, tumekuwa Afrika ya Kusini siku nne, tumekuwa Namibia siku mbili. Zimbabwe ilikuwa tukae siku mbili lakini wakamuomba aongeze siku ya tatu. Ndugu zangu wanamuona ni Mwafrika mahiri, shupavu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninawaambia Watanzania wote wenye umri wangu tumshukuru Magufuli kwa kufanya mambo haya makubwa ambayo Baba wa Taifa aliyajenga, Mzee Mwinyi akaichukua nchi hii kipindi kigumu, tumepigishwa magoti tumekataa na waliofuata wamejenga msingi. Mkapa, Kikwete na sasa Magufuli na Magufuli ndio atakuwa Rais wa mwisho kwa maoni yangu aliyemuona Nyerere akiwa mtu mzima. Na ni vizuri Mungu atambariki kwa kukamilisha miradi yote ya Mwalimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwaambie tulipifika Pretoria moja ya sababu kubwa ya kushangiliwa kwanza kuwaona Rais aliyestaafu na Rais aliyemwachia wapo pamoja na wameshuka pamoja is very rare, lilikuwa ni jambo la fahari. Nchi nyingine Rais Mstaafu na Rais aliye madarakani hata kusalimia hawasalimiani. Jambo kubwa, kwa hiyo Mheshimiwa nilikuwa kwenye uwanja nimeona aliyeshangiliwa zaidi kuliko wote ni Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tumekwenda Nambia, tumekwenda Zimbabwe na kote watu wametupokea vizuri, na safari imekuwa ya mafanikio makubwa na manufaa makubwa kwa nchi yetu. Leo hawatanikasirisha leo sikasiriki ng’oo, ndio leo sikasiriki ng’oo, mtazoza mpaka mtachoka. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, yapo maswali tuliyoyapata kwa maandishi na ambayo tumeyajibu na mengi yanafafan na yale ambayo yamekwishatolewa, kuna swali kutoka Mheshimiwa Lucia Michael Mlowe, Mheshimiwa Ritta Kabati, Mheshimiwa Rhoda Edward Kunchela, Mheshimiwa Christopher Chiza, Mheshimiwa Janet Mbene, Mheshimiwa Mwanne Mchemba, Mheshimiwa Sonia Juma Magogo, Mheshimiwa Hamoud Abuu Jumaa, Mheshimiwa Zuberi Kuchauka, Mheshimiwa Juma Othman Hija, Mheshimiwa Zainab Mndolwa Amir na Mheshimiwa Janeth Moris Masaburi.

Mheshimiwa Naibu Spika, michango yote hii tumeipokea na tumeipa majibu na tutasambaza majibu yote ya maswali hayo ya maandishi tuliyoletewa.

Mheshmiwa Naibu Spika, ningependa tena nichukue fursa hii kukushukuru sana Naibu Spika, kuwashukuru Wabunge wote kwa michango mikubwa waliyoitoa kwa Wizira yetu na imani yangu Inshallah katika mwaka huu wa fedha ambao tutauanza baada ya Bunge la hili la Bajeti kukamilika tutaendelea kutekeleza vipaumbele vyote vilivyopo.

Mheshimiwa Naibu Spika, moja, hatutakaa kimya nchi yetu inapobezwa, hatukaa kimya nchi yetu inapotukanwa, hatutakaa kimya nchi yetu inapochokozwa. Tutajibu tutafafanua tutaeleza tulifanikiwa Geneva tutafanikwa New York na tutafanikiwa mahali popote, huu sio wakati wa kukaa kimya, huu sio wakati wa kupuuza, kila linalotolewa lijibiwe tena lijibiwe kwa stahili kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kumaliza, mimi sipendi sana kujieleza mimi ni nani, lakini Mheshimiwa Naibu Waziri amesema na Mheshimiwa Naibu Waziri na Mheshimiwa Ummy Mwalimu ni wanafunzi wangu wa jurisprudence mara baada ya kuwa nimerejea toka masomoni nje, nimewafundisha jurisprudence, lakini mara nyingi katika nchi hii sio mara ya kwanza kuombwa na nchi yangu kufanya kazi ngumu. Mheshimiwa January Makamba yupo hapa, Sheria ya Mazingira hiyo anayoitumia aliyeisimamia, aliyeitunga na kuhakikisha inakuja Bungeni wakati Mheshimiwa Chenge kaka yangu akiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali ni Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi na ninaomba niwasomee Hansard na nimsome wakati huo Waziri wa Ofisi ya Makamu wa Rais, Mheshimiwa Arcado Ntagazwa anasema nini kuhusu Palamagamba Kabudi ndani ya Bunge hili mwaka 2004. (Makofi)

Anasema; “Nimalize sehemu hii ndogo kwa kumshukuru na kumpongeza, ataniwia radhi kama nitatamka jina lake yabidi nifanye hivyo, Dkt. Palamagamba Kabudi, Mhadhiri wa Sheria katika Kitivo cha Sheria, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Dkt. Palamagamba Kabudi ndio Mshauri Mwelekezi (Consultant) kwa lugha ya kiingereza wa Mradi wa Kubainisha Mfumo wa Kitaasisi na Kisheria katika jitihada za Taifa letu kuhifadhi na kusimamia mazingira, kujihakikishia maendeleo endelevu. Tunawashukuru Benki ya Dunia, waliohisani mradi huo na kupitia kwa Dkt. Palamagamba Kabudi Tanzania tuna mahali pa kujidai, kwani kwa yakini kuwa nchi yetu tunao wataalam wazalendo wanaokidhi sifa zitakiwazo Kimataifa. Maana Dkt. Palamagamba Kabudi sio peke yake, wako zaidi kama huyu.” Hiyo ilikuwa tarehe 10 Novemba, 2004. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati Sheria ya Kupambana na Rushwa inatungwa mwaka 2004, wakati upinzani chini ya Dkt. Wilbrod Slaa na Hamad Rashid na CCM wameshindwa kuelewana, mimi ndio niliyeitwa ku-facilitate maelewano hayo. Sasa naomba nimnukuu Dkt. Wilbrod Slaa, Kiongozi wa Upinzani wakati huo Bungeni, ambaye aliongea baada ya Halima Mdee kumaliza kuongea; anasema hivi: “Kwa bahati mbaya, Waziri ame-quote mifano ya mtu mmoja mmoja walioleta hisia zao, lakini taarifa ya mwisho iliyokuwa summed up na Profesa Kabudi ambaye alikuwa rapporteur wetu ambaye mimi ndiye nikaja kuwakilisha, haikusema hivyo.” Mwaka 2007 brokered, compromise between the opposition and CCM, tena na Dkt. Slaa na Hamad Rashid. (Makofi)

Kwa hiyo, mtu yeyote ambaye ana wasiwasi au anaishi kwa hofu ya Kabudi, aendelee kuishi na hofu hiyo. Yeyote anayeishi na hofu ya Kabudi aendelee kuishi na hofu hiyo. Kabudi hatatetereka, Kabudi hataacha kufanya kazi. Kwa hiyo hatatetereka, ishini na hofu ya Kabudi, Kabudi anaishi kwa neema ya Mungu. (Makofi/Kicheko/Vigelegele)

Mheshimiwa Naibu Spika, msisahau ndani ya Bunge hili, mimi kwenye timu hii nimeingia wakati wa dirisha dogo. Nimesajiliwa kwenye dirisha dogo, hilo mlifahamu. Kwa hiyo, endeleeni kuishi na hofu ya Kabudi, endeleeni kuishi na husuda ya Kabudi, endeleeni kuishi na wivu wa Kabudi, lakini yeye atafanya kazi bila uoga wala bila kutetereka, kwa sababu nchi yangu ni muhimu kuliko mimi mwenyewe. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Mama yako!

WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, nchi hii ni kubwa kuliko sisi wote, kwa hiyo, nitaitumikia nchi hii bila uoga, bila wasiwasi, bila chuki kwa sababu ni wajibu niliyoitiwa na mwezi huu ni Mwezi Mtukufu wa Ramadhan, nawaomba wote muisome Surat Yussuf mtaelewa. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Ipo.

WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Wakristo mkasome kitabu cha Mwanzo Sura ya 42 mpaka 48 kisa cha Yusufu na nduguze, mtajua. Huyu ndio Yusufu, msimpeleke utumwani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kueleza hayo, naomba kutoa hoja. (Makofi)