Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. Baada ya kuunga mkono hoja hii muhimu ya Wizara ya Nishati, naomba pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri na Naibu wake pamoja na watendaji wote wa Wizara hii kwa kazi kubwa wanayoifanya ya kuitoa Tanzania gizani na kutupatia nishati ya kuendeshea viwanda.

Mheshimiwa Spika, pia naomba kuishukuru Serikali kupitia Waziri kwa kututengea fedha kutoka fungu la TANESCO kwa ajili ya kupeleka umeme Makao Makuu ya Tarafa ya Ketumbeine yenye vijiji 20 ambavyo tangu mradi wa REA kuanzishwa nchini hadi leo hawajafaidika bado kupata umeme.

Mheshimiwa Spika, kwa ajili ya ufanisi na uendelevu wa mradi mkubwa wa Stiegler’s Gorge, naomba kushauri Serikali iwekeze kwa makini katika zoezi la kuhakikisha kuwa vyanzo vyote vya kupeleka maji kwenye Bwawa la Stiegler’s Gorge yahifadhiwe na kutunzwa kwa gharama yoyote.

Mheshimiwa Spika, pili, katika usanifu unaoendelea na ujenzi wa Stiegler’s Gorge Dam, ni vizuri Serikali izingatie na kujipambanua namna ya kukabiliana na athari zinazoweza kujitokeza kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi. Serikali iwekeze katika kuwatafutia wananchi wanaotegemea maji ya vyanzo vinavyopeleka maji hadi Bwawa la Stiegler’s Gorge vyanzo vya mbadala ili maji yote yaelekezwe katika mradi huu wa kuzalisha umeme kwa ajili ya utoshelevu na uendelevu wake majira yote ya mwaka hata katika majira ya ukame.

Mheshimiwa Spika, mwisho naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha hoja yake ayajibu maswali mawili yafuatavyo; moja, ni lini vijiji 30 vya Wilaya ya Longido ambavyo bado havijafikiwa na umeme wa REA; watapata nishati hii? Ni vijiji vingapi vimeingizwa katika bajeti ya mwaka huu wa 2019/2020?

Mheshimiwa Spika, kuna vijiji ambavyo vimeshafikiwa na umeme lakini makazi yameongezeka na kuna vitongoji vingi havijapelekewa umeme bado. Mwaka huu wa fedha 2019/2020 Serikali imetenga fedha za kufanya ujazilizi katika vijiji vya Wilaya yangu ya Longido. Kati ya maeneo ambayo yana uhitaji mkubwa wa mradi wa ujazilishi ni pamoja na vijiji vya Mundarara kwenye machimbo ya madini ya Ruby, Mairowa (Kata ya Engarenaibor), Namanga, Longido, Olmolog, Elerai, Kamwanga na vijiji vyote 20 vya Tarafa ya Ketumbeine ambavyo bado havijafikiwa na umeme wa REA.

Mheshimiwa Spika, kwa haya machache, nashukuru na natamka tena kuwa naunga mkono hoja.