Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati

Hon. Vedasto Edgar Ngombale Mwiru

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati

MHE. VEDASTO E. NGOMBALE: Mheshimiwa Spika, shukrani kwa kunipa nafasi. Nianze kwa kutoa pongezi kwa Waziri na Naibu Waziri, mnafanya kazi nzuri, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi leo nitajikita zaidi katika maeneo ambayo yana tatizo kubwa sana, hasa kwenye suala zima la fidia. Wakati wa utekelezaji wa mradi wa gesi pale katika Kituo cha Somanga Fungu, walipokuwa wanapeleka umeme maeneo ya Rufiji na Ikwiriri wakati wa ujenzi wa njia ile ya umeme TANESCO ilifanya fidia kwa wananchi, lakini ilipofika katika Kijiji cha Somanga walifanya fidia na wakawasahau wananchi tisa.

Mheshimiwa Spika, Nimekuwa nikifuatilia fidia ya wananchi hawa mpaka leo haijapatikana, naomba niwataje. Kuna mwananchi anaitwa Mohamed Mtombwane, Amir A. Mtauka, Athuman Kiwanga, Mpara, Mwinchande Mtauka, Yusuph Masendela, Ally Gumbi, Athuman Mchoro na Rashid Matana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Hawa wananchi wananikera sana na suala hili mara nyingi nakuwa nawasiliana na watu wa TANESCO lakini mpaka sasa fidia zao hazijalipwa, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja basi awaone hawa wananchi, ni muhimu sana hawa wananchi walisahaulika.

Mheshimiwa Spika, lingine, wakati wa utekelezaji wa mradi huo huo, kuna eneo TANESCO walichukua pale Somanga Fungu, kulikuwa kuna eneo la wananchi lakini kuna eneo lilitambulika kama eneo la Kijiji, TANESCO ilifanya tathmini na ikaja kufidia. Wakati inakuja kufidia kwa bahati mbaya sana wananchi wakasema hapana lile eneo siyo la Kijiji ni la wananchi na wakajitokeza wananchi 63. Wakati hilo linafanyika tayari cheque ilishakuwa imeandaliwa, kukawa na mvutano matokeo yake zile pesa zikawa zimerudi tena TANESCO.

Mheshimiwa Spika, Nimefuatilia sana tangu mwaka 2015 mpaka sasa wananchi 63 hawajapata fidia ya yale maeneo na maeneo yale yameshatumiwa na TANESCO. Kwa hiyo naomba sana, wananchi hawa fidia hizo wapate. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine nizungumzie suala la mradi huu sasa kilovoti 400 ambao sasa unaendelea. Mradi huu una malalamiko makubwa sana hasa maeneo ya Somanga. Ifahamike eneo la Somanga ndilo eneo la kwanza ambalo limeanza kutoa umeme wa gesi kutokea Songosongo; lakini katika hali isiyoeleweka Mradi huu wa kilovoti 400 unafanyiwa tathmini na tayari asilimia 79 ya watu wameshaanza kulipwa.

Mheshimiwa Spika, Mradi huu ni wa Somanga fungu Kinyerezi, lakini TANESCO wameanza kulipa Kinyerezi na bado hawaja walipa watu wa Somanga ambako gesi yenyewe imetoka, sasa kuna maneno ambayo hayapendezi maana wale wananchi wananiuliza kwani sisi TANESCO wanatuona malofa au kwa kuwa tuko Kilwa, kwa nini, waanze kuwalipa watu wa Dar es Salaam na siyo sisi ambako gesi yenyewe ndiyo imeanza kutoka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Tumefatilia sana na sasa ni kama mwaka wa nne, mlichukua maeneo yao, wanashindwa kufanya shughuli za Kilimo, lakini bado hamtaki kufanya fidia, nikuombe Mheshimiwa Waziri utakapokuja basi uje na maneno yenye faraja kwa ajili ya malipo ya wale watu wa Somanga ambao wao ndiyo nafikiri ilipaswa wawe watu wa kwanza kufidiwa na si watu wa Kinyerezi kama ambavyo mlifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jingine, nijielekeze sasa kwenye suala zima la REA, naomba katika awamu hiyo sasa inayokuja basi TANESCO waangalie Kata ya Kandawale, Kata ya Kandawale, Kata nzima haijapata umeme ina vijiji vinne kuna Kijiji cha Kandawale, Mpopela, Ngarambi na Namatewa, lakini katika Kata ya Miguruwe kuna Kijiji cha Zinga, Kibaoni, Mtepela na Kingombe hawajapata umeme, lakini waangalie pia Kijiji cha Mwengei, Mkarango, Namakoro, na Nambondo havijapata umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Jingine ambalo ningesema ni suala zima la ujenzi wa Kiwanda cha Mbolea pale Kilwa Masoko. Inashangaza katika bajeti zilizokuwa zinapita taarifa za ujenzi wa Kiwanda tulikuwa tunaona katika hotuba ya Waziri, lakini katika hali ya kushangaza mwaka huu hatujaona chochote hakijasemwa chochote. Sasa Mheshimiwa Waziri awe wazi tu katika aina hii ya gesi tuliyoipata, maana sisi tumepata gesi kavu, gesi ambayo haija-associate na mafuta, je upo uwezekano wa kujenga Kiwanda cha mbolea ambacho kitakuwa kina manufaa, naomba Waziri aje atueleze hili kuliko kuwa tumebaki na matumaini, ahsante. (Makofi)