Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati

Hon. Dr. Shukuru Jumanne Kawambwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bagamoyo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati

MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Spika, nakushuru sana kwa kunipa fursa hii ya kuchangia hoja ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati. Awali kabisa niungane na Waheshimiwa Wabunge walioongea kumpa pongezi sana Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kazi nzuri wameendelea kuifanya katika sekta hii. Pia nampongeza Katibu Mkuu na watumishi wote wa Wizara ya Nishati kuendelea kufanya kazi nzuri ya kulijenga Taifa hili.

Mheshimiwa Spika, naipongeza Serikali kwa Mradi wa Stiegler’s kwa kweli mradi huu ni mradi wa maendeleo na mkombozi sana wa maendeleo ya kiuchumi na kijamii yetu. Megawatts zile 2,115 zitatuchangia sana katika kuendeleza huduma ya maji, huduma ya afya, huduma za kielimu, viwanda, standard gauge, reli na kadhalika. Kwa kuzingatia lengo ni megawatts 10,000 ifikapo mwaka 2025 ni kwamba Mheshimiwa Waziri ajitahidi mapema hata kabla ya miaka mitatu kwa sababu tunahitaji bado Megawatts nyingi sana kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nishukuru pia kwa niaba ya Mkoa wa Pwani kama sisi wenyeji wa mradi huu kwa kweli tumeupekea kwa mikono miwili na tutajitahidi kwa kila hali kuhakikisha kwamba unafanikiwa na madhara yoyote yanaweza kujitokeza ya kimazingira bila shaka Tanzania tunao watalamu wetu wazuri ambao watajipanga kwa ajili ya kudhibiti madhara yoyote ya kimazingira.

Mheshimiwa Spika, ningependa kuzungumzia ahadi zile ambazo zinatolewa kwa ajili ya kupeleka umeme vijiji na maeneo yote yanaahidiwa kupelekewa umeme vijjijini ni vizuri sana tukatekeleza ahadi hizo Waswahili wanasema ahadi ni deni. Katika Jimbo la Bagamoyo, Kijiji cha Kondo kilikuwa katika Mradi wa REA awamu ya pili mpaka Juni, 2016, mradi ulipomalizika kutekelezwa. Katika REA, awamu ya tatu, mzunguko wa kwanza mpakaleo hicho kijiji hakimo kabisa na wala hatujui lini kitatekelezwa. Hata hivyo, Mheshimiwa Waziri aliahidi hapa Bungeni kwamba miradi yote ambayo itakuwa haijatekelekezwa katika awamu ya pili, basi itapewa kipaumbele katika awamu ya tatu.

Mheshimiwa Spika, Sasa hili ni jambo ambalo kulitekeleza ni muhimu sana kwa sababu ni ahadi ya Mheshimiwa Waziri na wananchi wakiwa wamesubiri tangu 2013, awamu ya pili ya REA mpaka leo 2019 wanasubiri, hata Mbunge akizungumza namna gani wanamwona tu kama anapiga maneno hana kitu cha kweli ambacho anaendelea kukisema. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri aendelee na ahadi yake ile ile ya first in first out. Waliokuwa kwenye awamu ya pili wapate na nisisitize katika awamu ya tatu waanze wao kutekelezewa kabla ya wengine.

Mheshimiwa Spika, naomba kushauri kwamba kwa ufanisi wa miradi hii ya umeme vijiji basi REA izingatie mapendekezo ya Wabunge ambayo yanawasilishwa kwa utaratibu ambao umewekwa kwa maana kupitia katika ofisi za TANESCO Wilaya na TANESCO mikoa. Baada ya hapo inapelekwa REA lakini wasifanye vinginvyo. Katika Jimbo vya Bagamoyo vitongoji saba katika Kata ya Dunda vimeorodhesha katika awamu tatu ya REA ambavyo vyenyewe vina umeme, hakuna mahali pa kuweka umeme na havikupendekezwa na TANESCO Wilaya wala havikupendekezwa na TANESCO Mkoa, vimekuja namna gani?

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nawaomba wataalam wa REA wawe wanaangalia mapendekezo ya Wabunge na hasa yale ambayo yamepita katika taratibu zilizowekwa na hiyo ndio dira ya kutekeleza miradi hiyo isiwe wanachomekea chochote ambacho wamekipenda hata ambapo umeme upo hakuna shida yoyote wananchi wenyewe wanashangaa. Vile vitongoji ni vya Mjini Bagamoyo, hakuna nyumba ambayho haina umeme, vikawekwa mle. Kwa hiyo haina tija, badala yake tunahangaika kutoa scope mahali pamoja kupeleka sehemu nyingine katika hali nzito sana.

Mheshimiwa Spika, ningependa kumalizi kwa kusema kwamba tunapotekeleza miradi hiii katika vijiji basi msisitizo uwe, Kijiji kile ikiwezekana basi kiwekewe kwa ujumla wake badala ya kuweka vijiji kwa mfano katika Jimbo langu, Kata ya Yombo, Kijiji cha Matimbwa kimewekewa umeme, lakini siyo kijiji chote, vitongoji kadhaa havina umeme, Kongo kadhalika. Kwa hiyo, hilo ni jambo ambalo linafaa liangaliwe kwa umakini.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi hii na naunga mkono hoja. (Makofi)