Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili pia na niweze kuchangia katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati. Kama wenzangu walivyokwishakutangulia kusema Wizara hii inao watendaji wazuri sana. Na kwa maana hiyo, nipende tu kwa kweli, kuwapongeza; nimpongeze Ndugu yangu Mheshimiwa Medard Kalemani na dada yangu Mheshimiwa Subira Mgalu kwa kazi nzuri sana ambayo wanaendelea kuitendea nchi yetu. Ninaamini kabisa kwamba, Tanzania ya viwanda inakuja na niseme tu kwamba, kwa kweli, ninaunga mkono shughuli mbalimbali ambazo zinafanywa na Wizara hii ukiwemo mradi mkubwa wa Stiegler’s Gorge ambao unatekelezwa na Taifa letu ambao tunatarajia kupata megawati 2100. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninajua kwamba, lengo letu kama Serikali ni kupata megawati 10,000 ifikapo mwaka 2025. Nina imani kubwa kwamba, ndani ya kipindi hicho kama kweli watendaji hawa wataendelea na morali waliyonayo ninaamini kabisa kwamba, Tanzania itafikia uzalishaji wa megawati 10,000 kipindi hicho kitakapokuwa kimefikia na Tanzania ya viwanda itawezekana kwa sababu, hakuna viwanda bila kuwa na nguvu za umeme zinazoweza kuwa za uhakika tukaweza kufanikiwa kwenye sekta hiyo. Kwa hiyo, niseme tu kwamba, kwa kweli Wizara hii imekuwa ni Wizara ya mfano.

Mheshimiwa Spika, na kwa wale ambao wanapinga kuendelea kuzalisha umeme katika Stiegler’s Gorge na wanaosema kwamba, wao wanataka return kwenye REA ambayo imewekezwa katika Tanzania hii, basi mimi niwaombe kwamba, kwa kweli, wabadilike mawazo kwa sababu, Watanzania ambao wamepata huduma hii ya umeme kupitia Mradi wa REA na TANESCO leo hii ukisema kwamba, uuzime au uondoe hiyo huduma, kelele ambazo utazisikia hapo hutakaa usahau. Kwa hiyo, nimeona kwa mfano kabisa katika Wilaya yangu ya Mbogwe baada ya huduma hii ya umeme kuwekwa kwa Wananchi, Wananchi kwa kweli wamefurahia huduma hizi na kwamba, maisha yamekuwa marahisi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niombe tu kwamba, utekelezaji wa Mradi huu wa REA Awamu ya III uendelezwe kwa kasi zaidi na kwamba, wakandarasi kama wewe Mheshimiwa Kalemani umekuwa ukifika mara kwa mara katika Wilaya yangu ya Mbogwe na umehamasisha utekelezaji wa Mradi huu wa REA Awamu ya III, lakini naona kasi bado kidogo, lakini naomba tu kwa kweli, Mungu akujalie na msaidizi wako Mheshimiwa Mgalu muendelee kufanya kazi hii kwa ustahimilivu ambao mnauonesha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kingine nikushukuru Mheshimiwa Waziri baada ya kuwa umekuja umeweka umeme katika eneo la Nyakafuru, wachimbaji wangu wadogowadogo katika eneo hilo la dhahabu ninaamini kwamba, kwa kweli shughuli za uzalishaji wa dhahabu katika eneo la Nyakafuru litakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la pili ninachotaka kuomba tu ni kwamba, REA imekuwa inatoa huduma katika maeneo machache. Naomba ule mradi wa densification na wenyewe ufanyiwe wepesi, ili kusudi uanze utekelezaji mara moja. Na vile vijiji ambavyo bado havijafikiwa katika utekelezaji wa REA naomba Serikali ifanye haraka ili ikiwezekana mwaka 2020/ 2021 vijiji vyote viweze kuwa vimepata hii huduma ya umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nasema haya kwa sababu, tumeshuhudia kwamba maeneo mbalimbali yanachangamka sana yanapopata huduma hii ya umeme. Kwa hiyo, niombe tu kwamba, kwa kweli, kwa wale ambao watakuwa hawahitaji umeme kwao basi, huko Mbogwe sisi tunauhitaji kwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema maneno hayo mimi naomba tu niendelee kuwaombea kwa Mungu Wizara hii waendelee kufanya kazi zao kwa ukamilifu, ili kusudi Tanzania ya viwanda iweze kufikiwa. Baada ya kusema hayo naomba kuunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri asilimia 100 kwa 100, ahsante sana. (Makofi)