Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati

Hon. Nape Moses Nnauye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtama

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nichangie kwenye mapendekezo ya bajeti hii ya Wizara ya Nishati. Nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri na Naibu wake kwa kazi nzuri wanayofanya, wanafanya kazi nzuri sana na wasaidizi wao. Kwa kweli katika Mawaziri wasikivu na wanyenyekevu nadhani Mheshimiwa Kalemani na msaidizi wake wanafanya kazi nzuri sana. Na hii haimaanishi kwamba, hakuna changamoto, lakini usikivu wao na unyenyekevu wao unapunguza sana machungu ambayo yangekuwepo kwenye Wizara hii kwa hiyo, kwa kweli nawapongeza na nadhani waendelee hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili nataka niipongeze sana Serikali kwa kuhuisha, kwa kufufua na kuendeleza mazungumzo juu ya mradi wa uwekezaji pale Lindi wa LNG. Tulipiga kelele hapa, nadhani bajeti mbili zilizopita, lakini Serikali imesikiliza na imehuisha na Mheshimiwa Waziri juzi umekuja Lindi kwa mazungumzo yale tunayo matumaini sasa kwamba, mradi huu ambao kwa kweli kwanza ni mkubwa kuliko miradi yote mikubwa katika nchi yetu na hata ukijumlisha ukichukua reli, ukachukua ATC, ukachukua Stiegler’s, ukijumlisha kwa pamoja Mradi wa LNG bado una thamani kubwa kuliko miradi yote kwa pamoja. Kwa hiyo, naamini uamuzi huu ni uamuzi wa busara, uamuzi mzuri, nimesimama kuipongeza kwa dhati Serikali yangu kwa kazi nzuri mnayofanya kwenye mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mradi huu pamoja na kwamba, ni mkubwa lakini mradi huu ni ushahidi wa ushiriki wa sekta binafsi katika kuendeleza miradi mikubwa ya namna hii kwa sababu, hela za Serikali zitakazoingizwa ni kidogo sana. Sehemu kubwa ya fedha hizi karibu dola bilioni 30 ni fedha ambazo zinaletwa na sekta binafsi kwa hiyo, ni mfano mzuri wa ushiriki wa sekta binafsi katika uendelezaji wa miradi mikubwa. Ninaipongeza Serikali kwa uamuzi huu, sasa ninayo mapendekezo mawili yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, la kwanza tukamilishe mazungumzo yamechukua muda mrefu na wenzetu wanaotuzunguka wata-take advantage ya kuchelewa kwetu na halitakuwa jambo zuri. La pili, ushiriki wa wazawa, local contents kwenye huu mradi, Serikali haiwezi kukwepa wajibu wake, tukiwaachia wazawa peke yake ushiriki wao utakuwa mdogo; wito wangu kwa Serikali vizuri Serikali ikajihusisha kwenye maeneo mawili, moja kuzionesha fursa na kuwapa elimu wazawa ili washiriki vizuri, lakini ya pili kuwawezesha hawa wazawa washiriki.

Mheshimiwa Spika, nchi za wenzetu huwaachi wananchi wako wakaenda wenyewe. Ukiwaacha wataenda kushiriki kuuza nyanya, lakini kama tunataka washiriki kwa ukweli kwenye Wizara yako, lakini Wizara ya Uwekezaji, vizuri tukaanzisha room ambayo itawachukua wazawa na kuwawezesha kiuchumi ili washiriki, ili local content yetu iwe nzuri. Kwa hiyo, pamoja na pongezi, lakini malizeni mazungumzo ya huu mradi, lakini pia Serikali ijipange kuwawezesha wazawa kushiriki kwenye huu uchumi mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili nataka nimpongeze pia Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri anayofanya kwenye REA yeye na Naibu wake. Wanafanya kazi nzuri sana, wanakimbizana sana, najua wakandarasi kwenye maeneo mengi wanawaangusha kwa sababu kasi yao ndogo, lakini kwa kweli mnyonge mnyongeni, Waziri Kalemani na Naibu wake wanafanya kazi nzuri, wanakimbizana, wanajituma. Ninaamini kama kuna Wizara Mheshimiwa Rais ameweka Mawaziri wazuri, hii Wizara amefanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninayo mapendekezo mawili; la kwanza nadhani ni vizuri tukaligawa Shirika letu la TANESCO, mapendekezo haya yamekuwa yakizungumzwa. Hebu fikirieni kwa miaka mingi inazungumzwa tugawe uzalishaji, usambazaji na uuzaji yawe ni maeneo tofauti yanayojitegemea, itasaidia sana kuboresha utendaji wa Shirika letu la TANESCO. Na kwenye upande sasa wa uzalishaji kwa sababu tunakwenda kwenye kuzalisha umeme kwa kutumia vyanzo tofauti, vizuri tukavutia wawekezaji binafsi kutoka kwenye private sector watusaidie kwenye kazi ya kuzalisha umeme halafu kazi ya kusambaza iendelee. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Ninaunga mkono hoja na mapendekezo ya Wizara hii, ahsante sana. (Makofi)