Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati

Hon. Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia Wizara ya Nishati, Wizara ambayo ni muhimu sana kwa uchumi wetu wa Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Dkt. Kalemani, kwa kazi kubwa anayoifanya kwenye Wizara hii; Naibu Waziri wetu ambaye ni Mheshimiwa Subira Mgalu; Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu, Mkurugenzi wa REA, kwa kweli kazi wanayoifanya ni kazi ya uhakika nichukue nafasi hii kipekee kabisa kuwapongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napongeza kwa sababu gani, kwa kweli kwa kipindi kirefu, kumekuwa na tatizo kubwa la umeme, vijiji vingi katika nchi ya Tanzania vilikuwa havina umeme, lakini leo hii kutokana na taarifa ni vijiji vingi sasa vya Tanzania vimeweza kupatiwa umeme, vijiji zaidi ya 5,000 ni jambo ambalo la kipekee sana, tunapenda kupongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nipongeze kwa ajili ya mipango iliyopo, kwa sababu mpaka mwaka 2020 wanakusudia kufikia vijiji zaidi ya 10,278. Kwa hiyo mimi binafsi nina imani kubwa kwamba hata kwenye Jimbo langu la Busanda, vijiji vyote vitaweza kupatiwa umeme kwa mpango huu ambao wameuweka.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Kanda ya Ziwa kuna Mradi mkubwa wa umeme wa kilovoti 220, kutoka Bulyanghulu kwenda Geita na mradi huu unapitia katika maeneo katika Jimbo langu la Busanda. Naomba sana, kwamba kupitia mradi huu viko vijiji 10 ambavyo vinatakiwa kupata umeme huu wa gridi ya Taifa, hivyo basi wakati ambapo utekekelezaji unavyoendelea naomba vijiji hivi viweze kupatiwa umeme mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na pongezi hizo pia, jana nilikuwa napiga simu kule jimboni nimeambiwa tayari Wakandarasi wako wanafanya kazi maeneo ya Bujura. Kwa kweli, ni kiasi cha kupongeza kwa kazi kubwa ambayo Wizara inafanya kwa kweli wanafanya kazi njema sana kwa ajili ya Watanzania wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, najua kwamba suala la umeme, ni suala muhimu sana, ili tuweze kufikia uchumi wa kati katika Taifa la Tanzania, lazima vijiji vyetu viweze kupata umeme wa uhakika na ndiyo kazi ambayo Serikali inafanya kwa sasa hivi. Kwa hiyo niombe Serikali iweze kuongeza bajeti kwenye Miradi ya REA, kwa sababu REA ndiyo ambayo tunaitegemea kuweza kusambaza umeme vijijini. Kwa hiyo niombe sana bajeti ya REA, iweze kuongezeka zaidi ili hatimaye basi vijiji vya Tanzania viweze kupatiwa umeme kupitia REA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile napenda pia kuiomba Serikali kwamba wanapofanya utekelezaji wa miradi hii umeme vijijini wahakikishe kwamba zile sekta muhimu za umma kwa mfano, katika shule, Vituo vya Afya, pamoja na sekondari, kwenye huduma za kijamii, tuhakikishe kwamba umeme huu unapelekwa kipaumbele katika sekta hizo. Nasema hivyo kwa sababu, katika maeneo mengi ya vijijini ambako wamepata umeme, unakuta shule hazina umeme, Vituo vya Afya havina umeme, mfano tu Bukoli pale umeme wamepata umeme tangu mwaka 2014 lakini hivi sasa naongea Kituo cha Afya Bukoli hakijaweza kupatiwa umeme mpaka sasa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Kengele imeshagonga Mheshimiwa Bukwimba, ahsante sana.

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja ili waweze kutekeleza miradi hiyo katika vijiji hivyo. (Makofi)