Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia Bajeti hii ya Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitachangia vitu vitatu, lakini awali ya yote niipongeze Wizara, nimpongeze Waziri, Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla pamoja na Naibu Waziri, Mheshimiwa Kanyasu, kwa kazi nzuri wanayoifanya. Nimpongeze pia Katibu Mkuu wa Wizara hii pia kwa kazi nzuri na ushauri mzuri, pamoja na watendaji wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee kabisa niwapongeze Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro, Ndugu Manongi pamoja na wa TANAPA Ndugu Allan Kijazi, kwa kweli wamekuwa na mchango mkubwa sana kwa Tanzania na hasa kwa mimi ninayetoka Mkoa wa Arusha nawapongeza sana kulingana na kazi nzuri wanazofanya za kijamii, na hasa katika kuwasaidia wanawake. Hongera sana Ndugu Manongi pamoja na Ndugu Allan Kijazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitazungumzia katika upande wa promotion na advertisements na hapo ndipo tunapojiuliza nini maana ya utalii. Maana ya utalii pasipokuwa na promotion pamoja na advertisements ni sawa na kazi bure. Tunafahamu umuhimu wa haya mambo mawili katika kuhakikisha kwamba tunautangaza utalii wetu, tunaitangaza Tanzania kimataifa na hapo basi ndipo ambapo tunapoweza kupata watalii wengi kuja nchini Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa bahati nzuri, Nchi ya Tanzania Mwenyezi Mungu ametujalia na tuna kila sababu ya kujivunia kutokana na maliasili zilizopo pamoja na vivutio vingi vilivyopo katika nchi hii. Wakati mwingine ndipo tunapojiuliza kwamba tunasemwa ni nchi maskini, au sisi maskini; umaskini wetu unatoka wapi wakati tuna utalii, tuna maliasili na tuna mambo mengi ambayo yanaweza kutuletea fedha za kigeni na hatimaye kumkomboa Mtanzania?

Mheshimiwa Naibu Spika, jana tuliona wageni waliofika hapa ambao kwa namna moja wamechangiwa na Wizara hii kuweza basi kuja hapa na kwa namna moja au nyingine, hasa yule Miss Ukraine. Hata hivyo, nitakwenda kwa upande wa hapa nyumbani kwetu kuona ni kwa jinsi gani tunawatumia Watanzania ambao wameonesha mafanikio makubwa katika kuwa-brand na wao sasa wakatumika kama mabalozi wetu kuweza kuutangaza utalii wa Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, juzi nilisimama kwa Mbwana Samatta na nitaendelea kumzungumzia Mbwana Samatta kutokana na kazi nzuri aliyoifanya ya kuitangaza ramani ya Tanzania kupitia soka la kulipwa kule Nchini Ubelgiji. Wizara inapaswa sasa basi kumtangaza kama huyu ni balozi ili aweze kuendelea kuutangaza utalii wetu kule.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mbwana Samatta kwa bahati nzuri sana amefanya mazungumzo na daktari wa hiyo timu na amehamasika kuja kutembelea Tanzania. Kama ameweza kufanya hivyo, kaka yangu, Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla, kaka yangu, Mheshimiwa Kanyasu, kwa nini tusimtangaze huyu na kumtumia kuwa kama ni brand Balozi, kuweza kuitangaza nchi yetu na kuutangaza utalii wetu kwa kupitia soka analocheza? Kwa kufanya hivi, Mbwana Samatta ataweza kwa kiasi kikubwa pia kuweza kuwaleta watalii wengi kuja kutembelea nchi yetu na hatimaye kupata pesa kutokana na wale watakaokuja hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, juzijuzi tumemuona mwanadada Azara Charles ambaye tumekuwa tukimuona ni mtu wa kawaida akikaa chini na kupiga zile danadana. Lakini Azara ameweza kumhamasisha kiasi kwamba mpaka Rais wa Taifa kubwa la Marekani, Donald Trump, kuweza kumzungumzia mwanadada huyu ambaye sisi Watanzania tumemwona kwa muda mrefu tukimchangia vipesa vidogovidogo na tayari sasa Azara ameingia mkataba na Kampuni ya Nike.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa je, sisi kama Watanzania tunamtumiaje Azara ili kuweza kuutangaza utalii wetu huko atakakokwenda? Hii itasaidia kwa Watanzania. Lakini pia wasanii wetu na wanamuziki mbalimbali na wao pia mbali ya kufaidika, lakini Taifa tutaweza kufaidika mara mbili zaidi kutokana na kazi zao au vipaji vyao wanavyovifanya. Na…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Amina.