Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. DKT. STEPHEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia hii hoja muhimu ya Wizara yetu ya Maliasili na Utalii ambayo na mimi ni mjumbe wa kamati yake ya kudumu. Kwa hiyo mambo mengi ambayo ningependa kuyasemea bahati nzuri yapo katika ripoti ya makini tuliyoandaa kama kamati. Kwa sababu nimepewa dakika 5 sina muda wa kuyapitia hayo ila nina maswali machache ambayo nitamuomba Waziri na kweli azingatie ayatolee ufafanuzi baadaye atakapokuja kuhitimisha hoja yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la kwanza ni kwenye haya maeneo ya jumuiya ya hifadhi ya wanyamapori ambayo tunaita WMAs na nitatumia mfano wa WMA ya Jimbo langu ya Enduimet. Naomba Mheshimiwa Waziri utakapokuja kuhitimisha hoja yako baadaye unipatie ufafanuzi kuhusu hili suala la kucheleweshwa kwa mgao wa fedha za WMA zinazotokana na upigaji picha (photographic safaris) na hizi za uwindaji. Maana kwenye mfumo zinapokelewa, na tulitegemea kila mwezi baada ya watalii kupita, wanapewa mgao wao, baada ya msimu wa uwindaji kufanyika wanapewa hela yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, uhalisia ni kwamba haiji kwa wakati na ukweli ni kwamba hii inaathiri sana shughuli za uhifadhi kuwalipa ma-game scouts na kufanya shughuli nyingine za kulinda rasilimali lakini pia inachelewesha miradi ambayo vijiji vilivyotenga maeneo yao yahifadhiwe yalishabuni na walikuwa wanategemea hayo mapato ili waweze kujiletea maendeleo waone manufaa ya eneo walilolitenga.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ambalo Mheshimiwa Waziri nitakuomba utoe ufafanuzi baadaye ni kuhusu utaratibu usiwafurahisha wanajamii wa WMA, labda zote lakini mimi naseme ya Enduimet ambayo ndiyo ya pekee tuliyonayo ambayo imeshasajiliwa ya uwindaji. Hawa jamii ya WMA wanao watu wao waliondaliwa tayari wamefunzwa, wapo village game scouts wanajua kusimamia, kukagua na kusaini vibali; lakini uhalisia ni kwamba wanapokuja wale viongozi wa idara ya wanyamapori wanawaleta wawindaji wanawa-bypass, hawawashirikishi, na wanasahau kwamba hawa ni watu waliajiriwa na jamii yenyewe waliopewa mamlaka kamili na ambao wanaaminika, wanalalamika kwamba kulikoni mamlaka yao yanaporwa wakiangalia mbona hawashirikishwi. Mheshimiwa Waziri utakapokuja baadaye naomba utolee ufanunuzi hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo linahitaji ufafanuzi maana nimejikita kwenye WMA kama eneo nyeti, ni hili la hii Jumuiya ya Enduimet ambayo imetokea sintofahamu baada ya eneo lao la uwindaji lenye hadhi ya grade A, grade namba I kushushwa hadi kuwa grade namba II bila kuwashirikisha wanajumuiya na kusababisha kupoteza mapato yanayotokana na uwindaji katika eneo la grade A kwa asilimia 50. Jamii imeshikwa na taharuki wanashangaa kwa nini hawajashirikishwa, pengine kuna vigezo vya msingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri utakapokuja hapa hebu uwaambie wananchi wa Enduiment kulikoni maana wamejipanga kuja kukuona ofisini lakini waliposikia leo nitachangia hapa, wakaomba nilisemee mbele ya Bunge zima ijulikane kwa sababu wao walishaingia mkataba na muwekezaji kwamba wamemsainisha grade A lakini wameshalipwa kwa mara ya kwanza malipo ya grade II ambayo ni nusu ya malipo ya grade A.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo nilipenda kulisemea kwa haraka haraka kwa sababu dakika zangu zinaisha, ni oparesheni za kudhibiti wawindaji haramu. Mimi naunga mkono asilimia 100 kudhibiti wawindaji haramu kwa sababu kizazi hiki na vijavyo vitategemea rasilimali hii ya wanyamapori. Lakini kuna utaratibu unaotumika ambao unawasababishia watu na raia wasio na hatia kutiwa hatiani na kuumia karibu yote magerezani.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi ninavyoongea, nina barua hata hapa ya mmoja lakini sitaweza kusoma kwa sababu ya muda, wapiga kura wangu waliopo mahabusu wananiandikia. Kuna mmoja hapa sitaki kumtaja hata jina namhifadhi, lakini amewekwa mahabusu takriban miaka miwili sasa, tangu mwaka 2017 na kosa alilolifanya niliamini kwamba vyombo vilivyopo vinavyobaini watuhumiwa vina uwezo wa kuwadadisi, kuwafikisha mbele ya vyombo vya sheria, kuwahukumu na kuwafunga wasio na hatia na kuwaachia wasio na hatia. Kuna watu wanatumika kuwarubuni watu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kiruswa, kengele imegonga, lakini naona una barua ya huyo mtu; nadhani unaweza kuwaona watu wa Serikali, utawaona wao na orodha yako yote wewe wakabidhi ili sasa uweze kuwafuatilia, kwa sababu hata ukitaja hapa na wao watahitaji muda wa kuifuatilia.