Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Juma Kombo Hamad

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Wingwi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Awali ya yote nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya njema mchana huu na kupata fursa hii ya kuchangia kwenye bajeti hii ya Wizara muhimu, Wizara ya ELimu.
Pili kwa sababu ni mara ya mwanzo kabisa nichukue fursa hii pia kuwashukuru wapigakura wangu wa Jimbo la Wingwi kwa kunipatia ushindi mkubwa wa asilimia 90 dhidi ya mgombea mwenzangu. Pia nikishukuru chama changu, Chama cha Wananchi (CUF) kwa kuniamini kabisa na kunipa fursa hii, nakiahidi kwamba sitakiangusha, nitakitumikia kwa nguvu zangu zote kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba nianze kwa kusema kwamba ili tufanikiwe na ili tuendelee tunahitaji tuwekeze kwenye suala zima la elimu. Kinachoonekana hapa bado kama vile hatujakuwa tayari kuwekeza katika suala zima la elimu. Kinachoonekana hapa ni kama vile tunakuja kutaniana, kwa sababu kile ambacho kimezungumzwa mwaka wa jana, kile ambacho kimezungumzwa mwaka wa juzi ndicho kile kile kinachopigiwa kelele, hakiongezeki wala hakipungui.
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ambayo ili zungumzwa mwaka wa jana tulipaswa leo tuje tuione angalau imetatuliwa kiasi fulani ili tuondoke pale tulipokuwa mwaka wa jana na sasa tuzungumzie kitu kingine. Lakini hadi sasa wenzangu wengi wamezungumza hapa, tunapiga kelele kwa matundu ya vyoo, tunapiga kelele ukosefu wa madawati na vitu vingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ninamuomba Mheshimiwa Waziri, kwa nia njema kabisa, hebu fuatilia zile hotuba mbili, hotuba ya Kambi ya Upinzani pamoja na hotuba ya Kamati. Kama utazifuata vizuri basi zimetoa mwanga mzuri wa kukuongoza kufikia kule Watanzania tunakokuhitaji. Na wala sioni sababu ya kwamba usifuate mawazo yale ya vitabu vile viwili, ni vitabu ambavyo vimezungumza vizuri, vimetoa mapendekezo mazuri, vimetoa maelekezo mazuri ambayo yatatutoa hapa tulipo na kuelekea pale tunapopahitaji.
Ninakuomba sana mama yangu, kwamba kwa hili bora tu ulifuate ili maelekezo yale ukichanganya na uliyo nayo wewe mwenyewe basi utapata kitu cha kushika na mwakani utatueleza kitu kipya kabisa hapa kwenye Bunge lako hili Tukufu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika uwekezaji huu yamezungumzwa mengi, lakini lazima tukubali kugharamia, lazima tukubali kuchagua vijana tuwapeleke wakasomee taaluma mbalimbali ili waje waisaidie Tanzania; nchi nyingi zimefanya hivyo. Hata China pale ilipo leo kwanza ilianza zaidi miaka kumi kula hasara kwenda kuwasomesha vijana nje ya nchi kusoma kwa ajili ya taaluma fulani ili kwenda kuisaidia nchi yao. Sasa na sisi si aibu wala si fedheha.
Leo kuna mtu alitoa mfano hapa, mpaka leo tunategemea marubani, tunagemea ma-captain wa meli zile ambazo ziko hapa ndani ya nchi yetu ukienda pale unawakuta wote ni wageni. Kwa nini tusiende tukasomeshe wakwetu? Hivi kuna ugumu gani kuwa rubani? Hivi kuna ugumu gani kuwa captain wa meli? Hivi kuna ugumu gani kuwa meneja wa kiwanda fulani au mtandao fulani ambaye huyu atakuwa ni mzalendo wa nchi yetu? Naomba kumshauri Mheshimiwa Waziri afuate yale mawazo, naamini atatukwamua katika hatua hii na tutakwenda katika hatua nyingine nzuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ambalo ninaomba kulizungumzia hapa ni suala la mikopo. Suala la mikopo limekuwa na malalamiko makubwa na ya muda mrefu hasa kwa upande wa Zanzibar. Mimi nikuombe kitu kimoja katika hili, nikuombe wakati utakapokuja, au ujiandae kuanzia sasa, kama utakuwa hujajiandaa basi ujiandae vizuri ili kuwe na utaratibu maalum wa utoaji wa mikopo. Suala la elimu ya juu, suala la Bodi ya Mikopo ni suala la Muungano, Wazanzibari wanahusika katika suala hili, hawapaswi kama vile kuchotewa, kama vile ni waalikwa. Zanzibar si mualikwa katika ile Bodi ya Mikopo, Zanzibar ni mshirika kwa sababu suala la elimu ya juu Kikatiba, kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni suala la Muungano.
Sasa mimi nikuombe tu kwamba uandae utaratibu mzuri, wakati unakwenda kufanya udahili unatuletea hapa bajeti, unaisoma bajeti. Ukionesha kwamba fungu hili ndilo la mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu utuambie basi katika fungu hili kiasi hiki ndicho kinachokwenda kwa wanafunzi watakaodahiliwa watokao Zanzibar. Sioni kama kuna dhambi, sioni kama kuna tatizo hapa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamuomba sana Mheshimiwa Waziri sana kwamba hili ulifanye ili kuondoa haya malalamiko ya muda mrefu. Utakapotuambia, pengine fungu la mikopo lina milioni 40, lakini hizi Shilingi 200,000 zitakwenda kwa wanafunzi wa Zanzibar, wewe utakuwa umejiondoa kwenye malalamiko, na umeitoa wizara kwenye malalamiko. Tutajua tuna wanafunzi wangapi kutoka Zanzibar ambao watapata mikopo kutoka Bodi ya Mikopo ya Tanzania.Nitakuomba sana hili ulichukue, ulifikirie na ulipatie maamuzi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la tatu ambalo ninaomba kulizungumzia hapa ni suala la uwekezaji hasa katika vyuo vikuu. Kumekuwa na malalamiko ya muda mrefu, na Serikali hapa ilifanya jambo kubwa na lenye nia njema kabisa. Suala la uanzishwaji wa sekondari katika kila kata lilikuwa ni suala muhimu, limetekelezwa na Serikali kwa kiasi fulani, hivyo hivyo, lakini lipo na limetekelezwa. Sasa, kuna ukanda huu wa Kusini, baada ya kuanzishwa sekondari hizi za kata imepelekea wanafunzi wengi kujiunga na sekondari za O-Level na A-Level. Udahili wa wanafunzi kwenda vyuo vikuu umeongezeka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini miaka mingi mmekuwa mkisema Chuo cha Ualimu kilichoko Mtwara mtakigeuza kiwe Chuo Kishiriki cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam mpaka leo suala hili halijachukuliwa hatua yoyote. Tunakuomba Mheshimiwa Waziri, kwa heshima zote mama yangu Ndalichako ukija hapa utueleze, kile chuo ni lini kitachukuliwa hatua ya kugeuzwa sasa kuwa Chuo cha Ualimu na sasa kiende kwenye kuwa chuo kishiriki kisaidie ule ukanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mikoa mitatu, Lindi, Mtwara na Ruvuma, huu ni ukanda mmoja, mikoa hii imefuatana kabisa, lakini hakuna hata chuo kikuu kimoja cha Serikali. Tunakuomba sana suala hili lichukuliwe hatua na ni vyema utakapokuja hapa sasa utuambie ni lini suala hili litachukuliwa hatua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie kwa kusema kwamba hakuna elimu bora bila huduma bora za walimu. Muda umefika sasa kuwaonea huruma walimu, wamehangaika muda mrefu sana. Imefika muda sasa kuboresha maslahi ya walimu katika nyanja zote, ukae pamoja na TAMISEMI uboreshe, uone kwa namna gani mtashirikiana kuikwamua kada hii ya walimu katika sekta au katika maslahi ya walimu. Walimu hawa ni wetu, ni Watanzania wenzetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wengi wamekuwa wakisema, hata wewe leo usingekuwa Waziri wa Elimu kama hujapitia kwa walimu. Ulianza darasa la kwanza mpaka ulipofika, waliokuwezesha hapo ni walimu. Hebu wahurumie walimu, waonee huruma walimu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ninaomba mchango wangu kwa leo uwe huo, ninaamini kwamba mawazo yangu haya yatasaidia kwa namna moja ama nyingine kufikia pale tunapopahitaji, ahsante sana.