Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Oliver Daniel Semuguruka

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nianze kwa kuwapongeza Mawaziri husika. Mheshimiwa Luhaga Mpina na Mheshimiwa Ulega, pamoja na Makatibu Wakuu na Watendaji wote wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa Hotuba yao nzuri ya bajeti iliyowasilishwa hapa Bungeni. Sasa naomba kutoa maoni yangu katika Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, changamoto ya malisho kutokana na kutokuwa na Mpango wa Matumizi bora ya Ardhi, hivyo kusababisha migogoro kati ya Wakulima na Wafugaji.

Mheshimiwa Spika, baadhi ya Wilaya katika Mkoa wetu wa Kagera wana maeneo maalum ya malisho hasa yale yaliyokuwa Ranch za Taifa lakini kwa Jimbo la Ngara hakuna maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, changamoto nyingine tuliyonayo ni ya masoko ya mazao ya mifugo, mfano ngozi, maziwa, nyama pamoja na mayai ya kuku.

Mheshimiwa Spika, sababu zinazofanya ngozi nyingi kuwa na ubora wa chini ni pamoja na upigaji wa chapa ovyo hususan katika maeneo muhimu ya ngozi, hali mbaya ya miundombinu ya machinjio, makaro, mabanda ya kukaushia na kuhifadhia ngozi.

Mheshimiwa Spika, nchi yetu ina utajiri mkubwa wa mifugo ambayo ingezalisha ngozi kama malighafi za viwandani na kuongeza pato la Taifa.

Mheshimiwa Spika, shughuli za ufugaji wa samaki nchini unafanywa na wafugaji wadogo wadogo kwa asilimia kubwa. Ufugaji wa samaki hukabiliwa na matatizo na changamoto nyingi, kama ukosefu wa teknolojia bora, upungufu wa vifaranga bora na miundombinu ya usafiri kuwa duni.

Mheshimiwa Spika, changamoto katika sekta ya uvuvi inakabiliwa na upungufu katika sera na sheria, elimu duni juu ya shughuli za uvuvi katika jamii, uvuvi uliopitiliza na hivyo kuathiri rasilimali za uvuvi.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na mwendelezo wa wavuvi kuchomewa nyavu zao za kuvulia kila mara na kumekuwa na matamko kutoka Wizara husika juu ya matumizi ya nyavu sahihi za kuvulia.