Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Kunti Yusuph Majala

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru na mimi kwa kunipatia nafasi niweze kusema machache kwenye Wizara yetu hii ambayo imebeba Watanzania walio wengi.

Mheshimiwa Spika, mimi nitaomba nizungumzie suala zima la wagani (maafisa mifugo), lakini pili migogoro na tatu ni ushuru kwenye minada yetu na ntagusia kidogo suala zima la nyavu haramu.

Mheshimiwa Spika, wafugaji wetu wengi walioko vijijini wana changamoto kubwa sana ya wagani ama maafisa mifugo. Kwanza maafisa mifugo hawajitoshelezi, lakini pili hao waliopo hawafanyi kazi ipasavyo kwa mujibu wa maadili yao ya kazi. Leo afisa ugani aliyeko kijijini yeye amekuwa ni mchuuzi. Analipwa mshahara na Serikali lakini bado anapohitajika kwenda kutimiza wajibu na majukumu yake mtu huyu ukimfuata atakwambia kwanzasina usafiri, hilo ni kweli hawana usafiri, lakini pili, akienda kufanya hiyo kazi atakwambia sasa unanipa shilingi ngapi; mtumishi huyu analipwa na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hawa watu, maafisa ugani waliopo tunaomba Wizara iweze kuwafuatilia mmoja baada ya mwingine kwa sababu wamekuwa ni kero na changamoto inayosababisha wakulima ama wafugaji wetu kuacha kuwatumia kutokana na biashara yao ya kutoa huduma, badala ya kutoa huduma kwa jamii, wanalipwa mishahara na kodi hizohizo za Watanzania, wanaacha kufanya hiyo kazi wanataka walipwe fedha nyingine ili waweze kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maafisa ugani hawa bado wana shida ya vitendeakazi. Afisa ugani huyu uliyempeleka kwenye kata pale ana vijiji vitatu ama vinne; kutoka makao makuu ya kata mpaka kwenda Kijiji A unaweza ukakuta kuna kilometa 20 mpaka 30; vijiji vyetu hata vya Mkoa wa Dodoma unavijua jinsi vilivyo; mtu huyu hana usafiri, hana pikipiki wala baiskele. Hivi Serikali hii ya uchumi wa kati, Serikali ya viwanda tunaifikiaje hiyo ndoto bila kuwaboreshea maisha vitendeakazi vya hawa maafisa ugani wetu ili waweze kufikisha huduma kwa wakulima wetu?

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie suala la migogoro ya ardhi; limesemwa na Wabunge wengi lakini suala hili ni kama vile limetulia kidogo, limepoa, lakini linafanyika chini kwa chini, kuna mambo yanayoendelea huko huwezi kuamini. Naibu Waziri alifika Wilaya ya Chemba na Wilaya ya Kondoa, kwenye Pori la Swagaswaga pamoja na Mkungunero. Kuna watu walikamatiwa ng’ombe wao wakiwa wanachunga, si kwenye hifadhi, ni mpakani na hifadhi, wale watu wa hifadhi wakaenda wakawasukumia wale ng’ombe kwenye hifadhi wakawakamata.

Mheshimiwa Spika, walivyowakata wakaenda wakawaambia kila ng’ombe mmoja alipiwe shilingi laki moja. Watu wale wakasema hizo hela kwa sasa hatuna, wakawaambia nendeni mkatafute mrudi. Walivyorudi wakahojiwa kila mfugaji mmoja wewe ulikuwa na ng’ombe wangapi, mfugaji anasema nilikuwa na ng’ombe 200 anaambiwa ng’ombe hawa 200 mara 1000 tujumlishe. Lakini watu hawa walikuwa wakilipa hizo faini, wanapokabidhiwa ng’ombe hawafiki ng’ombe 200, mtu atapewa ng’ombe 150, atapewa ng’ombe 80. Wakiuliza ng’ombe wetu wengine wako wapi wanaambiwa ng’ombe wamepotea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mambo haya yanasononesha, mambo haya yanasikitisha, mambo haya yanahuzunisha na yanatia simanzi sana ndani ya taifa letu la Tanzania. Taifa hili, wakulima hawa, wafugaji hawa, huyu mfugaji anatakiwa alipe ada ya mwanafunzi, anatakiwa ale, anatakiwa afanye mahitaji yake yote kulingana na hawa ng’ombe wake. Umeenda umemchukulia ng’ombe wale, umemlipisha faini, unamtaka nini huyu mfugaji? Tanzania ya wanyonge ipi katika taifa letu leo la Serikali ya Awamu ya Tano? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hatua zinazochukuliwa na Wizara bado hazina dhamira ya dhati ya kwenda kupambana na watu hawa ambao wameendelea kuwadhalilisha Watanzania walio wengi katika taifa hili ambao ndio walipa kodi na wao ndio wanalipwa mishahara na haohao walipakodi wanaowanyanyasa. Naomba watu wale ambao ng’ombe wao hawakurudishwa, Mheshimiwa Waziri ukija naomba uniambie watu wa Mkungunero na Swagaswaga waliokuwa wamekamatiwa ng’ombe wao, hawakurudi, naomba uniambie watu wale mnawachukulia hatua gani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Kuhusu Suala Zima la Ushuru wa Minada. Tunafahamu minada haipo kwenye vijiji vyote wala kwenye kata zote, tuna minada ambayo tumeiteua. Lakini ni kwamba katika minada hii, kumekuwa na ushuru wa usafirishaji na kwenda kuuza, mfano mwananchi anayetoka Kijiji cha Mlongia kwenda kuuza ng’ombe Mnada wa Soya, huyu mtu anatakiwa kukata ushuru…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Kuniti, nakushukuru.

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.