Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kupata fursa hii ya kutoa mchango wangu kwenye Wizara hii ya Mifugo na Uvuvi. Mchango wangu utakuwa zaidi kwenye eneo la uvuvi, na hii ni kwa sababu ninatoka Ukerewe; na Ukerewe inaundwa na Visiwa. Katika eneo letu square kilometer 6,400 zaidi ya asilimia 90 ni maji. Katika idadi ya watu tuliyonayo 400,000 na sehemu zaidi ya asilimia 95 wanategemea zaidi uvuvi; kwa hiyo mchango wangu utajikita zaidi kwenye eneo la uvuvi.

Mheshimiwa Spika, uvuvi na mifugo unachangia sehemu kubwa ya Pato la Taifa. Ninaipongeza Serikali kwa jitihada zake za kulinda rasilimali za nchi hii ili ziweze kuwasaidia Watanzania kwa ujumla wake.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na operesheni ambazo zimekuwa zinaendelea kwenye maeneo mbalimbali kwenye uvuvi na mifugo; lakini kwenye eneo la uvuvi operesheni hizi zimekuwa na madhara. Binafsi nimekuwa muumini mkubwa sana wa uvuvi endelevu na nimekuwa ninaunga mkono operesheni hizi kwa dhamira ya kulinda rasilimali zetu; lakini madhara kadhaa ambayo yamekuwa yanasababishwa na operesheni hizi nimekuwa siku zote sikubaliane nazo.

Mheshimiwa Spika, tunafanya mambo haya, tunatengeneza sera, tunatunga sheria, tunafanya operesheni hizi ili kulinda rasilimali lakini wakati huohuo tukihakikisha kwamba maisha ya wananchi wetu kule chini hayaathiriki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa zimefanyika operesheni hizi, bahati mbaya sana hapo nyuma tulikuwa na dada mmoja ametajwa jana anaitwa dada Judith, alitusababishia madhara makubwa sana kwenye eneo la Ukerewe, amepelekwa Kigoma kule. Sasa operesheni hizi niombe sana Wizara, kwa mfano kule Ukerewe kwenye Jimbo langu wananchi wengi wameathirika na operesheni hizi. Wamedhulumiwa, wamenyanyaswa, wamechomewa nyavu zao.

Mheshimiwa Spika, lakini tatizo kubwa linalonisumbua mimi, tunafanya operesheni hizi lakini mbadala wake ni upi? Kwa sababu tukumbuke sehemu Kama Kanda ya Ziwa specifically kwa Ukerewe zaidi ya asilimia 95 ya vijana wameajiriwa na kujiajiri kupitia uvuvi. Kwa hiyo unapovuruga mfumo wote wa uvuvi automatically unaathiri maisha yao lakini unaathiri vilevile maisha ya ujumla ya kiuchumi ya Visiwa vya Ukerewe kwa sababu kila kitu kiuchumi kinategemea shughuli za uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nimeona kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri kuna marekebisho ya sheria kwa mfano kwenye nyavu zitakazotumika kuvua dagaa. Nimewahi kusema hapa dagaa hawavuliwi kwa kunyoosha wavu kwamba wale dagaa wanase kwenye wavu ndio uwakusanye hapana, dagaa wanavuliwa maji marefu tena kwa kuchotwa, sasa kule tulikuwa tunatumia nyavu za milimita sita, wameleta milimita nane mpaka milimita kumi inakuwa ni hasara kubwa sana kwa wavuvi wetu wanaoafanya shughuli za uvuvi hususani uvuvi wa dagaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nashauri; la kwanza, badala ya kuweka vikwazo kwenye uvuvi huu kwa ku-limit saizi za nyavu jambo ambalo linaathiri sana wavuvi wetu, kwa sababu mvuvi tuchukulie gharama anazoingia kwenda kuvua ni kubwa sana, halafu tuchukulie anatumia mafuta ya taa, anatumia petroli bado kuajiri wale watumishi anatumia zaidi ya shilingi 300,000 au shilingi 400,000 kwa siku halafu kwa kutumia nyavu za milimita kumi anapata dagaa sijui thamani yake shilingi 30,000 au shilingi 40,000 bado kuna kodi nyingi anapaswa alipe tunakuwa hatuwatendei haki wananchi hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo badala ya ku-limit saizi za nyavu, nishauri Wizara iangalie uwezekano wa kufanya uvuvi wa msimu, kwamba kuanzia mwezi fulani mpaka mwezi fulani kusifanyike uvuvi, baadaye mwezi fulani na kuendelea uvuvi ufanyike. Mbaya zaidi tunaweka limitation hizi kwenye maeneo yetu, wenzetu majirani zetu Kenya, Uganda wanaendelea na shughuli za uvuvi, samaki hawako eneo moja, tunapowazuia hapa leo wanahama wanaenda Kenya, wanaenda Uganda na Congo wenzetu kule wanawavua wale samaki. Kwa hiyo tunawasababishia umasikini wananchi wetu kwa faida ya majirani zetu, kwa hiyo ni muhimu sana Wizara iliangalie hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukiachilia mbali eneo hili la uvuvi wa dagaa sijui na vitu gani, tumeweka saizi za nyavu, tukumbuke kuna species nyingi sana za samaki ziwani, kuna samaki wengine ambao ukiweka wavu wa milimita tatu, kuna samaki wengine wadogo ambao hawakui kufikia kiwango hicho, sijui mmefanya research kwa kiwango gani. Tukumbuke ecological disaster kwenye Ziwa Victoria imesababishwa na upandikizaji wa sangara kwenye ziwa lile. Kwa hiyo katika species zilizokuwepo zaidi ya 500 nyingi zimepungua kwa sababu samaki wengi wanatumika kama chakula na wanaliwa na sangara. Sasa tunawalinda sangara, hawa samaki wengine tunatumia mfumo gani kuwalinda, matokeo yake tunawaadhibu wananchi kwamba wasivue samaki wale kwa sababu tu kwamba wanapungua kitu ambacho wanaliwa na sangara, sasa hatuwatendei haki wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kule Ukerewe kila wakati wananisumbua wananipigia simu bwana tunazuiliwa kuvua ngere kwa sheria ipi, kwa utaratibu upi? Tunazuiliwa kuvua furu kwa utaratibu huu, kwa sheria ipi? Kwa hiyo niombe Wizara itoe tamko la kuruhusu uvuvi wa ngere na furu, kwa sababu kupungua kwao ni kwa sababu wanaliwa na sangara. Ningu kwa mfano tunavua kwa nyavu zipi? Kwa hiyo niombe Wizara iliangalie jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakati wa operesheni hizi kama nilivyosema awali, wananchi wengi sana walinyang’anywa mali zao, wamenyang’anywa mashine, nyavu zimechomwa, mitumbwi imeharibiwa mpaka leo mashine zile za wavuvi ambao wamehangaika kweli kwa jasho na damu kupata mashine zile zimeshikiliwa kwenye vituo mbalimbali. Niombe Mheshimiwa Waziri atoe tamko wananchi wetu vifaa vyao vile waweze kupewa ili waendelee na shughuli zao za uzalishaji mali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunafanya yote haya lengo ni kulinda rasilimali, lakini tuimarishe uchumi wa wananchi wetu. Tunaweza kuimarisha uchumi wa wananchi wetu tunapochoma nyavu, tunawapa njia mbadala, tumekuwa tuna- encourage uvuvi wa vizimba, je, tunapata faini, tunakusanya mapato, tunarudishaje pesa hizi kuweza kuelimisha vijana wetu kujifunza namna ya uvuvi wa vizimba? Bahati mbaya uvuvi huu wa vizimba ukianza kufuatilia kwa mfano ukitaka kuweka vizimba vyako kuna taratibu nyingi mno, kuna tozo nyingi mno zaidi ya sita, saba, sasa kwa mtu wa kawaida kuvuka vikwazo vyote hivi ni ngumu sana na gharama ni kubwa.

Mheshimiwa Spika, leo hii kwa mfano nikiuliza kwa Mheshimiwa Waziri hapa leo wanipe kama wana database wanipe orodha ya maeneo ambayo yana sifa za kuweka vizimba kwenye maeneo mbalimbali. Kwa mfano, waniambie kwamba Ukerewe ni eneo lipi ambalo wameainisha, wamefanya research, wakaona kwamba eneo moja, mbili, tatu yanafaa kwa ajili ya uvuvi. Kwa hiyo, mtu anapotaka kufanya uvuvi huu anaanza kuhangaika hatua moja baada ya nyingine, vikwazo vingi hatimaye sasa hata ile dhamira yake inakuwa imepungua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niombe sana kama nilivyoshauri mambo matatu ambayo ni muhimu sana. La kwanza, Mheshimiwa Waziri kama nilivyosema aruhusu, atoe tamko, vifaa vilivyokamatwa vya wavuvi warudishiwe ili waendelee na shughuli zao, lakini watoe tamko la…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Joseph.

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)