Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Tunza Issa Malapo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naskushukuru. Awali ya yote napenda kuipongeza Hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, ina mambo mengi mazuri, Serikali itulie isome na ifanyie kazi ushauri ambao wameutoa. Pia ukiangalia kwenye kitabu cha Kamati nacho pia kina mambo mazuri, kina ushauri nzuri, pia Serikali itulie isome ifanyie kazi kwa maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi natokea Mtwara, Mtwara kuna Bahali ya Hindi. Ukifika Mtwara Mjini sasa hivi samaki wengi ambao tunakula wanatoka Msumbiji. Wanatoka Msumbiji si kwa sababu sisi watu wa Mtwara hatuna bahari ama hatuwezi kuvua ni kwa sababu vyombo vya uvuvi vilivyopo ni duni. Wavuvi wengi wanatumia mitumbwi kwa makasia hivyo wanashindwa kuvua samaki kwenye kina kirefu. Pia ukienda upande wa Msumbiji nyavu zilezile ambazo Tanzania kwa kiasi kikubwa zinachomwa kule zinatumika na samaki hao wanarudishwa wanakuja kwetu kuuzwa na sisi tunanunua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tuna bahari kubwa ambayo tulitarajia kitoweo cha samaki kiwe ni chakula kikuu, lakini sasa hivi Mtwara kula samaki ni anasa, kwa sababu samaki utaambiwa wanauza shilingi 2000 au shilingi 3000 ni samaki mdogo lakini bahari tunaiangalia. Sasa ushauri wangu kwa Serikali nawaomba waone haja ya makusudi kabisa ya kuwekeza, tukipigwa kwenye korosho basi tukimbilie kwenye uvuvi. Korosho hali tete kwenye uvuvi hali tete mambo yanakuwa tafrani haipendezi, tunashindwa hata pamoja pa kujishikia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukifungua katika ukurasa wa 41 wa hiki kitabu cha Kamati unaona wameeleza kuna uvuvi wa samaki aina ya Jodari, wanasema asilimia 67 ya samaki waliouzwa huko nje duniani mwaka 2018 wamevuliwa kutoka ukanda wa bahari kuu ya Tanzania na watu wengine sio sisi Watanzania. Pia ukisoma pale kwenye ukurasa wa 41 Kamati imetoa ushauri ndio maana nikasema, Serikali ijitahidi kusoma hiki kitabu ili wapate ushauri, wamesema kuwa na ujenzi wa viwanda vya kuchakata samaki aina ya jodari kwenye ukanda wa Pwani wa Bahari ya Hindi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiangalia masuala ya viwanda naona kwa asilimia kubwa amelekezwa kwenye maeneo ambayo kuna Ziwa, maeneo ya Ukanda wa Ziwa Victoria, lakini ukija huku kwenye ukanda wa bahari sijajua kama kuna kiwanda chochote, kule kwetu Mtwara najua hakuna kiwanda cha uchakataji wa samaki, lakini tuna bahari ule ukanda wote ule kutoka Mtwara, Kilwa huko mpaka unakuja Dar es Salaam, sijakiona kiwanda cha kuchakata mazao yanayotokana na samaki wa maji chumvi. Ndio mpaka sasa hivi ukipita humu madukani kwenye mabucha ya samaki, samaki wa maji baridi ni wengi kuliko samaki wa maji chumvi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakatoa ushauri mwingine, (b) ununuzi wa meli za kufanya uvuvi katika bahari kuu ya eneo la Tanzania, hakuna meli kubwa za uvuvi, hawa samaki kama jodari ndugu yangu huwezi kuwavua kwa kutumia mitumbwi ile ya kwetu ya asili huwezi. Kwa hiyo, ni lazima wawekeze haya mambo mengine ya kukimbilia vitambulisho, mtu mama anauza mboga unamng’ang’aniza atoe kodi uchumi tunauacha kwenye bahari kuu. Pesa tunaziacha huku, ndio maana kila siku tunataka tuwafinye watu wenye biashara ndogo ndogo lakini huku zinapokuja kupatikana pesa nyingi hatuwekezi ili kusudi tuongeze pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatakiwa tuwe serious, kuna mambo mengine yangekuwa yanafanyika for free, watu wanafanya biashara za mboga mtu ana mchicha wake, lakini wewe mtu wa uvuvi unachotegemea mtu afanye kosa ukamtoze faini, ndio uje hapa maduhuli yameongezeka, maduhuli yameongezeka, lakini ukiangalia mengi ni faini, hatuwekezi vya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukurasa huo wa 41, Kamati ikashauri ujenzi wa maeneo ya kuhifadhia samaki na mazao yake, hakuna ya kutosha. Kwa hiyo niwashauri wasome vizuri, hatuna bandari za uhakika za uvuvi, watu wanauza tu holela holela, mtu akienda na hicho kimtumbwi chake, akivua visamaki viwili, vitatu, anakuja anauza, matozo kibao matokeo yake maendeleo ya wavuvi wetu yanakuwa kila siku ni duni yaani mtu ili apate tu kitu cha kula kwa siku ambapo hii ingekuwa ni sekta iliyoendelezwa nafikiri ingesaidia Watanzania na pia ingeongeza pato la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee kidogo kuhusu ufugaji wa kuku wa nyama na mayai. Ukiangalia kwa kiasi kikubwa hii mifugo inawasaidia wajasiriamali wadogo ambao wengi wao ni wanawake ambao mimi nawawakilisha hao wanawake, tumekuwa na tatizo kubwa sana la upatikanaji wa vifaranga, lakini pia hata hao vifaranga wakipatikana kuna changamoto kubwa sana ya masoko, hakuna masoko ya uhakika. Mtu anafuga kuku mpaka wanafikia stage ya kuuza hapati soko kuku wanakaa wiki mbili wiki tatu zaidi matokeo yake anaamua kuuza kwa bei ya hasara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri kama Wizara waangalie kwa undani nimekuwa na interest kidogo na sehemu hii, waangalie kwa undani na kufuatilia tatizo hasa ni nini, watoe ushauri kwa wafugaji hawa wadogo ili waweze kujiongezea kipato, kwa sababu kama mtu anafuga kuku thamani yake shilingi 5,000 halafu anakuja kuuza kwa shilingi 4,000 anapata hasara, wategemezi wanazidi kuongezeka, Taifa halipati kipato, lakini hizi sekta zikiangaliwa kwa undani kama kuna changamoto wawaaambie watu, kama kuna kuku wanaongia kutoka nje wafanye utaratibu mzuri, kama kuna mayai yanayoingia kutoka nje ili kusudi ili soko litengamae, watu waweze kuuza na kufuga kwa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushuru. (Makofi)