Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia kwenye hoja hii ya Wizara ya Mifugo. Nitangulize pongezi zangu za dhati kwa Mheshimiwa Waziri wa Mifugo, ndugu yangu Mheshimiwa Luhaga Mpina, Naibu wake Mheshimiwa Abdallah Ulega, Makatibu Wakuu, ndugu yangu Profesa Elisante Ole-Gabriel na Dkt. Rashid Adam kwa kazi kubwa wanayofanya kama Wizara katika kuleta mapinduzi ya sekta ya mifugo ambayo kwa miaka mingi imesahauliwa na kuwekwa pembeni kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa mtoto mdogo wakati nilipokuwa nasikia jinsi Wizara ya Mifugo inavyobebwa na Serikali ya awamu ya kwanza. Wakati ule na nimepitia nyaraka zilizopo, kulikuwa na Sheria inayoitwa The Ranch Development and Management Act, ya mwaka 1964.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nyakati hizo nyanda za malisho zilipewa hadhi yake, ziliundwa Commissions, zikagawanya Kanda, zikaanzishwa na kuhamasishwa Jumuiya za Kifugaji na Ranch za Ufugaji, ndiyo wakati ule pia hata katika ukanda mkubwa wa Masai Steppe iliyokuwa Wilaya ya Maasai, ambayo leo ina Wilaya karibu sita ndani yake ikiwemo Longido, Monduli, Simanjiro, Ngorongoro, kukawa kuna Masai Ranch. Ile taasisi ilikuwa imewezesha, ina mitambo ya kuchimba mabwawa, ina magari, inatoa tiba ya chanjo, dips za kuongesha na kwa kweli hata wafugaji wa wakati ule walipoambiwa walipe kodi ya kichwa cha ng’ombe hawakulalamika maana yake wanajua Serikali inawatunzia mifugo na walilipa kwa furaha, kulikuwa na upungufu wa kitu kimoja tu, masoko, lakini Serikali haikujali wanauza wapi ili mradi wanahudumiwa ili uchumi wao uweze kuimarika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipoangalia nyaraka zilizofuatia, kuna hii Sera ya Mifugo ya Mwaka 2006, halafu ikaja na Sheria ya Nyanda za Malisho ya Mwaka 2010. Hizi zote zinasisitiza kabisa na kuweka mkazo kwamba, ili mifugo iwanufaishe wafugaji na kuliletea Taifa mapato makubwa, ni lazima mifugo wapewe maeneo ya malisho, maji, tiba, masoko, sambamba na kuimarisha miundombinu ya barabara na viwanda vya kuchakata nyama na mazao ya mifugo. Hivi vitu vyote vimekuwa ombwe kubwa katika kukuza na kuimarisha sekta ya mifugo, lakini katika hotuba hii, iliyoandaliwa kwa makini na mambo ambayo Waziri amebainisha kwamba anakwenda kufanya, imenijaza matumaini na naamini kwamba akiyasimamia tutaona mapinduzi katika sekta hii ya mifugo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamuomba Waziri basi azingatie katika suala la malisho, hata yale maeneo ambayo hayana migogoro kama Longido. Sisi tuna maeneo lukuki ya malisho lakini yana uhaba mkubwa wa maji; na ninakushukuru kwa sababu kwenye ziara yako ya juzi ulipopita ulitujaza matumaini ukatambua mabwawa yaliyovunjika, mabwawa yaliyojaa udongo na ukasema kwamba utatusaidia kukarabati, yatawekwa kipaumbele katika bajeti hii, sambamba na kutujengea yale mabwawa nane yaliyobomoka ukijua na kutilia maanani kwamba sisi wananchi tumetengeza kwa nguvu zetu kupitia wadau na halmashauri yenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikutajie tu baadhi ya nyanda za malisho ili ujue ni kwa jinsi gani Longido ina maeneo ambayo yakiboreshwa na yakawekezwa tuna maeneo ya kutunza mifugo yatakayokuwa na tija kubwa; na sisi tumeimarisha mifugo kweli kweli kwa ajili ya hivi viwanda ambavyo pia vitajengwa na Longido pia ikiwa ni mnufaikaji wa kiwanda kimoja kitakachochinja ng’ombe 500 kwa siku na mbuzi 2,000. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna nyanda za malisho, sisi tunaita Ngaron, nikutajie tu baadhi. Kuna Loorboro, Oldenja, Engasurai, Naambala, Leleki, Ildonyo-dapashi, Loomunyi, Ngurmausi, Lookinyoyo, Loosikitok, Olesulenge, Kitang’a- engutak, Idonyo-oonyokioo, Ang’ata-eopir, Endonyo- nanyokie, Loolwaa, Ndashat, Orkiloriti, Orpelela, Lekuruki, Kelembusi, Endonyo-emali, Endarakwa, Kitenden, Ndiakakati, Endapitipit, Kesertet, Emesera na Molonjoni. Hizo zote ni nyanda ziko wazi ni maeneo mahususi yanayopata majani kwa haraka, mvua hata wiki moja ikinyesha lakini mara nyingi wakati ule bado hali ya tabianchi haijabadilika ni moto tu na mchwa ndiyo anakula yale majani kwa sababu hakuna maji katika nyanda hizo. Mheshimiwa Waziri tupatie kipaumbele kuweka mabwawa, kuweka visima virefu, mifugo watashamili, mbuzi, ng’ombe, kondoo na hivi viwanda havitatindikiwa malighafi vikapokuwa vimekamiliaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine la mwisho ni kero. Kwa kweli kwa miaka yote hii Tanzania haijawa na soko la uhakika la mifugo na kwa miaka yote hii hatujaona nguvu ya Serikali katika kutusaidia kutunza hii mifugo. Kwa hiyo hii operesheni iliyoanzishwa inayoitwa Zagamba ambayo imezagaa kule kwetu Longido imewaumiza wafugaji na wachuuzi wa mifugo kutoka sehemu mbalimbali ya Tanzania waliokuwa wanatumia mpaka huu wa Kenya kupeleka mifugo Kenya kwenye soko lenye tija. Kwa sababu licha ya kwamba walikuwa wanasimamia Sheria lakini pia kwa kanuni ulizoweka. Kwamba akipatikana mtu anayekwenda kuvusha mifugo au akituhumiwa tu anapigwa faini 500,000, hata kama alikuwa anapeleka mbuzi wawili maskini ya Mungu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwingine bado mifugo haijalipiwa kwenye masoko; nadhani zile tozo zinazojulikana; unakuta yule mtu anawekewa na faini. Kwa mfano kuna watu walikamatwa walikuwa ni watatu wenye ng’ombe kila mtu 500,000, mbuzi 30,000 kwa sababu sasa faini ng’ombe 50,000 halafu bado akifika kule mpakani wanatozwa kodi zingine za kupeleka ng’ombe nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wengi wamefilisika kwa sababu ya operesheni, rushwa pia imetumika na kuna pia msimamizi wa kikosi huko amekuwa na unyama wa hali ya juu. Mimi siwezi kumtaja kwa jina lakini ile operesheni Mheshimiwa Naibu Waziri alipokuja tulikaa tukasema kama wafugaji hatukushirikishwa katika kuweka hizi taratibu. Kama tungelishirikishwa tungeulizwa mnaenda kupata faida kiasi gani mkipeleka mifugo Kenya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakasema kama tungelitozwa hata hizo kodi, kwa mfano kodi ya kupeleka ng’ombe Kenya ni 30,000 ya kupeleka mbuzi ni 7,500, ukiweka na kodi za halmashauri inafika 9,000 na sasa hivi ukiwaambia wafugaji wanawenda kupata faida kiasi gani hawapati. Wakaililia kabisa Serikali wakasema ng’ombe awe 15, 000, mbuzi awe 4,500, wao wenyewe wapewe kazi ya kusimia operesheni ya wanaotaka kutosha mifugo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanatoroshwa kwa sababu hawapati faida tena wakilipa hizo tozo; na mbaya zaidi ni hizo faini ambazo zina wafilisi wengi. Mheshimiwa Waziri nakuomba, kwa sababu hizo ziko ndani ya kanuni, ukiacha Sheria ambayo naomba pia Bunge hili tubadilishe, tuweke kodi zinazoendana zipunguzwe mpaka pale Serikari itakapokuwa imetuwekea masoko ya uhakika na viwanda ndipo sasa wafugaji wetu waweze kuwekewa faini kubwa wakitaka ng’ombe Kenya kwa sababu hawa sababu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamwomba Mheshimiwa Waziri abadilishe hizo kanuni zake. Haiwezekani mtu anayekamatwa akipeleka mbuzi watatu alipe 500,000 halafu mtakuwa mmemfilisi hata hao mbuzi wenyewe hawafiki 300,000 wakiwauza laki moja moja…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri usipofanya hilo mimi niko tayari kushika shilingi kwa sababu kwa kweli tuna kero kubwa ya watu ambao wamefilisika kwa sababu ya kanuni ulizotunga ambazo zimekuwa kandamizi na za kuumiza wafugaji wetu wanaotafuta riziki kwa sababu hapa nchini kwetu bado hatuna masoko ya uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa hii.