Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. OMARY T. MGUMBA): Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyetupa afya na uzima tumeipata nafasi hii ya kuchangia katika sekta hii muhimu kwa Watanzania, sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Spika, pia natoa shukrani zangu za dhati kwa Mwenyezi Mungu na nichukue fursa hii kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa John Pombe Joseph Magufuli, kwa kuniamini na kuniteua kuwa Naibu Waziri wa Kilimo katika kumsaidia katika majukumu kwenye sekta hii ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, natoa pia shukrani za pekee kwa Waziri wa Kilimo Mheshimiwa Japhet Hasunga (Mb) kwa ushirikiano mkubwa anaonipa katika kutekeleza majukumu yangu. Vile vile ninamshukuru Mheshimiwa Innocent Bashungwa, Naibu Waziri mwenzangu kwa ushirikiano mkubwa anaonipa katika kuwatumikia Watanzania; tunafanya kazi hii kwa pamoja kama timu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niishukuru Kamati ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji, Kambi Rasmi ya Upinzani pamoja na Waheshimiwa Wabunge wote kwa michango yao. Aidha, nawashukuru wapiga kura wangu kwa kuendelea kuniamini na kunipa ushirikiano wa kutosha pale ambapo ninapokuwa katika Bunge hili na sehemu zingine kuwawakilisha. Nipo hapa kwa sababu yao, niko hapa ndiyo sauti yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nachukua nafasi hii kukishukuru chama changu Chama Cha Mapinduzi kwa ushirikiano mkubwa kinachonipa katika kutekeleza majukumu haya hasahasa kusimamia Ilani ya Chama Cha Mapinduzi kwenye Sekta hiyo ya Kilimo. Aidha, namshukuru Katibu Mkuu na Naibu Katibu Mkuu pamoja na watendaji wa Wizara ya Kilimo na taasisi zilizokuwa chini ya Wizara kwa kazi nzuri wanayofanya na ushirikiano wanaonipa katika kutimiza majukumu yangu.

Mheshimiwa Spika, baada ya shukrani hizo, ninaomba sasa nichangie hotuba yangu ya Mheshimiwa Waziri wa Kilimo kwa kutoa maelezo na ufafanuzi wa hoja mbalimbali zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge katika sehemu kuu mbili ambazo ni umwagiliaji na zao la kahawa na kama nitapata muda nitaenda kwenye miwa pia na mbegu za mafuta kwenye mafuta ya kula.

Mheshimiwa Spika, kabla ya kuanza na hoja hizo mbili, sisi kama Serikali niishukuru sana michango ya Wabunge. Wengi wamezungumzia kuhusu bajeti kwamba bajeti ya sekta ya kilimo ni ndogo. Pamoja na ukweli huo wengi wana- refer azimio la Malabo na lile la Maputo. Ni kweli lakini tuna maazimio mengi ambayo tumeingia kama nchi. Tutoe mfano tu, afya tunatakiwa tutenge asilimia 15, elimu asilimia 20, kilimo asilimia 10, tuna asilimia 45 kwa mambo matatu tu; lakini ukiangalia vipaumbele tulivyokuwa navyo viko vingi. Kwa hiyo hii bajeti kwa mazingira tuliyonayo na hasa uchumi wetu ni vizuri kwamba tukazingatia badala ya kujielekeza kwenye maazimio ambayo hayaendani na hali halisi ya uchumi wetu.

Mheshimiwa Spika, pia bajeti hii ya sekta ya kilimo tunaitekeleza kwa kupitia mpango wetu wa ASDP II. Kama tulivyoeleza bajeti hii kwenye ASDP II asilimia 40 ndiyo Serikali na asilimia 60 itatekelezwa na sekta binafsi. Kwa hiyo sekta binafsi nayo ina mchango mkubwa sana katika kuendeleza kilimo katika nchi hii.

Mheshimiwa Spika, kilimo ni kipana, ni kilimo mazao, kilimo mifugo, kilimo mifugo, kilimo uvuvi, na kilimo misitu, Kwa hiyo bajeti yake huwezi kuiona tu kwenye Wizara hii moja ya Kilimo, utaiona kwenye Wizara zote hizo zingine pamoja na Wizara zile za Kisekta. Kama mnavyokumbuka bajeti hii ni mwendelezo wa mipango wa Serikali tangu mpango ule wa mwanzo.

Mheshimiwa Spika, tulikubaliana kama Serikali, mpango wa mwanza ulikuwa kwanza kuondoa vikwazo vya kimaendeleo na ndiyo maana sasa hivi bado Serikali tunaendelea kuondoa vikwazo vya kimaendeleo ili kumkwamua mkulima; ndiyo maana tunaboresha hiyo miundombinu ya barabara, reli, pamoja na ndege, yote ni ili kuwezesha mazao ya wakulima ili yaweze kufika kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, Hoja Mahsusi Kuhusu Mambo ya Umwagiliaji. Kulikuwa na hoja kutoka kwenye Kamati yetu ya Kilimo lakini pia Kambi Rasmi ya upinzani na pia katika michango ya Wabunge mbalimbali. Ni kweli eneo la umwagiliaji kama nchi bado ni dogo sana ambalo eneo linalofaa kwa umwagiliai tuna hekta zaidi ya milioni 29 lakini mpaka sasa tumeendeleza hekta 475,000.

Mheshimiwa Spika, Serikali imejipanga ndani ya miaka 10 tuweze kuongeza eneo la uzalishaji kutoka hekta 475,000 mpaka hekta 1,000,000. Kama nilivyosema awali hiyo sisi kama Serikali pamoja na kushirikiana na Sekta Binafsi pia na Serikali za Halmashauri na kupitia Benki yetu ya Maendeleo ya Kilimo na Benki nyingine kwa sababu tukisema kwamba tunategemea hela za kibajeti, maeneo haya ya umwagiliaji yote hatutaweza.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Benki yetu ya Maendeleo ya Kilimo na Benki nyingine za kibiashara kama CRDB, NMB, Azania, Benki ya Posta na zingine zote, hizi sasa tumesema kwamba kwa sababu tunaenda kwenye kilimo cha biashara, zinakwenda kwa maelekezo ya Serikali na mipango hiyo kwamba Serikali tunakwenda kudhamini asilimia 50 ya fedha zote zilizotolewa na benki hizi za biashara ili kwenda kuendeleza miundombinu ya umwagiliaji katika nchi hii badala ya miradi yote ya umwagiliaji kusubiri pesa za kibajeti kwa udhamini wa Serikali kwa kushirikiana na Serikali za Halmashauri za Wilaya pamoja na Tume ya Taifa ya Umwagiliaji ambao wao watahusika kwa ajili ya kutoa utaalam kwa ajili ya ramani na kusimamia ujenzi ili halmashauri hizi na miradi hii tuweze kuchukua mikopo ya masharti nafuu kuiendeleza miradi hiyo ili tuwe na kilimo cha uhakika cha umwagiliaji katika nchi hii.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tutakuwa kweli na miradi itategemea fedha za kibajeti lakini pia tutakuwa na miradi ya kibiashara ambayo itapata fedha kutoka kwenye taasisi zetu hizi za fedha kwenye benki hizo ambazo nimeziainisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na mkopo huu utalipwa ndani ya miaka mitano mpaka miaka 15; na mingine iwe ni fursa kwa wafanyabiashara wakubwa kuchukua ardhi kwenda kuwekeza miundombinu ya umwagiliaji, baadaye tutaweza kuwakodisha kwa wakulima na wanufaika wengine utaweza kulipa tarayibu mpaka pale ambapo pesa itakaporudi. Mpango huu tunauweka katika ile mpango wetu wa kwamba jenga, endesha, baadaye unakabidhi baada ya malipo ya ujenzi ule kurudi.

Mheshimiwa Spika, la pili kwenye umwagiliaji, tumeona baada ya Wizara hii kuja kwetu cha kwanza ambacho kama Serikali tulichokifanya kwa pamoja ni kuielekeza mhasibu (CAG) kufanya ukaguzi maalum kwenye miradi yote ya umwagiliaji nchini.

Mheshimiwa Spika, na nikiri, baada ya taarifa hiyo ambayo tulishai-table hapa kwenye Bunge lako Tukufu, tutaijadili vikao vijavyo baada ya Bunge la Bajeti ambapo tumeona madhaifu mengi sana katika miradi hii; na ndiyo maana sehemu nyingine miradi kwamba imemalizika, maji haitoi au miradi imejengwa chini ya kiwango. Yote hayo sisi kama Serikali tumeyapokea na tumeshaanza kuyafanyia kazi hata kabla hatujaanza mjadala hapa Bungeni.

Mheshimiwa Spika, cha kwanza, tumeunda timu maalum ya kiuchunguzi kwenda kuyathibitisha yale ambayo aliyoyagundua CAG kwa mujibu wa sheria ili sasa wale wote ambao waliotufikisha hapo kwanza tuwachukulie hatua lakini kubwa zaidi ni kujifunza wapi tulifanya vibaya ili kuja na mikakati ya kuweza ku-address tatizo lililokuwepo na kwenda kuwa na kilimo cha uhakika cha umwagiliaji.

Mheshimiwa Spika, pia, katika suala la umwagiliaji sasa tunataka kufanya mapitio ya kimuundo. Badala ya Tume ya Taifa ya Umwagiliaji kuwa tu kwenye kanda, sasa tunataka tuishushe mpaka kwenye ngazi ya kata, vijiji mpaa ngazi ya halmashauri. Kwa hiyo tutakuwa na wataalam Makao Makuu kwenye Tume ya Taifa ya Umwagiliaji lakini pia tutakuwa na wataalam wa umwagiliaji kwenye kanda, tutakuwa na wataalam wawili kwenye mkoa na baadaye tutakuwa na wataalam wengine kwenye wilaya. Baadaye tutawajumuisha pamoja na wale wa halmashauri ili miradi hii isimamiwe maalum. Kila mradi ambao utasimamiwa, utakuwa na Meneja maalum au Mhandisi maalum wa kuusimamia mradi huo, badala ya sasa miradi mingi ilikuwa inasimamiwa na Engineers wa Kanda ambao wanaishi Makao Makuu Dar es Salaam, kitu ambacho kimechangia miradi mingi kujengwa chini ya kiwango.

Mheshimiwa Spika, pia kulikuwa na hoja za Wabunge mbalimbali, ambao wamezitoa. Kwa mfano, Mheshimiwa Deo Ngalawa, alikuwa anazungumzia mkakati wa kuendeleza kilimo cha umwagiliaji badala ya kutegemea mvua. Ni kweli, hoja yake ni ya msingi, lakini katika kilimo hiki cha umwagiliaji kama nilivyosema katika maelezo yangu, kwa sababu kilimo tunategemea mvua, tunategemea maji ya ardhini kwa kuchimba visima, lakini pia kwa ajili ya kuvuna maji kwa ajili ya ujenzi wa mabwawa. Sisi kama Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji ili kuwawezesha wakulima hawa wadogowadogo, mpaka sasa tuliagiza mitambo ya kuchimba na kutengeneza miundombinu ya umwagiliaji na mitambo hiyo imeshafika na imeshafika hapa Dodoma. Lengo kwa wale wandarasi wa ndani wadogo wanaopewa, ambao uwezo wao wa vifaa ni mdogo, watakodisha kwa bei nafuu mitambo hii ili kurahisisha ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji katika maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vile vile kulikuwa na Mheshimiwa Neema Mgaya, alikuwa anasema kwamba Serikali iwekeze kwenye malambo, mabwawa ili kuongeza uzalishaji. Kama nilivyosema katika maelezo yangu kupitia mapitio ya mpangi kabambe, ambao tayari tulishauhaulisha, mpango wa umwagiliaji, yote lengo ni kwenda kujibu hoja za wananchi.

Mheshimiwa Spika, hoja ya pili, ni suala la kahawa, ni kweli, kwenye suala la kahawa, kama walivyosema Wabunge wengi na Kamati yetu ya Kilimo, walikuwa wanataka kujua mkakati wa Serikali wa kuhakikisha upatikanaji wa uhakika wa soko la kahawa. Kwanza, tulichofanya katika msimu huu unaokuja, cha kwanza tumeyatambua makampuni yote ya ndani ambayo yananunua kahawa zetu kwa ajili ya kuwapa vibali Vyama vyote vya Ushirika na wakulima na makampuni yanayonunua hapa kahawa, kuuza moja kwa moja bila kupitia mnadani. Hilo limeonesha mafanikio makubwa zaidi, kahawa zaidi ya asilimia 80 tunavyoongea, tayari zilishakuwa kwenye makubaliano ya kuweza kuuzwa moja kwa moja kwa wale wanunuzi wa kahawa wa uhakika ambao wanakwenda kuuza nje.

Mheshimiwa Spika, la pili, tuliona kwamba ni busara, kwa sababu kahawa ni zao la muda mrefu, tunawahimiza wakulima wetu walime kahawa, lakini hii fursa inaangaliwa na nchi mbalimbali duniani. Wanavyoona bei ya kahawa inavyopanda au bei ya mazao mengine, nao wanaangalia. Cha pili, tumeona kwamba ni vizuri kuingia makubaliano maalum na nchi zile za walaji katika nchi mbalimbali ili tuwe na soko la uhakika. Kahawa hii tunawahimiza wakulima walie, tunakwenda kuiuza kwa nani, kwa bei gani na kipindi gani ili tupate mikataba ya muda mrefu kati ya miaka mitano mpaka 20 ili tusije kuzalisha kahawa kwa wingi, baadaye inafika kule muda unakuwa umekwisha. (Makofi)

Watu wengi hapa walikuwa wanajiuliza kwa nini Kenya ni kubwa na Uganda…

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Naibu…

NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie dakika moja tu.

SPIKA: Ahsante, malizia dakika moja.

NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. OMARY T. MGUMBA): …wanasema kwa nini Kenya bei ni kubwa na Uganda, sababu ni hiyo, wenzetu walishakuwa na bilateral sisi tulikuwa bado, ndiyo maana kwamba wenzetu walikuwa wanapata mikataba mizuri kabla ya sisi na sisi sasa tumeamua tunafanya hivyo ili kuboresha bei ya mazao yetu nchi.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii na naunga mkono hoja. (Makofi)