Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

Hon. Willy Qulwi Qambalo

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Karatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Spika, kilimo kinaajiri zaidi ya asilimia 75 ya Watanzania na hivyo ni vyema sekta hii ambayo ndiyo imeajiri watu wengi wa hali ya chini iangaliwe kwa umuhimu mkubwa na ipelekewe fedha za kutosha. Upelekaji wa fedha kwenye Wizara hii bado uko chini sana.

Mheshimiwa Spika, kama nchi tunatakiwa kujitafakari juu ya hali isiyotia matumaini ya baadhi ya mazao nchini. Wakulima wa katani/mkonge wamekata tamaa, kahawa nao wamekata tamaa, alizeti, mbaazi, mahindi, hali ni mbaya, korosho ndiyo hiyo inayoyoma.

Mheshimiwa Spika, ni vyema tujiulize tumekosea wapi? Hivi mkulima wa Tanzania alime nini ili apate kunufaika?

Mheshimiwa Spika, mahindi ni zao linalolimwa kama chakula na biashara. Mbegu bora ya mahindi inauzwa ghali sana na hivyo kufanya wakulima wengi kushindwa kuzipanda. Serikali iangalie namna bora ya kuwapatia wakulima mbegu bora. Huko nyuma tulikuwa na mashamba ya kuzalisha mbegu kupitia kampuni ya TANSEED ambayo yalizalisha mbegu tena katika mazingira ya kwetu. Mbegu kwa sasa nyingi zinatoka nje na ndiyo maana zinauzwa ghali.

Mheshimiwa Spika, zao la mbaazi nalo lina hali mbaya sana. Mwaka jana zao hili lilipoteza thamani na halikuuzika mwanzoni na baadaye liliuzwa kwa bei ndogo sana. Serikali iwatafutie masoko ya mbaazi.

Mheshimiwa Spika, kama kweli kilimo kinathaminiwa Serikali iwaajiri maafisa wengi wa ugani ili wakulima wapate mafunzo na ushauri wa kitaalam kwa karibu sana.