Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

Hon. Eng. Edwin Amandus Ngonyani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Namtumbo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

MHE. ENG. EDWIN A. NGONYANI: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja. Nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa pumzi. Aidha, nimshukuru Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kazi kubwa iliyofanyika katika kufufua zao la tumbaku Wilayani Namtumbo, pamoja na kutuletea soko la Stakabadhi Ghalani kwa mazao ya ufuta, soya, alizeti na dengu. Nimpongeze pia Mheshimiwa Rais kwa kumwona mchapa kazi, Waziri Mheshimiwa Japhet Hasunga na kumkabidhi Wizara hii ngumu ya Kilimo na Umwagiliaji. Yeye ni msikivu bila kujali aina ya hoja anazoletewa, anatusikiliza kwa unyenyekevu, ahsante sana.

Hata hivyo, kama mwakilishi wa wananchi wa Wilaya ya Namtumbo ambayo wakazi wake ni wakulima wadogo wasio na kipato cha uhakika, naomba aendelee kupokea hoja zifuatazo na kuzifanyia kazi:-

Mheshimiwa Spika, kwanza, Benki ya Kilimo iwahudumie wakulima. Itoe mikopo kwa wakulima wadogo kupitia Vyama vyao vya Ushirika kama vile AMCOs zinazounda Chama Kikuu cha SONAMCU. SONAMCU inalazimika kukopa kwenye benki za kibiashara kwa ajili ya pembejeo na hivyo kutozwa riba kubwa inayomwongezea mkulima mdogo umaskini.

Mheshimiwa Spika, pili, Mfuko wa Pembejeo nao uwahudumie wakulima wadogo. Changamoto kubwa ya wakulima wadogo ni upatikanaji wa mbegu bora na mbolea. Pembejeo sio matrekta tu, tukopeshwe vile vile kwenye upatikanaji wa mbegu na mbolea.

Mheshimiwa Spika, tatu, tunampongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa maamuzi ya kijasiri ya kununua korosho baada ya soko la zao hilo kuvurugwa na kutaka kumuumiza mkulima. Kwa Namtumbo, tunayo Tarafa moja ya Sasawala ambayo wakazi wake hutegemea zaidi zao la korosho. Wapo walioanza na kulipwa lakini wapo wakulima 76 waliouza jumla ya tani 104.485 za korosho hawajalipwa kabisa hadi hivi leo. Nimwombe Mheshimiwa Waziri ahakikishe wakulima hao wanalipwa haraka ili wapate nguvu ya kuendelea na kilimo cha korosho cha msimu mpya ambao umeshaanza na palizi na upuliziaji wa sulphur.

Mheshimiwa Spika, nne, kuna vikwazo vingi vinavyoathiri soko na uzalishaji wa zao la tumbaku na mazao wengine ya kimkakati. Tozo ni nyingi mno na utekelezaji wa kodi ya ongezeko la thamani (VAT) hauko sawa. Marejesho ya kodi hiyo hayafanyiki kwa wakati na hivyo kuathiri mtaji wa kufanyia kazi working capital kwa wanunuzi na wachakataji wa mazao hayo hususan zao la tumbaku. Hebu Mheshimiwa Waziri amshawishi Waziri wa Fedha na Mipango na Wajumbe wa Baraza la Mawaziri waelewe madhara ya kutolipa VAT return kwa wakulima wetu. Soko la mazao hayo litakufa na watakaoathirika ni wakulima wetu maskini.

Mheshimiwa Spika, tano, taasisi za udhibiti katiba sekta ya kilimo ni nyingi mno na zinafanya kazi zinazofanana. Ukienda kwenye tumbaku, sukari, korosho, chai ama pamba hali ya utitiri wa tozo inafanana. Viwango vya tozo za taasisi za udhibiti ni vikubwa mno, vinaongeza gharama za uzalishaji na kuzifanya bidhaa zetu zishindwe kushindana kwenye soko huria.

Mheshimiwa Spika, naiunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri wa Kilimo kwa asilimia mia moja na naomba majibu chanya ya maeneo matano ya hapo juu.