Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, awali ya yote napenda kumpongeza Waziri kwa hotuba yake nzuri pamoja na Naibu wake, Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara kwa kazi kubwa na nzuri wanazofanya kwa nia ya kukuza na kuendeleza sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Spika, pili, napenda kuishukuru Serikali yetu sikivu na kibinafsi na kwa niaba ya wananchi wa Longido namshukuru Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Magufuli kwa maagizo yake ya kuwapelekea chakula wananchi wa Wilaya ya Longido waliokumbwa na uhaba wa chakula cha nafaka ya mahindi kufuatia ukame wa muda mrefu. Rais alitoa maagizo na Serikali kupitia Waziri wa Kilimo waliwatengea na kuwapeleka wananchi wa Longido mahindi ya bei nafuu ya Serikali jumla ya tani 10,000 ambayo yatawatosha hadi msimu ujao wa mvua.

Mheshimiwa Spika, baada ya pongezi na shukurani hizi, naomba sasa nijielekeze kwenye kuchangia hoja ya bajeti ya Wizara ya Kilimo iliyoko mezani mbele yetu.

Mheshimiwa Spika, kwanza, kuhusu kilimo chenye tija; kwa kuwa bado kilimo ndiyo uti wa mgongo wa uchumi wa nchi yetu, iko haja ya Serikali kuwekeza katika masuala ya msingi ambayo yakizingatiwa, wakulima wa Tanzania ambao wengi ni wakulima wadogo wadogo wanaotumia zana duni kama majembe ya mkono na plau, zana ambazo kamwe hazitatoa na kutupeleka kwenye mapinduzi ya kilimo chenye tija. Ili tuondokene na kilimo duni, Serikali iongeze bajeti na kuwekeza kwa nguvu zote katika maeneo yafuatayo:-

(a) Kuhakikisha kila Kijiji kina Afisa Ugani;

(b) Kutoa ruzuku ama mikopo ya kuwezesha wakulima kupata na kutumia zana bora za kilimo kama vile power tillers na matrekta na hivyo kutokomeza kabisa matumizi ya majembe ya mkono na plau kama zana za msingi za kilimo; na

(c) Kusambaza pembejeo za kilimo (mbegu bora, mbolea na madawa bora) kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, pili, kuhusu athari za mabadiliko ya tabianchi; kwa kuwa mabadiliko ya tabianchi yamekuwa yakiathiri kwa kiwango kikubwa kilimo kinachotegemea mvua. Nashauri Serikali iongeze bajeti ya kuwekeza katika ujenzi wa miundombinu ya kuendeleza kilimo cha umwagiliaji. Tanzania tuna maeneo mengi yenye rutuba yanayofaa kwa kilimo isipokuwa changamoto ni vyanzo vya kudumu vya maji ya kuendeshea kilimo cha umwagiliaji.

Mheshimiwa Spika, nashauri Serikali kufanya usanifu wa kujenga mabwawa ya umwagiliaji na kuboresha skimu za umwagiliaji ili kukuza kilimo chenye tija katika nchi yetu. Hili liende sambamba na kufundisha wataalam wa kilimo cha umwagiliaji.

Mheshimiwa Spika, katika Kata yangu ya Tingatinga Wilayani Longido kuna maombi ya muda mrefu ya bwawa la umwagiliaji kwenye nyanda za chini katika eneo linapotawanyika mikondo ya Mto Simba unaotokea Mlima Kilimanjaro. Survey zilifanyika tunachoomba ni bajeti ya kujenga bwawa hilo.

Mheshimiwa Spika, vilevile naomba kushauri Serikali kuwekeza katika kufanya utafiti na usanifu wa skimu bora za umwagiliaji kwa kutumia maji ya Mto Ngarenanyuki ambayo hufaa sana kwa kilimo cha nyanya, vitunguu, viazi na mboga za aina mbalimbali. Matumizi yasiyo ya kitaalam ya maji ya mto huu kwa sasa yamesababisha maji kutowafikia wakazi wa Vijiji vya Mwendo wa chini hasa wa Kijiji cha Ngareyani kilichopo Wilaya ya Longido.

Mheshimiwa Spika, naishauri Serikali ijenge matanki makubwa ya maji ya umwagiliaji yapitishwe kwenye mabomba hadi kwenye mashamba badala ya mifereji inayotumiwa kwa sasa ambayo huchapusha maji toka mtoni bila kurudisha na kupelekea kukauka kwa mto na uharibifu wa mazingira wa nyanda za mto huu muhimu.

Mheshimiwa Spika, tatu, kuhusu uwekaji wa chakula cha akiba; pamoja na mpango mzuri ulioko tayari wa Serikali kuwa na maghala mikoani kwa ajili ya kuhifadhia chakula cha akiba, naomba niendelee kusisitiza kwa Serikali kuendelea kuona umuhimu wa kuwekeza zaidi katika kuhifadhi chakula kingi zaidi cha akiba (hasa nafaka) kwa ajili ya kukabiliana na uhaba unaoweza kutokea wakati wowote kutokana na kuongezeka kwa kasi ya mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi.

Mheshimiwa Spika, kwa haya machache, namalizia kwa kutamka kuwa naunga mkono hoja.