Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri wa Kilimo. Kilimo ni uti wa mgongo wa uchumi wa nchi yetu na kinaajiri zaidi ya asilimia 70 ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu utajikita zaidi katika suala la ardhi na changamoto zake kwa wakulima wetu. Suala la kupima na kujua hali ya udongo kabla ya kutumia mbolea ni jambo la msingi sana, lakini kwa bahati mbaya sana wananchi wamekuwa hawapati huduma za kitaalam kupima acidity na alkalinity of soil kutokana na kutokuwa na vituo vya kupimia udongo na ubora wake. Nashauri Serikali ianzishe vituo vyenye kujitosheleza kwa wataalam na vifaa vya upimaji ili kujua ubora wa udongo na aina ya mbolea inayofaa kwa wakulima kulingana na mazingira husika na ikiwezekana kila wilaya au tarafa au kata viwepo vituo vya kupimia ubora na aina ya udongo na mbolea inayofaa kwa ajili ya kurutubisha na kushauri aina ya mbegu inayotakiwa.

Mheshimiwa Spika, viwanda vya mbolea pamoja na viuadudu pia viuatilifu ni vema vikawekezwa zaidi nchini ili kuhakikisha wananchi wanapatiwa huduma hizi kwa bei nafuu ili kuongeza tija katika uzalishaji wa mazao ya chakula na yale ya biashara.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na viwanda vya kuongeza thamani kwenye mazao ya kilimo ni jambo la msingi sana, hivyo basi naishauri Serikali kuweka mazingira rafiki kwa wawekezaji katika Sekta hii ya Viwanda. Viwanda kwa ajili ya kuongeza ubora na thamani vinatakiwa kuwekeza katika Viwanda vya Nguo, Viwanda vya Kubangua Korosho, Viwanda vya Kukamua Mafuta ya Alizeti, Michikichi, Karanga, Pamba. Aidha, viwanda kwa ajili ya kuchakata matunda pia ni vema vikaongezwa ili kuwakomboa wakulima wa matunda.

Mheshimiwa Spika, suala la vipimo kwa ajili ya mizani ya kupimia uzito kwa ajili ya wakulima wetu bado kuna shida kubwa hasa kutokana na wanunuzi mara zote ndio huwa ni wamiliki wa mizani ambayo siku zote huichezea kwa lengo la kuwapunja wakulima, hivyo basi ni vyema Serikali ikaweka mkazo kuhakikisha kwamba wakulima wanamiliki mizani yao wenyewe na Mamlaka au Wakala wa Vipimo nchini kuihakiki mizani hiyo mara kwa mara ili kuepusha wakulima kupunjwa.

Mheshimiwa Spika, suala la mabadiliko ya tabianchi; iko haja kwa Serikali kuwekeza zaidi katika Idara ya Utabiri wa Hali ya Hewa kwani kwa sasa utabiri wa hali ya hewa nchini unafanyika kwa kubahatisha na matokeo yake wananchi wanapata hasara kwa kutokupata taarifa sahihi na matokeo yake wananchi wanapambana na ukame au mafuriko na hivyo kuathiri wakulima kwa kiwango kikubwa.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa uharibifu mkubwa wa mazingira unaathiri moja kwa moja Sekta ya Kilimo kwa vile uharibifu wa mazingira kwa kukata miti husababisha ukame na mmomonyoko wa udongo, naishauri Serikali kuwekeza katika uhifadhi wa mazingira kwa kupanda miti na kuwashauri wakulima kutokata hovyo miti basi wahakikishe wanaacha baadhi ya miti mashambani.