Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

Hon. Daniel Edward Mtuka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Manyoni Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

MHE. DANIEL E. MTUKA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kupata fursa hii walau ya dakika tano. Ninayo tu mambo machache sana kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, la kwanza, niende moja kwa moja kwenye hoja yangu, kaka yangu Mheshimiwa Mwaka, Mbunge wa Chilonwa, yeye alizungumzia hali ya hewa katika eneo la kati ya nchi hii ni kame. Naunga mkono hoja yake na mazungumzo yake, ni kweli kabisa tuko kwenye eneo kame, lakini kuwa na ukame maana yake sio kwamba hatuna udongo au hauna rutuba. Udongo wetu una rutuba ya kutosha, Mkoa wa Singida na Dodoma.

Mheshimiwa Spika, nikizungumzia hali ya Manyoni kwa mfano, bonde la ufa, limeimega Manyoni pamoja na Dodoma, kwa hiyo tumeshirikiana ule ukame. Kwa upande wangu bonde la ufa, hali ni ngumu sana kwa mfano kwa mwaka huu hatuna chakula, lakini nije na pendekezo la Mkakati kwa maana ya kupunguza sasa au kuondokana na hali ya njaa.

Mheshimiwa Spika, sisi Manyoni, tuna eneo linaitwa Bwawa la Tope la Bahi, Bwawa hili lina mito miwili mikubwa, ambayo inatoka ukanda wa Kaskazini, Manyara inamwaga maji kwenye lile bonde, ni bonde lina rutuba kubwa ya kutosha. Naomba Wizara hii ya Kilimo itusaidie, kukomesha njaa kwenye bonde hili, kwa upande Dodoma kwa maana ya Bahi na upande wa Manyoni. Tuwekeeni Bwawa kubwa la mkakati kwenye bonde hili, tunayo mito miwili mizuri inaleta udongo wenye rutuba ambao umetoka kule juu.

Mheshimiwa Spika, maji yapo ya kutosha na uwezekano ni mkubwa, hebu tusaidieni sana, walete wataalam, wafanye utafiti, watuchimbie bwawa la kutosha. Tunazo ekari zaidi ya 50,000 nzuri zenye rutuba tukaweka bwawa pale, watakuwa wametusaidia kabisa lakini tutalisha na sehemu zingine za nchi hii ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna kabwawa kamoja si ka mkakati ambako tayari andiko limeshakamilika liko Wizarani, mwaka jana ilikuwa iwekwe kwenye Bajeti ianze kwa sababu utafiti, upembuzi yakinifu ulishafanyika, usanifu wa kina umeshafanyika, kila kitu kiko tayari ni kujenga tu. Mwaka jana ilikuwa iingizwe kwenye bajeti wakasema tutaingiza mwaka huu, nimeuliza maswali karibu mara tatu katika Bunge hili, Bwawa la Mbwasa, lakini nimeangalia Bajeti tena halipo, sijui tatizo ni nini? Njaa itatuua jamani na mimi sioni aibu, nitaomba tu chakula kwa sababu lile bonde halina chakula sasa, lakini wakitujengea kabwawa haka, ile njaa nitakuwa nimeondokana nayo, hebu tusaidieni tuna maji ya kutosha, tusaidieni jamani.

Mheshimiwa Spika, naomba waangalie, Bajeti Kuu bado haijasomwa, waangalie bwawa hili, waliingize kwenye Bajeti ya mwaka huu, tuchimbiwe bwawa pale Mbwasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho, Singida tumejinasibu kwamba tunalima alizeti na ndiyo brand yetu sisi, lakini bei ya mbegu iko juu sana hii ambayo imefanyiwa research kwa maana ya hybrid. Kwa mfano kilo moja tu ya mbegu inaitwa hysun F124 inauzwa kwa wastani wa shilingi 35,000 kilo moja. Wakulima wangu wale wa Manyoni wale, Singida yote ni wachovu, kilo moja shilingi 35,000 watalima wapi? Nani atanunua hiyo mbegu? Watuletee angalau ruzuku basi watunyanyue nyanyue ili tupandishe zao hili la alizeti, hii bei si rafiki kwa maana kwamba Singida tuwe ma-giant wa uzalishaji wa alizeti na mbegu hii, hapana.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana, malizia. (Makofi)

MHE. DANIEL E. MTUKA: Mheshimiwa Spika, baada ya machache hayo, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante. (Makofi)