Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

Hon. Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa hotuba nzuri, lakini na kazi wanayoifanya yeye na Manaibu Waziri.

Mheshimiwa Spika, nina mambo machache sana leo ya kuzungumza, mambo kama mawili tu. Jambo la kwanza ningeomba kuchangia kwenye kilimo cha mkonge, kwa mwaka 2014 - 2018 kwenye mkonge tumezalisha tani 190,649. Katika hizo Mkoa wa Tanga peke yake umezalisha tani 106,221 na katika Mkoa wa Tanga Wilaya inayoongoza kwa kuzalisha mkonge ni Wilaya ya Korogwe hasa Halmashauri ya Korogwe. Hata hivyo, tumekuwa na changamoto kadhaa kwenye zao la mkonge, changamoto kubwa ya kwanza ni usimamizi usioridhisha wa taasisi inayosimamia zao la mkonge. Pia ushiriki mdogo wa taasisi zetu za utafiti kama ile ya pale Mlingano kwenye kusaidia kuendeleza zao la mkonge.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi tumekuwa na wakulima wadogo wengi kule Korogwe na Mkoa mzima wa Tanga, lakini tuna changamoto kubwa sana. Wakulima walio wengi hata mbegu wanaokota kutoka kwenye mashamba ya mkonge ya muda mrefu kwenda kupanda kwenye mashamba yao. Mbegu hizi zinafanya mkonge huu usiweze kuwa na muda mrefu wa kuvunwa lakini tungeweza kuvitumia vizuri vyuo vyetu vya utafiti na taasisi za utafiti kama pale Mlingano tungeweza kuwa na mbegu bora na wakulima wetu wangelima na wangeweza kuvuna mkonge kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Spika, inawezekana changamoto kubwa inayotusumbua ni fedha. Kwenye zao la mkonge kwa miaka mingi tunapata service levy ya 0.3%, lakini kwa mujibu ya Sheria ya Fedha kwenye mazao haya ya biashara tunapaswa pia kuwa na ushuru wa mazao produce cess lakini kwa mujibu wa Sheria ya Fedha produce cess anayepaswa kuilipa ni mnunuzi.

Mheshimiwa Spika, sasa wakulima hawa wakubwa wa mikonge ambao wanazalisha singa wenyewe mnunuzi wanamkuta nje, ambapo kule nje wanamkuta wakala hakuna nani ambao; kwa hiyo ni vigumu sana kupata produce casse wanapoleka mkonge kule nje; na hata halmashauri zetu zimekuwa zikikosa sana mapato kwa sababu hii.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia vizuri kama tungekuwa tunapata produce cess 2014 mpaka 2018 tungepata zaidi ya bilioni tisa kwenye produce cess peke yake. Kwenye service levy tumepata takriban shilingi milioni sita na kitu. Nilikuwa naiomba sana Serikali tuangalie namna, hapa hatuombi kuibua kodi mpya, hii kodi ipo kwa mujibu wa sharia. Changamoto tuliyonayo ni namna ya kupata fedha hizi; kwa sababu mnunuzi anayepaswa kulipwa yuko nje ya nchi na hajumo ndani ya nchi.

Mheshimiwa Spika, tuna mfumo mpya sasa hivi; na ninampongeza sana Mheshimiwa Mkuu wetu wa Mkoa wa Tanga, ametusadia sana na ametusaidia kupata haki na faida kwa wakulima wadogo wa mkonge. Tuna wakulima wadogo wa mkonge ambao wanauza mazao yao ya mkonge kupitia vyama vyao vya ushirika na mnunuzi anapatikana kwa kushindanishwa kwenye mnada. Sasa tunapopata mnunuzi anayeshindanishwa kwenye mnada ananunua mazao ya wakulima hawa wadogo wa mkonge yule mnunuzi analipa produce cess kwa sababu yeye anakuja kununua ndani; lakini hawa wakulima wakubwa wanaopeleka nje hawalipi, hatimaye hii ita-discourage hawa wanunuzi wanaokuja kununua mazao ya wakulima wadogo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Mnzava.

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.