Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo Zilizowasilishwa katika Mkutano wa Kumi na Nne na Mkutano wa Kumi na Tano wa Bunge

Hon. Jenista Joackim Mhagama

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Peramiho

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo Zilizowasilishwa katika Mkutano wa Kumi na Nne na Mkutano wa Kumi na Tano wa Bunge

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU,SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.

Kwanza kwa dhati kabisa jukumu hili la kupokea majedwali mbalimbali ya marekebisho ya sheria ambayo yamekuwa yakichambuliwa na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo limekuwa likifanywa na Ofisi ya Waziri Mkuu, na sisi pia tumekuwa na wajibu wa kuweka Mezani Magazeti yote ya Serikali yanayohusiana na sheria ndogo nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli sisi tumekuwa ndio tukienda kupokea mapungufu yote yanayojitokeza kwenye sheria ndogo ambazo zimekuwa zikitungwa chini ya taasisi, mamlaka mbalimbali za Serikali na Wizara mbalimbali. Na kifupi niseme Ofisi ya Waziri Mkuu ndiyo imekuwa na nafasi kubwa ya kukutana ana kwa ana na Kamati ya Sheria Ndogo na kuyajua na kuyafahamu yote yanayojiri katika mfumo mzima na mlolongo wa utungaji wa sheria ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nasema hivyo kwa nini; nataka nianze kwa kumpongeza sana Mwenyekiti wa Kamati hii ya Sheria Ndogo kwa kazi nzuri anayoifanya ndugu yetu, mzee wetu, Mheshimiwa Chenge amekuwa akifanya kazi nzuri sana siyo kwa niaba ya Kamati tu lakini kwa Serikali nzima. Lakini anashirikiana bega kwa bega na Makamu Mwenyekiti, ndugu yangu Mheshimiwa Ngeleja na Wajumbe wa Kamati hii ni wabobezi na ni Wajumbe mahiri kwelikweli katika kuishauri Serikali kwenye eneo hili la kusimamia na kuendelea kuzipitia sheria hizi ndogo zinazoletwa na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya yote yanafanyika kwa kuzingatia Kanuni ya 37(2) ambayo inatutaka sisi Serikali baada ya utungwaji wa sheria zote ndogo kuziwasilisha hapa Mezani, na tumekuwa tukifanya hivyo katika kila mkutano na baada ya hapo Kamati ya Sheria Ndogo inapata nafasi ya kuzifanyia uchambuzi. Niungane na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, jambo hilo sisi kama Serikali tumekuwa tukilishughulikia vizuri. Mwanasheria Mkuu wa Serikali amejibu hoja mbili na mimi nitajibu hoja kama mbili zilizobakia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali tuliagizwa na Kamati ya Sheria Ndogo kwamba kila wanapotoa jedwali kama hili lililotolewa leo, taasisi, Wizara na mamlaka nyingine zote ndani ya Serikali zihakikishe kwamba katika yale maeneo ambayo tumekubaliana kati ya Kamati na Serikali yanakuka misingi ya utungaji wa sheria mama katika utekelezaji wake kwa kutunga hizo sheria ndogo haraka sana zifanyiwe mabadiliko ili ziweze kuendana na sheria mama na ziweze kuwafaa wananchi katika matumizi yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba lilihakikishie Bunge lako hili Tukufu katika Mkutano wa Kumi na Nne na Mkutano wa Kumi na Tano wa Bunge agizo hilo limeanza kutekelezwa.

Nitatoa mfano wa sheria ndogo mbili tu lakini nyingi zimeshafanyiwa kazi; mfano Sheria Ndogo ya Ushuru wa Stendi Halmashauri ya Chalinze ya mwaka 2018 kifungu cha 9(6) kimekwisha kurekebishwa na kimetangazwa upya baada ya marekebisho katika Gazeti la Serikali Na. 604 la tarehe 16, Agosti, 2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mwingine ni Sheria Ndogo za Ushuru wa Maegesho Halmashauri ya Mji wa Bunda ya Mwaka 2018 kifungu cha 4(2), na yenyewe imetangazwa katika Gazeti la Serikali Na. 606 la tarehe 16, Agosti, 2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesema hizi ndogo mbili tu lakini zile zote ambazo tulishaletewa. Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu tumeshaandika kwenye wizara mbalimbali, na wizara zimeshafanya marekebisho na zimeshatangaza kwenye kwenye Gazeti la Serikali kama tulivyoagizwa na Kamati ya Sheria Ndogo. Tayari tumeshawasilisha nakala za magazeti hayo kwenye Ofisi ya Katibu wa Bunge. Kwa hiyo Kamati ya Sheria Ndogo tunaomba kuwahakikishia kwamba tunatekeleza maagizo yenu. Mlitushauri pia kwamba mamlaka zote zilizokasimiwa na Bunge madaraka ya kutunga sheria ziwashirikishe wadau katika utungaji wa sheria hizo ndogo; tunafanya hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hapa kwa mfano nina Sheria Ndogo za Uchaguzi wa Serikali za Mitaa. Mlimsikia Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, alitoa ushahidi pia hapa wakati wa kutungwa kwa sheria hizo ndogo zitakazosimamia pia uchaguzi ambapo wadau wote walishirikishwa. Kwa hiyo mawaziri wamekuwa wakifanya kazi hiyo kwa kuzingatia maagizo ya Kamati yetu ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, agizo lingine lilikuwa kwanza, kuimarisha Ofisi ya Mpiga Chapa wa Serikali ambayo iko chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kazi hiyo imefanyika vizuri. Tumeshaanza kununua mitambo na tumeshaanza kuiondoa ile mitambo ambayo ilikuwa imepitwa na wakati na mingine iliyoharibika tumeanza kuitengeneza ili kuiimarisha ifanya kazi yake vizuri. Vilevile mmetuambia ofisi ile ishughulike kufanya uhariri kwa kushirikiana na mamlaka zote ambazo zimetunga hizo sheria ndogo. Kazi hiyo tumeanza kuifanya, na matokeo chanya ya kuanza kufanyika kwa kazi hiyo ni kama ifuatavyo;

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mkutano wa Kumi na Nne wa Bunge, Serikali iliwasilisha sheria ndogo kama 196, na baada ya uchambuzi kupitia kwenye kamati ndogo tuliona kwamba, kama nitakuwa nina kumbukumbu sahihi, sheria ndogo 14 ndiyo zilizoonekana na kasoro. Kwa hiyo unaona kwamba tayari Serikali inazidi kupunguza mapungufu ambayo yanajitokeza kwenye utungaji wa sheria wa sheria ndogo. Hii yote ni kazi nzuri inayofanywa na Kamati yetu ya Sheria Ndogo ambayo sisi Serikali inatusaidia sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, labda mfano mwingine mdogo wa mwisho, Mkutano wa Kumi na Tano wa Bunge Serikali iliwasilisha mezani sheria ndogo kama 174, na baada ya uchambuzi wa Kamati ya Sheria Ndogo tuliona sheria kama 22 zilikuwa na matatizo. Kwa hiyo unaona kwamba kuna trend pia ya kazi nzuri ambayo inaibuliwa na Kamati ya Sheria Ndogo inayotufanya sisi ndani ya Serikali kujipanga sawasawa na kuhakikisha sasa zile sheria ndogo tunazozileta ziwe ni sheria ambazo zinafuata mfumo wa uandishi wa sheria kwa kuzingatia sheria mama, na vile vile ziwe zinakidhi matakwa halisi ya watumiaji wa sheria hizo ambao ni wananchi wa Tanzania. Tumesema sisi na tumekubaliana ndani ya Serikali, tumeweka mpango mkakati wa kujitathmini wenyewe ndani ya taasisi na wizara mbalimbali kuhakikisha kwamba jambo hili halijirudiirudii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli wakati mwingine ninaomba nikubaliane na Kamati ya Sheria Ndogo, wakati mwingine makosa tunayoyafanya ni makosa ambayo kwa kweli yangeweza kurekebishwa mapema kabla hata sheria haijaanza kutumika wala haijafika Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwa ushauri miongozi ambayo tumekuwa tukiipata kutoka kwenye Kamati ya Sheria Ndogo tutaendelea kuizingatia. Nia ni njema, na hatima yake ni Tanzania yetu, kwa manufaa ya Watanzania wote kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza sana Kamati ya Sheria Ndogo, na kwa kweli kazi yenu ni kazi nzuri, kazi njema iliyotukuka. Waheshimiwa Mawaziri wote tutaendelea kuwaunga mkono, tutakuwa pamoja na ninyi kwa sababu tunasaidiana kwa ajili ya ustawi wa taifa la Watanzania na sisi wote ni Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)