Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo Zilizowasilishwa katika Mkutano wa Kumi na Nne na Mkutano wa Kumi na Tano wa Bunge

Hon. William Mganga Ngeleja

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sengerema

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo Zilizowasilishwa katika Mkutano wa Kumi na Nne na Mkutano wa Kumi na Tano wa Bunge

MHE. WILLIAM M. NGELEJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, nilishaunga mkono hoja dakika chache zilizopita wakati nawasilisha kwa niaba ya Mheshimiwa Mwenyekiti wetu wa Kamati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie jambo moja la uelewa lakini pia na ushauri kwa Serikali. Ukiondoa kasoro ambazo tumekuwa tukiziona katika hizi sheria ndogo za kiuandishi wakati mwingine mambo madogomadogo yale ya kawaida, jambo kubwa ambalo nataka kulizungumza kwa niaba ya Kamati yetu lakini lenye manufaa kwa nchi kupitia Bunge lako Tukufu, na ni jambo la kukumbushana, ni kutambua kwamba mfumo tulionao wa utungaji wa sheria ndogo hizi za aina yoyote ile kimsingi hautoi fursa ya kuzifanyia marekebisho zile kasoro ambazo zimebainika katika sheria hizo ndogo kabla hazijaanza kutumika. Na hiyo ndiyo changamoto kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia jambo la kufumua huo mfumo ni jambo kubwa sana, hatuwezi kuzungumza katika muktadha huu. Ushauri wangu kwa Serikali na kwa kupitia Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Mawaziri waliopo; inaweza kutumika hekima na busara tu administrative ya kiuongozi kwamba pengine hizi sheria ndogo zinapokuwa zimemaliza kutungwa, na kutokana na uzoefu tuliouona kwa sababu zipo kasoro zingine ni za msingi ambazo tunazibaini ambazo kimsingi kwa sababu ya ule uasili wake kwamba sheria ndogo au kanuni zikitungwa na Serikali zinaanza kutumika kabla hazijafika Bungeni, wananchi wengi wanaweza kuumia wakaathirika na hizo sheria zenye kasoro kubwa za msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kwa Serikali na hasa kwa Ofisi ya Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali; waone kama unaweza kufanyika utaratibu wa kiutawala tu hekima ikatuma na busara kwamba hizi kanuni na sheria ndogo zote ambazo zinatungwa kabla hazijatumika zile ambazo zinakidhi vigezo vya kuletwa Bungeni, zisianze kwanza kutumika, zije Bungeni zipitiwe na Bunge halafu ndiyo zikafanye kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu utaratibu umeaza lakini huu umeanza kwa hekima na busara za Mawaziri katika baadhi ya maeneo. Mheshimiwa Dkt. Mwakyembe tunaye hapa, tunampongeza sana, lakini pia Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mheshimiwa Mpina, na Waheshimiwa Mawaziri wengine wamekuwa wakinisimamisha, nakumbuka Ofisi ya Nishati na Madini pia tulishawashari mara kadhaa. Sasa tunashauri huu utaratibu na hekima hizi zirasimishwe kiutawala kwa sababu kufumua ule utaratibu, narudia tena, inahitaji mjadala mpana wa kisera na mfumo mzima wa sheria, huko ni mbali sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nalisema hili nikirejea ambacho kilishawahi kufanywa na Bunge hili Tukufu pamoja na Serikali yetu. Mwaka 2007 wakati nchi iko kwenye kiwango cha juu kabisa cha perception au niseme mgogoro uliokuwa unajitokeza ama tafsiri na dhana na namna ambavyo sisi tunanufaika na rasilimali za madini na hasa katika kuiona na ule usiri ya mikataba, Bunge lako Tukufu lilikaa na Serikali wakakubaliana. Kwa wale wanaohitaji kuiona ile mikataba ya madini ambayo kwa utaratibu wa kisheria wakati huo ilikuwa siyo rahisi mwananchi yeyote kuiona, hata sisi Wabunge, ulianzishwa utaratibu hapa Bungeni kama mtu anahitaji mikataba kupitia Ofisi ya Bunge mikataba ilianza kutolewa hapa kupitia Ofisi ya Bunge. Aifikie mtu asome ayaseme anayotaka kuyaona halafu aishauri Serikali ama Bunge namna bora ya kuboresha maeneo hayo, kabla hatujarekebisha zile sheria zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hata hili kwa sasa Serikali inaweza kutafakari vizuri, narudia tena, administratively tu wakaona kwamba pengine sasa kweli kama ambavyo Bunge limekuwa likipewa-concerned wakae pamoja, kanuni yoyote inapoingizwa hapo Mezani isitumike kwanza kule mpaka sisi tutakapoipitia Kamati ya Sheria Ndogo. Na sisi Kamati ya Sheria Ndogo tuko tayari sana, sana kuliko ilivyokuwa jana, kuliko ilivyokuwa juzi, kuzipitia kanuni zote ambazo Serikali inatutumia hata kwa uharaka wanaokusudia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)