Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo Zilizowasilishwa katika Mkutano wa Kumi na Nne na Mkutano wa Kumi na Tano wa Bunge

Hon. Saed Ahmed Kubenea

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Ubungo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo Zilizowasilishwa katika Mkutano wa Kumi na Nne na Mkutano wa Kumi na Tano wa Bunge

MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi inayofanywa na Kamati ya Sheria Ndogo ni kazi nzuri sana, nasi kama Wabunge tunaipongeza sana Kamati hii chini ya Mheshimiwa Adrew Chenge mzoefu, Mwanasheria Mkuu wa zamani wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Miswada au Sheria nyingi zinazoletwa hapa Bungeni zinakuwa na matatizo makubwa sana. Jana tumepitisha sheria hapa ya kumpa mamlaka Mkurugenzi wa EWURA ambaye atakuwa na mamlaka ya kushtaki, kufuta mashtaka na kuharibu mali. Sasa huko tulishatoka, vyombo kama TAKUKURU kwa mfano, tulivitungia sheria humu ndani visiweze kupeleka mashtaka Mahakamani bila kupeleka kwa DPP. Polisi tuliwaondolea mamlaka ya kupeleka kesi Mahakamani bila kupata kibali cha DPP ili kuondoa upendeleo na kukomoa watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima tuwe tuna- balance hivi vitu, hatuwezi kuchukua mamlaka ya mtu yote tukakabidhi kwa mtu mmoja yeye mwenyewe ndiyo akawa Mwendesha Mashtaka, yeye mwenyewe ndiyo akawa Hakimu, yeye mwenyewe ndiyo akawa mlalamikaji, haya ni mambo yanayokwenda kinyume cha Katiba yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana Serikali inapotaka kuleta Miswada au Sheria Ndogo katika Kamati zetu za Bunge ni lazima izingatie Katiba yetu ambayo ni msingi mkuu wa sote tuliopo hapa tuliapa kuilinda na kuitetea, tukija humu Bungeni tukiweka ushabiki wa kivyama, tukiweka ushabiki wa kukomoana hatutaitendea haki nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashauri sana kwamba hii kazi ambayo inafanywa humu Bungeni na Kamati zetu za Bungeni na Bunge lenyewe ni kazi nzuri lakini Serikali ilete mambo haya yawekwe vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma hili jedwali asilimia karibu 70 ya sheria ndogo zilizoletwa humu zina makosa makubwa ya kiuandishi na mengine yanapingana na Katiba yetu. Kwa mfano, kuna Sheria hii ya Madaktari hata Kamati inasema inapingana na Ibara ya 13(3) ya Katiba ambayo inatoa uhuru wa kila mtu kutobaguliwa kwa mujibu wa sheria. Serikali ambayo imeapa kulinda Katiba lakini inatunga Kanuni na inaleta sheria ndani ya Bunge inayopingana na Katiba unashangaa kwamba Mheshimiwa Waziri ameapa kulinda Katiba, Manasheria Mkuu wa Serikali ameapa kulinda Katiba, Kamati inasema sheria hiyo mnayoleta humu ndani inapingana na Katiba! Wao wamo ndani wanataka mpaka watu waende Mahakamani waka-challenge hivi vitu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitengemea Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Mawaziri waliopo humu na bahati njema Waziri Mkuu yumo humu ndani wangelichukuwa hili jambo wakaliondoa kabisa wakakubaliana na mapendekezo ya Jedwali la Kamati ya Sheria Ndogo ili jambo hili lisituletee matatizo. Hatuwezi kutunga sheria humu ambazo zinapingana na Katiba. Unashangaa kwamba sisi tumekuja humu tumeapa kulinda Katiba lakini tunapitisha Sheria na Kanuni zinazopingana na Katiba na Kamati inatuelekeza humu kwamba hii inapingana na Katiba Ibara ya 13(3) wameainisha sasa tunafanya nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hata sheria tunazotunga humu ndani ya Bunge, Serikali inaleta sheria wakati mwingine unashangaa baada ya miezi sita sheria inabadilishwa. Wakati wa kuipitisha vigelegele, hoihoi utadhani unakomoa, unatunga sheria dhidi ya wakoloni, kumbe unatunga sheria dhidi ya Watanzania wenzako. Yaani utadhani unatunga sheria dhidi ya makaburu kumbe unatunga sheria dhidi ya Watanzania wenzako, halafu baada ya miezi sita unakuja unasema sheria hii tumeshauriwa tumeona tuondoe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jamani, tuliwaambia leteni sheria zenye maslahi ya nchi, msilete sheria kwa kukomoa watu, sisi sote ni Watanzania. Leo mnaweza mkawa chama tawala kesho mkawa chama cha upinzani; leo mnaweza mkawa mko madarakani, kesho hamko madarakani. Wapo wengi ambao walikuwa madarakani jana – siyo juzi, jana – leo hawapo, jana siyo juzi wala majuzi, mifano ipo na mnaijua, hatutaki kuyasema humu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nikushukuru sana kwamba vyombo hivi ambavyo vimetungwa kwa mujibu wa kanuni zetu tuvitumie vizuri, siyo kwa kukomoa watu. Nakushukuru sana.