Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Kuridhia Mapendekezo ya Ubadilishaji Hadhi Sehemu ya Eneo la Pori la Akiba Kigosi Kuwa Hifadhi ya Taifa Kigosi pamoja na Azimio la Kuridhia Mapendekezo ya Ubadilishaji wa Hadhi Sehemu ya Eneo la Pori la Akiba la Igalla Kuwa Hifadhi ya Taifa ya Mto Ugalla pamoja na Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Minamata kuhusu Zebaki (Minamata Convention on Mercury)

Hon. Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Azimio la Kuridhia Mapendekezo ya Ubadilishaji Hadhi Sehemu ya Eneo la Pori la Akiba Kigosi Kuwa Hifadhi ya Taifa Kigosi pamoja na Azimio la Kuridhia Mapendekezo ya Ubadilishaji wa Hadhi Sehemu ya Eneo la Pori la Akiba la Igalla Kuwa Hifadhi ya Taifa ya Mto Ugalla pamoja na Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Minamata kuhusu Zebaki (Minamata Convention on Mercury)

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushuru sana kunipa nafasi niweze kuchangia na kwa ujumla mambo mengi yameshazungumzwa na Wabunge wengine waliochangia, lakini nitumie nafasi hii kwanza kabisa kusema naunga mkono maazimio yote yaliyoletwa na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuunga mkono maazimio yaliyoletwa na Serikali, pia nitumie nafasi hii kuipongeza sana Serikali kwa kazi kubwa wanayoifanya hasa watu wa Wizara ya Maliasili na Utalii kwa ulinzi mkubwa wa rasilimali zetu, hata ongezeko la tembo mpaka wanakuja kwenye makazi ya watu sasa hivi ni matokeo ya kazi kubwa wanayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya kazi kubwa mliyoifanya ya kuhifadhi na tembo wamekuwa wengi basi mtusaidie kwenye yale maeneo kama kule Korogwe tumeathiriwa sana na tembo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaunga mkono, nichangie kwa upande wa maazimio haya mawili ya kubadilisha hadhi Mapori ya Akiba ya Ugalla na Kigosi kuwa Hifadhi za Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli ziko faida nyingi sana kupandisha hadhi mapori haya na tunajua kwamba Hifadhi ya Taifa ni hatua ya juu kabisa ya uhifadhi kwa maana kwenye Hifadhi ya Taifa haturuhusu shughuli nyingine za kibinadamu, kwa hiyo kwa mapori haya kupandishwa hadhi kuwa Hifadhi ya Taifa tutakuwa tumeimarisha ulinzi wa rasilimali zetu, ikiwemo wanyama na baionuwai nyingine kwenye maeneo haya ya mapori.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tunaipongeza sana Wizara na tunaunga mkono azimio hili kwa sababu ni jitihada za kwenda kuongeza na kuimarisha ulinzi wa rasilimali zetu, lakini pia iko faida nyingine ya kupandisha hadhi mapori haya na kuwa Hifadhi ya Taifa. Faida nyingine kubwa ni kwenda kusaidia kuongeza mchango kwenye Pato la Taifa, lakini pia kwenda kugusa maisha ya watu wetu, hasa kwenye maeneo ambayo yanapakana na hifadhi hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo nyuma tulikuwa tunapiga kelele kidogo baadhi ya watu kwenye mambo kama ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Chato, sasa kwa kazi kubwa inayofanywa na Serikali sasa hivi ya kuimarisha miundombinu kama ujenzi wa viwanja wa ndege, kama reli ya SGR, kama ujenzi wa barabara, lakini pia kufufuliwa kwa shirika letu la ndege ni sehemu ya kutusaidia kwenda kuongeza pato kwa maana inakwenda kuchocheo utalii kwenye hifadhi hizi ambazo zitakwenda kuanzishwa sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi naunga mkono maazimio hayo, lakini naomba nishauri kwenye maeneo mawili, TANAPA ina hifadhi 19 na jambo hili limesemwa sana na tunaomba tuliweke msisitizo kidogo, tukichukua azimio tulilopitisha jana na haya mawili ya leo na yakienda kupita na hifadhi hizi zikianzishwa tutakuwa na jumla ya hifadhi 22 na hifadhi zinazoweza kujiendesha ni hifadhi tano. Kwa hiyo, unaweza ukaona huo mzigo wa kuendesha hifadhi nyingine ulivyokuwa mkubwa kwa TANAPA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na yale majibu mazuri sana ya kitaalamu aliyoyatoa Mheshimiwa Waziri wa Maliasili jana, lakini tunaomba tushauri vitu viwili, kitu cha kwanza, ni lazima Wizara iisimamie TANAPA vizuri na iwaelekeze waongeze Mkakati madhubuti wa kutangaza masoko ili kusaidia hifadhi hizi mpya zinazoanzishwa tusichukue muda mrefu sana zikaendelea kuwa tegemezi, ziweze kuanza kuingiza mapato vizuri na ziweze kuweza kujiendesha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo la pili ni kwenye mzigo wa kodi, lilisemwa jana, lakini hata mama yangu Mheshimiwa Lulida amelizungumza hapa. TANAPA wanalipa kodi nyingi, TANAPA wanalipa asilimia 15 wanatoa asilimia 15 ya gawio kwenda Serikalini, malipo ya asilimia tatu kwenda kwenye tourism development levy, wanalipa skills development levy, lakini pia wanalipa cooperate tax, lakini hayo yote siyo shida ile miradi wanayofanya kwa ajili ya kusaidia jamii ambazo zinapakana na Hifadhi za Taifa na yenyewe inakuwa inatozwa kodi kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nimuombe sana Mheshimiwa Waziri tunaunga mkono azimio hili, ni azimio zuri litatusaidia kuimarisha maliasili zetu, litatusaidia kuongeza pato la Taifa lakini...

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: ...salama nipongeze mkakati wa kuweza kutangaza vivutio vyetu ili waongeze utalii kwenye maeneo yetu, naunga mkono hoja.