Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

Hon. Dr. John Danielson Pallangyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Arumeru-Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niseme kidogo kuhusu Mpango huu wa Serikali ambao umeletwa mbele ya Bunge lako tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na kumpongeza Waziri wa Fedha na Mipango, Naibu Waziri na watendaji wake wote kwa kazi nzuri ambayo wamekuwa wanafanya. Kwa kweli wanafanya kazi nzuri sana ya kusimamia mapato pamoja na kupanga mipango ambayo imetufikisha mahali tulipofika. Niseme pia hata huu Mpango ambao wameuleta 2020/2021 ni mzuri na naunga mkono a hundred percent. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukiona Mawaziri wanafanya vizuri, watendaji wakuu wa Serikali wanafanya vizuri, ujue kwamba nyuma yao kuna kiongozi wao. Nichukue nafasi hii kwa dhati kabisa kumpongeza Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, ambaye anafanya kazi nzuri mno na ndiyo maana Mawaziri nao wanafanya kazi nzuri. Tumeshuhudia mambo mengi yanafanyika hapa nchini kwenye sekta nyingi; afya, elimu, nidhamu Serikalini, vita dhidi ya rushwa, umeme na kadhalika lakini kwa kipekee miradi mikubwa ya kimkakati; reli ya kisasa, Mradi wa Kufua Umeme Stiegler’s Gorge, kufufua Shirika la Ndege Air Tanzania kwa kununua ndege nane mpaka sasa. Sina haja ya kuyazungumza sana haya kwa sababu kila mmoja anayaona, kila mmoja anayafahamu lakini itoshe kusema kwamba tunampongeza Rais kwa kazi nzuri na tunamuombea maisha marefu na afya njema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo ni- comment kidogo kwenye Mpango huu na nianze na kilimo. Kilimo ndicho kimebeba Watanzania katika ajira kwani idadi kubwa ya Watanzania wanategemea kilimo na toka tunapata uhuru tumekuwa tunaimba kilimo ndiyo uti wa mgongo wa uchumi wetu. Yamepita maazimio mengi; Azimio la Iringa (Siasa ni Kilimo) na baadaye juzijuzi likaja Azimio la Kilimo Kwanza mpaka magari ya Wabunge na Mawaziri yakaitwa kwa jina hilo la Kilimo Kwanza lakini pamoja na hivyo bado kilimo hakijakaa sawa ni kwa sababu hatujaweka msukumo unaostahili kwenye kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani pale mwanzoni tulidhani kwamba mechanization alone ingetusaidia lakini kumbe kilimo cha kutegemea mawingu, kutegemea mvua hakitatufikisha mahali. Ndiyo maana mpaka leo toka tumepata uhuru kilimo chetu bado kinasuasua na niseme sasa wakati umefika kwenye Mpango huu wa 2020/2021 Wizara iangalie namna ambayo itaweka msukumo mkubwa kwenye irrigation. Tunaomba Serikali iwekwe nguvu nyingi kwenye miundombinu ya irrigation ili tubadilike tuache kungojea mvua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona mazao ya traditional cash crops, kahawa, pamba, tumbaku, wenzangu wamesema yamedorora. Kule kwetu kahawa ndiyo kabisa, tulikuwa tunaitegemea zamani lakini kahawa imekwisha kabisa kabisa na sababu kubwa ni pamoja na population boom. Yale mashamba ambayo yalikuwepo wamezaliwa watoto wengi badala ya mashamba sasa ni plots, kwa hiyo hakuna mahali pa kulima kahawa. Badala yake wananchi vijana wame-resort kwenye hot cultural farming. Nilipata faraja kubwa sana Mheshimiwa Naibu Waziri wa Kilimo juzi aliposema kwamba wanaleta Muswada wa kuanzisha mamlaka ambayo tunaamini ita-coordinate na ku-promote hot cultural farming. Suala hilo ni la msingi na lifanyike haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimeshuhudia vijana wanalima mboga mboga zao ukifika wakati wa kuvuna yale mazao yanaozea shambani kwa sababu barabara zimeharibika. Barabara za vijijini ni za kutengeneza, kwa hiyo msukumo mkubwa upelekwe katika kutengeneza miundombinu ya kufuata yale mashamba ambayo vijana wanahangaika, wanalima karoti, wanalima nyanya na pilipili hoho na kila kitu lakini mwisho wa siku yale mazao yanaoza kwa kukosa usafiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imefanya kazi nzuri sana kwenye miundombinu, barabara, madaraja na hata miradi mikakati ambayo imeshatekelezwa imefanyika vizuri. Nilisikia siku moja Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi akasema, sera sasa hivi imelenga kuunganisha mikoa kwa barabara za lami tu, lakini nikasema kwamba sera siyo static ni dynamic inaweza ikabadilishwa kidogo pale ambapo barabara inaonekana inaweza ikastawisha wananchi mradi utekelezwe. Hapa nitoe mfano, barabara ya King’ori – Malula kwenda King’ori Madukani kwenda Maruvango, kwenda Ngarenanyuki, Ngabobo, Uwiro inakwenda mpaka Oldonyo Sambu, barabara hii iko kilomita mbili kutoka junction ya KIA na mpaka wa Arusha na Kilimanjaro. Barabara hii inaunganisha barabara kuu ya Arusha – Moshi – Dar es Salaam na barabara ya Arusha kwenda Namanga – Nairobi na inazunguka Mlima Meru. Wale wananchi wote pale walikuwa wameachwa hawana miundombinu ambayo inaeleweka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, si hivyo tu, barabara hii iko kando kando ya hifadhi ya Arusha National Park, barabara hii ikijengwa kwa kiwango cha lami itatusaidia, itaongeza idadi ya watalii ambao wataingia pale Arusha National Park na kuongeza kipato cha Taifa kupitia utalii. Kwa hiyo nimwombe Mheshimiwa Waziri kwenye Mpango huu wa 2020/2021 asiisahau hii barabara, ina umuhimu wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa kweli imefanya kazi nzuri sana katika kuwapa wananchi maji lakini miradi ya maji tumeona inachukua muda mrefu, mingine mpaka Mheshimiwa Waziri anakuja anaingilia kati, anavunja mikataba ile, kwa hiyo usimamizi wa ile mikataba kidogo umekuwa ni tatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwamba huku tunakoelekea tujaribu kubadilisha mfumo, tutumie Force Account kwa sababu nimeona, nimeshuhudia kazi ikifanyika kwa mafanikio makubwa sana kwenye sekta ya afya. Vituo vingi vya afya vimejengwa kwa kutumia Force Account na ile miradi imetekelezwa vizuri kwa haraka haraka bila kupoteza muda na bila kutoa nafasi ya price variation.

Kwa hiyo nisema tu kwamba huku tunakokwenda hasa kwenye eneo la sekta ya maji, tubadilike kidogo tutumie Force Account ambayo ni...

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Pallangyo kwa mchango wako.

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi uliyonipa na naunga mkono hoja. (Makofi)