Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii

Hon. Saed Ahmed Kubenea

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Ubungo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii

MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nichangie jioni ya leo. Kwanza nianze mchango wangu kwa kunukuu maneno ya aliyekuwa Waziri Mkuu wa Tisa wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Edward Ngoyai Lowassa, liyoyatoa kwenye Bunge hili tarehe 7 Februari, 2008.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Lowassa alisema, “Bunge hili ndio chombo kikuu cha kusimamia Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kwamba hapa ndipo mahali pekee ambapo tunapaswa kuonesha umahiri wetu na utayari wetu wa kudumisha kwa vitendo demokrasia ya hali ya juu katika Taifa letu.” Mwisho wa kunukuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia mijadala yetu ndani ya Bunge na ukiangalia kazi yetu sisi kama Wabunge unapata shida kwamba Mbunge anasimama ndani ya Bunge anapongeza kwa asilimia mia moja halafu analaumu kwa asilimia mia moja. Anasema tokea mwaka 1967 nchi hii ilikuwa haijawahi kujenga hospitali, lakini imejenga baada ya mwaka 1977. Sasa unauliza hicho chama kilichokuwa kinaongoza hiyo Serikali ni kipi? (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unapata shida ukiangalia, mtu anajaribu kuweka ushabiki wa vyama badala ya kuweka maslahi ya nchi mbele. Kwa hiyo, ni rai yangu tu kwamba sisi Waheshimiwa Wabunge tujikite zaidi kuangalia Taifa letu na maslahi yake badala ya kuangalia ushabiki wa vyama vyetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ibara ya 18 ya Katiba yetu ambayo ni mchango wangu katika Kamati ya Huduma za Jamii, inaeleza wazi kwamba kila mtu anayo haki ya kupata habari na kutoa habari na ni wajibu wa Kikatiba wa kila raia. Sasa Kamati imeleta mapendekezo juu ya uboreshaji wa Kituo cha Television ya Taifa cha TBC. Walisema TBC iboreshwe ili iweze kutoa matangazo yake vizuri na iweze kusikika vizuri. Ni jambo zuri sana na tunaliunga mkono.

Mheshimiwa Naibu Spika, TBC ya sasa hivi siyo chombo cha Umma tena. Kimejaa ushabiki na hakiendeshi mambo yake kwa weledi ambapo upande wa pili wa watu wengine ambao wako ndani ya Bunge hili au wanaunda vyama ambavyo viko ndani ya Bunge hili au kwenye Taifa hili, hawapewi nafasi ya kutosha ya kutoa maoni yao. Sheria zilizopo, Kamati inapendekeza TCRA wasimamie leseni za TV za online na television za kawaida. Ni jambo ambalo binafsi silipingi. Ila kuna shida kidogo. Ukienda upande wa magazeti; na katika hili naomba ni-declare interest kwamba mimi ni Mwandishi wa Habari na mmiliki wa chombo cha habari.

Mheshimiwa Naibu Spika, magazeti katika nchi hii sasa hivi yanapewa leseni ya kuendesha kwa kila mwaka, jambo ambalo limeondoa uwezekano wa wawekezaji wakubwa wenye fedha kuja kuwekeza kwenye nchi, kwa sababu mtu hana uhakika kwamba baada ya leseni yake kumalizika atapata muda wa kupewa leseni nyingine? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yalikuwepo magazeti, yaliyumba kwenye uchumi, lakini wawekezaji wa ndani na nje walikuja kuyachukua wakayanunua, wakayaendesha na sasa yametoa ajira kubwa, yameleta mitambo ya kuchapisha magazeti, yameajiri watu wengi sana Watanzania wako hapa, wamepata kazi. Kwa hiyo, nitoe ushauri kwa Kamati na Serikali kwamba, ile sheria ambayo inatumika angalau kwenye television wanapewa leseni ya miaka mitano. Angalau basi kwenye magazeti wangeweka kipindi cha miaka mitano mpaka kumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye ardhi kuna miaka 33 mpaka miaka 99. Sasa tuangalie kwenye madini sheria zimebadilishwa, mambo haya yamebadilika; ili sasa tuweze kufungua uwanja mpana sana wa watu kupata habari kwa uwazi, kupata habari sahihi na kwa wakati sahihi, ili haki ya kila raia isivurugwe kwa sababu ya sheria tunazotunga hapa Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haki hii ya Kikatiba ni haki ambayo mtu haiombi ni yake amepewa kwa mujibu wa Katiba yetu. Ni muhimu sana haki hiyo ambayo tumepewa kwa msingi wa Katiba yetu ikalindwa na kudumishwa. Tunapata shida leo, tunalaumiwa dunia nzima kwamba Taifa letu haliheshimu uhuru wa watu kujieleza, haliheshimu uhuru wa watu kutoa maoni, haliheshimu uhuru wa watu kutoa habari. Sasa baadaye sisi tunakimbizwa na tuko porini…

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa. NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kubenea, kuna taarifa. Mheshimiwa Stanslaus Mabula.

T A A R I F A

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuokoa muda sitaisoma kanuni husika, lakini nataka nimpe Taarifa mzungumzaji kwamba suala la uhuru wa kujieleza ni suala ambalo liko wazi; na kwa sababu, Serikali ya Awamu ya Tano inasimamia jambo hilo, ndiyo maana rafiki yangu Mheshimiwa Kubenea pamoja na wenzake wakiwemo akina Mheshimiwa Mwambe, Mheshimiwa Komu na wengine ambao sitawataja kwa majina, wameukosa uhuru huo wa kujieleza ndani ya chama chao kufikia hatua ya kusema; na wameambiwa sumu haionjwi kwa kulamba na ulimi. Sasa ni haki ipi ya kujieleza anayoitaka? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka tu nimpe taarifa. Ahsante sana. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kubenea.

MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Naibu Spika, hayo ni majungu tu. Kwa hiyo, taarifa kama hiyo nimemwachia yeye mwenyewe. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haki hizi ambazo tumezizungumza ni haki za kisheria, kama zipo basi zinawezekana zipo kwa pande zote katika nchi. Hata kwenye chama ambacho naye anatoka hizo haki inawezekana zikawa zinavurugwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, jambo la muhimu ni kwamba tumekubaliana kwa mujibu wa sheria zetu na Katiba yetu. Mnalaumiwa sana na yeye anajua kwamba leo ukienda kwenye mitandao ya kijamii, ukienda kwenye ripoti mbalimbali za Amnesty International, World Bank, IMF, wanatulaumu na tunanyimwa misaada kwa sababu ya kuzuia hizi haki. Sasa hili jambo siyo geni, linafahamika na kila mmoja. Rai yangu, kwa nini tunakaa kwenye pori tunakimbizwa na simba, badala ya kurukia faru anaweza kukuokoa unaenda kurukia swala, anakuua? Simba anachukua wewe na swala pamoja. Tusifike huko.

Mheshimiwa Naibu Spika, vyombo vya habari Tanzania vinapita katika wakati mgumu sana. Vyombo vya habari havipati matangazo kutoka Serikalini, vinabaguliwa hasa vile vya binafsi, kuna urasimu mkubwa wa kutoa habari hata ndani ya Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wewe ni shahidi kwamba baadhi ya mijadala inayofanyika humu ndani haichukuliwi na vyombo vya habari. Kwa hiyo, sisi badala ya kwenda mbele sana, miaka 100 mbele, tunarudi nyuma miaka 50 iliyopita. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nakushukuru sana. Ahsante sana, Mungu akubariki. (Makofi)