Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Dr. Jasson Samson Rweikiza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Nipende kusema kwamba Serikali ya CCM inafanya vizuri kwenye eneo la elimu au Sekta ya Elimu kuna mafanikio makubwa sana tumeyapata kila mtu anayajua, lakini kwa vile kuna watu ambao wanajifanya hawayajui ni bora nirudie kidogo kwa ufupi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, leo kila Kata ina shule ya sekondari, nyingine mbili, nyingine tatu Kata moja. Kila Kijiji kina shule ya msingi, haya ni mafanikio makubwa; vyuo vya elimu ya juu mwaka 2005 kila mwaka tulidahili wanafunzi 36,000m leo tunadahili wanafunzi 150,000 vyuo vya elimu ya juum haya ni mafanikio makubwa. Leo tumesema elimu bure kuanzia darasa la kwanza hadi la kumi na mbilim haya ni mafanikio makubwa. Niipongeze Serikali, Wizara ya Elimu na CCM kwa ujumla, kazi nzuri, tumeweka misingi mizuri katika kuboresha elimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini bado kuna kazi ya kufanya, tuboreshe, tumeweka misingi mizuri sasa tuiboreshe. Shule binafsi zinafanya vizuri sana wamesema wenzangu jana hapa na mimi ni mmoja wa wamiliki wa shule binafsi, nitangaze maslahi, lakini shule binafsi zinafanya kazi nzuri sana. Niishauri Wizara isaidie shule hizi za binafsi, isizione kama zinafanya dhambi au kosa, zione kama ni mshirika katika kutoa elimu nzuri kusaidia kuelimisha Watanzania. Kwa hiyo, haya mambo ya ada elekezi wamesema Wabunge wengi, nisirudie, hayana maana, tuwaachie wenye shule wafanye shughuli zile, watoe elimu bora, ndio wanaoujua mzigo wanaobeba, mambo ya kupaka mabasi rangi ya njano tuachane nayo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, maana yake tusiwape masharti magumu na yakiwa magumu watashindwa, tutashindwa na mimi nikiwemo, tuwawezeshe ili tuweze kufanya kazi nzuri tuboreshe elimu. Kuhusu kodi wamesema Wabunge hapa kuna mzigo wa kodi haubebeki, watashindwa, tutashindwa kutoa elimu nzuri ambayo kwa kweli ndiyo msingi mzuri wa maendeleo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, elimu ni kila kitu amesema Mbunge Mheshimiwa Mbatia, elimu ndio roho ya Taifa, ni kweli na mimi naungana naye elimu ndiyo roho ya Taifa, tushirikiane katika kuboresha elimu. Shule binafsi mwaka jana kidato cha nne katika wanafunzi 100 bora, wa kwanza wa pili mpaka wa 100, wanafunzi 97 wametoka shule binafsi. Serikali ni watoto watatu, hawa utawabeza kweli? Sasa hapa ni kuwapunguzia mzigo wa kodi na mzigo wa masharti, maana watashindwa na tutadidimiza elimu, tutadidimiza maendeleo ya Taifa hili. Nasema tuboreshe elimu, tupambane, tusonge mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pale Bukoba Vijijini tuna Sekondari kama nilivyosema za Kata, za wananchi na nyingine 31, lakini hatuna Sekondari ya juu, A Level, hata moja. Imeainishwa moja ya Mahoro Secondary School miaka mingi, lakini hakuna kilichofanyika. Niiombe Wizara, hii shule nayo iboreshwe ipate madarasa ya Form Five na Form Six ili hawa vijana kutoka shule 31 hizi waende kupata elimu pale, elimu ya A Level, tuzidi kupiga hatua twende mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Awamu ya Nne ilikazania sana ujenzi wa maabara, jambo zuri sana. Tukajenga maabara kila shule ina majengo ya maabara, lakini hayajakamilika! Sasa naona mkazo umepungua pale, yale majengo mengine yamefika nusu, mengine kwenye linta pale, mengine yameezekwa, mengine hayajakamilika! Tusiyaache haya, yatabomoka, tumechanga pesa kwa tabu sana; kila mwananchi amechangia, hata mimi nimechangia hela nyingi sana kwenye majengo haya ya maabara, tusiyaache yakaporomoka.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara itafute namna ya kusaidia kwa kusaidiana na wananchi hawa waliozijenga hizi maabara zikamilike, ziwe nyumba kamili, ziwekwe vifaa vya sayansi, zitumike kama ilivyokusudiwa; ndiyo maendeleo yenyewe ya elimu kila shule iwe na maabara iliyokamilika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tuko kwenye kazi kubwa ya kuhakikisha kila shule inakuwa na madawati, shule za msingi na sekondari zina upungufu mkubwa sana wa madawati. Kazi inafanyika nishukuru, nimeona hapa katika taarifa Wizara ya Maliasili na Utalii imesema itatoa mchango wa madawati 168,500 nawapongeza, lakini hayatoshi, waongeze kwa sababu, pale nasikia kuna shilingi bilioni sita kwenye Wizara hiyo ya Maliasili na Utalii kwa ajili ya kusaidia jamii. Hizo shilingi bilioni sita ziende kwenye madawati, ndiyo jamii yenyewe na Wizara nyingine zifanye ziige mfano wa Wizara ya Maliasili na Utalii na taasisi nyingine ziige mfano huu, kama Bunge hili limetoa shilingi bilioni sita kwenye madawati na wengine waige mfano huo, ili baada ya muda mfupi madawati yatoshe, vijana hawa wasome katika mazingira mazuri, wasikae chini kwenye vumbi, wakae kwenye madawati ili waweze kusoma vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nizungumzie Walimu wa Shule za Msingi na Sekondari, kwangu mimi wana madai mengi sana, mafao yao hawalipwi. Mwalimu anahamishwa kituo anaambiwa nenda utalipwa baadaye! Anakaa miaka miwili au mitatu hajalipwa! Hili muliangalie wapate mafao yao. Mwalimu anapandishwa daraja haongezwi mshahara!
Mheshimiwa Naibu Spika, nina Mwalimu mmoja pale amekaa miaka 16 hajapanda daraja, tangu ameajiriwa hadi leo miaka 16, hajapanda daraja! Hajapewa warning kwamba, haendi kazini, anafanya kazi vizuri, miaka 16 hajapanda daraja! Mnamkatisha tamaa, hawezi kufundisha vizuri! Walimu waangaliwe, wapewe motisha inayotakiwa ili waweze kufanya kazi vizuri. Hawa ndiyo wanaotoa elimu, ndiyo wafundishaji, ndiyo wasimamiaji wa sekta nzima ya elimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho nizungumzie suala la juzi la wanafunzi wa Saint Joseph, wale karibu 500. Nasema hawa wasaidiwe wasifukuzwe, 55 ni wengi. Halafu wamekuwa admitted pale wamedahiliwa kwa vigezo vilivyokuwepo! TCU hata kama walikosea, lakini makosa yao siyo makubwa kiasi hicho. Kwa sababu, kama tunasema mtu ana D nne, wamesoma Certificate wakapanda Diploma, sasa wanafanya Degree; ndivyo hata CBE inavyofanya. CBE mtu anaingia ametoka Form Four ana D tatu, anasoma Certificate anamaliza, anaingia Diploma anamaliza, si anaingia Degree, kwa nini hawa watendewe tofauti? Wasaidiwe wapate msaada. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mbona tulichukua UPE miaka ya 70, walikuwa darasa la saba, wakapata mafunzo ya miezi mitatu wakawa Walimu wa UPE, mpaka leo ni Walimu wanafundisha shuleni. Baadaye tukachukua hawa vijana wa Form Six, wanaitwa Voda Faster sijui, wakapewa miezi mitatu kozi ya Ualimu, hadi leo ni Walimu wanafundisha! Sembuse hawa ambao wamefaulu vizuri D nne! Wameingia kwenye Certificate wamemaliza, wamesoma Dilpoma, leo wanasoma Degree mnawafukuza! Msiwafukuze, tumelipa hela nyingi Watanzania kwenye kodi zetu, wamesoma miaka mitatu, miaka minne na wengine miaka miwili. Wasaidiwe warudi chuoni wamalize ili wasaidie kupunguza pengo la upungufu wa Walimu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na naunga mkono hoja.