Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama Kuhusu Shughuli za Kamati Kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama Kuhusu Shughuli za Kamati Kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua nafasi hii kukushukuru wewe binafsi kwa kuniwezesha kupata nafasi ya kuweza kuchangia katika hizi hotuba za Wenyeviti wetu wawili wa Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama pamoja na Wizara ya Nishati na Wizara ya Madini.

Mheshimiwa Spika, nianze na hotuba ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama. Hotuba hii imeeleza vizuri kazi mbalimbali ambazo zimekuwa zikifanyika kwa Wizara mbili ambazo tunazisimamia, Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa na Wizara ya Mambo ya Ndani pamoja na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Spika, nchi yoyote duniani ambayo imeendelea kiuchumi ina tabia ya kuwa na vyombo vya ulinzi na usalama ambavyo ni imara. Kwa maana hiyo tunapotaka kujenga Tanzania ya Viwanda, ni muhimu pia kuwa na vyombo vya ulinzi na usalama ambavyo pia vimewekeza katika masuala mtambuka ya silaha za kivita zikiwemo ndege, meli, mizinga na vitu vingine vyote ambavyo vinahusiana na habari ya ulinzi na usalama.

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo, naishauri Serikali iendelee kuvipatia vyombo vyetu vya ulinzi na usalama bajeti inayostahili ili kusudi mashirika yetu ya Nyumbu na Mzinga yaweze kuwekeza zaidi katika miundombinu ya uboreshaji silaha na nyenzo za kivita ili kuweza kulihami Taifa letu ambalo lina rasilimali nyingi ambazo Mwenyezi Mungu ametujalia kuwanazo.

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo, kutokana na utajiri wa nchi yetu ulivyo mkubwa nina uhakika kwamba tunao maadui wa kutosha kutoka nje na ndani ya nchi yetu. Kwa hiyo, tusipokuwa na vyombo madhubuti tunaweza tukajikuta ujenzi wa uchumi wetu ukawa sasa unapata pingamizi mbalimbali. Kwa maana hiyo, naishauri tu Serikali iwekeze vyakutosha katika vyombo hivi.

Mheshimiwa Spika, pia nalipongeza Jeshi la Wananchi wa Tanzania pamoja na Jeshi la Kujenga Taifa kwa kuendelea na kuwa na mpango madhubuti wa kuweza kuwachukua vijana wetu na kuwajengea uzalendo katika makambi mbalimbali na pia Shirika letu la SUMA kwa kazi nzuri ambazo imekuwa ikizifanya.

Mheshimiwa Spika, naipongeza JKT kwa kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa uzio wa Mererani na kazi nyingine ambazo Jeshi letu hili limekuwa likizifanya. Naiomba tu kwamba Serikali iendelee kuiunga mkono inavyostahili.

Mheshimiwa Spika, aidha, nalipongeza Jeshi la Polisi kwa kazi nzuri ya ulinzi wa raia na mali zao na kwa vyovyote vile tunashukuru kwa sababu matukio ya uhalifu yamepungua katika nchi yetu. Kwa hiyo, naomba tu kwamba vyombo vyetu hivi vya ulinzi na usalama viendelee kuungwa mkono kwa kupewa pesa kwa ajili ya kujenga nyumba za maaskari wetu na kwa maana hiyo tuweze kuwarahisisha maisha Askari wetu.

Mheshimiwa Spika, Jeshi la Magereza limekuwa ni chombo madhubuti ambacho kimekuwa kikisaidia kuwarekebisha Watanzania wanaokuwa na matatizo ya kiuhalifu. Kwa maana hiyo, naomba tu Serikali iendelee kulisaidia jeshi hili katika kuhakikisha kwamba msongamano katika Magereza unapungua na ikiwezekana Serikali itoe pesa zaidi kuweza kujenga Magereza mengi zaidi ili kuweza kuwapa nafasi watu hawa, pamoja na kwamba ni wavunjifu wa sheria na wakosaji, lakini ni muhimu wakapatiwa matunzo mazuri wanapokuwa katika kipindi chao cha kutumikia adhabu zao.

Mheshimiwa Spika, nchi yetu imekuwa na zoezi la kuwapatia raia wa nchi hii vitambulisho vya Taifa. Zoezi hili linafanywa na Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), lakini tumeshuhudia katika siku za karibuni kwamba mamlaka hii imekuwa na changamoto kubwa ya kushindwa ku-cope na mahitaji ya Watanzania. Watanzania walio wengi hawajapata vitambulisho hivyo. Tatizo kubwa linaonekana ni fedha. Kwa hiyo, naiomba tu Serikali isaidie mamlaka hii ili iweze kusaidia kutoa vitambulisho vya kutosha na wananchi wetu waweze kutambulika kama raia wa nchi hii.

Mheshimiwa Spika, nije kwenye Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Naipongeza Wizara hii kwa sababu imekuwa ni kiunganishi kati ya Taifa letu na Mataifa mengine ya nje na tumeona ukuaji wa diplomasia ya uchumi, watu kutoka Mataifa mbalimbali wamekuwa wakija katika Taifa letu na kuwekeza na kwa maana hiyo kuchangia ukuaji mkubwa kabisa wa uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naiomba Serikali iendelee kutoa pesa kwa ajili ya miradi ya maendeleo katika Balozi zetu mbalimbali duniani ambapo tumeshuhudia wakati mwingine Serikali ikiingia gharama kubwa kupanga majengo kwenye Balozi zetu huko nje. Naomba Serikali iwekeze zaidi katika ujenzi wa nyumba na Ofisi ya Kibalozi huko Mataifa ya nje.

Mheshimiwa Spika, nichangie katika Wizara ya Nishati. Naipongeza sana Serikali kwa namna ambavyo imeendelea kuongeza miradi mikubwa ya uzalishaji wa umeme ikiwemo Kinyerezi I, II, III pamoja na mradi mkubwa wa Julius Nyerere Hydroelectrical Project ambao unajengwa ambao utakuwa ni mkombozi wa matatizo ya umeme hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaamini wazi kabisa kwamba ongezeko la Megawatt 2,115 itakuwa ni ingizo kubwa ambalo litasaidia sana katika kulifanya Shirika la Umeme (TANESCO) pamoja na Miradi ya REA kwenda katika maeneo mbalimbali nchini na Watanzania wengi watanufaika kwa kuwa na umeme ambao utakuwa na bei nafuu; na kwa maana hiyo Tanzania ya Viwanda itawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia naipongeza Serikali yetu kwa kuja na Mpango Mkakati na kubadilisha Sheria za Madini ili kuhakikisha kwamba Taifa letu linanufaika. Naipongeza Serikali kwa kuingia mkataba mpya na Kampuni ya Barrick ambako sasa imeanzishwa Kampuni ya Twiga ambayo Serikali yetu sasa itakuwa na hisa za asilimia 16 na manufaa yake tutayaona muda siyo mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashauri kwamba hata Makampuni mengine ambayo yamewekeza katika madini Serikali...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana. Mheshimiwa Augustine Manyanda Masele.

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na ninaomba kuunga mkono hoja. Ahsante.