Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge na Utawala na Serikali za Mitaa pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo

Hon. Vedasto Edgar Ngombale Mwiru

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge na Utawala na Serikali za Mitaa pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo

MHE. VEDASTO E. NGOMBALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kusema chochote katika michango ya kamati hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze tu kusema kwamba yapo malalamiko kwenye uchaguzi wa Serikali za Mitaa ambayo yanahitaji kufanyiwa kazi na nilitarajia kwamba kwenye taarifa ya kamati basi kuna chochote kingesemwa ili basi kuweka hiki kitu sawasawa. Kwa hiyo, nitake kwamba Serikali ifanyie hili suala kazi, wananchi wanalalamika sana juu ya namna ambavyo uchaguzi umeendeshwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jingine ambalo ningependa niseme ni kwamba zipo Halmashauri ambazo mpaka leo bado hazijapeleka michango ya makato kwa malipo ya Waheshimiwa Madiwani na Serikali isipokuwa makini tutaenda kwenye kumaliza wakati wetu, kwa baadhi ya halmashauri nyingine watashindwa kulipa viinua mgongo vya Waheshimiwa Madiwani. Kwa hiyo, ni jukumu la Serikali kuhakikisha kwamba kila halmashauri inapeka hiyo michango ili basi Waheshimiwa Madiwani waweze kupata stahiki zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala zima la TASAF. Ripoti ya Kamati inaonesha kwamba wafadhili wanatoa fedha lakini Serikali imeonesha kusuasua kutotoa pesa sawa sawa. Kwa hiyo, nachukua nafasi hii kuitaka Serikali ichangie ipasavyo ili basi michango hii iende kwa zile kaya masikini ziendelee kupata kama ilivyokuwa katika utaratibu wa kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la TARURA. TARURA inafanya kazi nzuri na mwaka huu mvua ni nyingi, kwa hiyo barabara nyingi zimeharibika. Kwa hiyo, naiomba Serikali ikubali ushauri wa Waheshimiwa Wabunge wa kuongeza asilimia ya mgawanyo. Kwa kupendekeza, TARURA ipate sasa asilimia 40 ili iweze kushughulikia ipasavyo barabara za mijini na vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepitisha sheria ya asilimia 10 ya mapato ya ndani iende kwa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu. Zipo Halmashauri zimeanza kutopeleka hizo asilimia 10 kama zinavyotakiwa na sheria na hivyo kuanza kuzalisha madeni. Kwa hiyo, nachukua nafasi hii kuzitaka Halmashauri zote zipeleke ipasavyo hizo asilimia 10 ili basi michango ile iende sawa sawa kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna hii asilimia mbili inayokwenda kwa watu wenye ulemavu. Watu wenye ulemavu wana chagamoto; ukisema waandae makundi ili wakopeshe, wengine wanakosa haki. Kwa mfano, mtu mwenye ulemavu wa akili unamweka katika kundi gani? Napendekeza kwamba watu wenye ulemavu wa aina hiyo, basi wazazi wao washirikishwe kwenye makundi hayo ili basi nao waweze kupata stahiki zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vinginevyo bado inaonekana kuna uwezekano mkubwa kwamba asilimia mbili inayotakiwa kwenda kwa watu wenye ulemavu isiende kwao kwa sababu vikundi vinavyotengenezwa vya watu wenye ulemavu ni vichache sana. Serikali iangalie utaratibu mwingine wa kuweza kuangalia namna gani itawapatia hizi fedha watu wenye ulemavu, ikiwezekana waangalie pia mahitaji yale muhimu ya watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nashauri Serikali sasa ilete Muswada wa Sheria kama ilivyozungumzwa kwenye Taarifa ya Kamati kwa ajili ya kusaidia Shirika la Masoko la Kariakoo lifanye kazi sawa sawa. Shirika hili ni la siku nyingi lakini inaonekana lina upungufu wa sheria na linashindwa kufanya kazi yake sawa sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, nizungumzie suala la pale Jimboni kwangu, Njinjo. Mkoa wa Lindi na Wilaya ya Kilwa na hasa Jimbo la Kilwa Kaskazini tumepatwa na kadhia ya mafuriko, hali ni mbaya sana. Ninavyozungumza, zaidi ya watu 26 wamepoteza maisha ikiwemo watu saba wa familia moja na watu sita wa familia nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninavyozungumza, katika zile Kata mbili kuna shule nne zimeharibiwa kabisa. Nachukua nafasi hii kuomba wenzangu wa TAMISEMI washirikiane na watu wa maafa wa Waziri Mkuu waangalie namna gani ya kuwasaidia wale watu. Isitoshe kwamba zaidi ya watu 10,000 wamekosa makazi na hivyo kulazimika kupewa viwanja kwa ajili ya kupata makazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii pia kuipongeza Serikali kwa namna ambavyo imeshughulikia tatizo hili. Naiomba huko ambako wananchi wanakwenda kupewa viwanja, basi Serikali ihakikishe haraka iwezekanavyo inapeleka huduma muhimu ikiwepo shule, miundombinu ya barabara, umeme na maji ili wale wananchi waweze kuishi maisha kama walivyokuwa wanaishi mwanzoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nichukue nafasi hii kuwaomba Jumuiya za Kimataifa, asasi za kiraia, watu mbalimbali kuchangia watu walioathirika na mafuriko. Ikupendeze, hata Bunge lako Tukufu, ikiwezekana, ikikupendeza basi nalo lichangie waathirika wa mafuriko katika Wilaya ya Kilwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nichukue nafasi hii kutoa pole kwa waathirika wote ambao wamekutwa na kadhia hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana, ahsante. (Makofi)