Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, ninashukuru sana kwa nafasi na vile kwa muda mfupi huu kuweza kuchangia na mimi kidogo katika taarifa ya hao Wenyeviti wawili; Mwenyekiti wa Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii na Mwenyekiti wa Kilimo, Mifugo na Maji.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kuwapongeza Wenyeviti hawa wote wawili, hoja zao ni nzuri. Niwapongeze Kamati yangu ya Kilimo, Mifugo na Maji kwa muendelezo wao uleule wakuendelea kutusimamia vizuri sana sisi kama Wizara ya Mifugo na Uvuvi na kuwezesha kutekeleza majukumu yetu vizuri sana hapa Bungeni lakini na maeneo mengine.

Mheshimiwa Spika, kwa nafasi hii ya muda mfupi napenda kusemea baadhi ya maeneo machache kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge wametupongeza sana kwa jitihada tulizozifanya za uwekezaji wa viwanda hapa nchini lakini wakaona kwamba kama vile tunaenda kwa spidi ndogo sana katika kuboresha mifugo yenyewe na katika kuhakikisha kwamba mifugo hii ipo salama na inazalishwa na inakua vizuri.

Mheshimiwa Spika, tumefanya mambo makubwa pia ya kuhakikisha kwamba tunapambana na magonjwa. Sasa hivi utakubaliana na mimi kwamba nchi nzima sasa hivi katika kipindi tu hiki cha nusu mwaka tayari tunakamilisha ukarabati wa majosho 449. Kama hiyo haitoshi tumepeleka dawa za kuogesha kwenye Wilaya zote kwenye majosho yote 1,725 ambayo tayari nchi nzima wanaogesha mifugo kwa ruzuku ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama hiyo haitoshi tumefanya mambo mengi kama ambavyo yamezungumzwa hapa na Waheshimiwa Wabunge. Kwa mfano, kuongezeka kwa maeneo ya malisho, leo maeneo yetu yameongezeka kutoka 1,400,000 mpaka leo tumefikia maeneo yaliyotengwa hekta 2,800,000. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na bado Serikali ikaenda mbali zaidi ikamega mpaka mashamba yake ya Serikali kwa ajili ya kuwagawia wafugaji na wakulima kwenye vijini 920 na imeelezwa kwenye kumega misitu na mapori ya akiba, imeelezwa kwenye kumega mashamba mpaka ya Serikali ya NARCO na mashamba mengine ya taasisi zetu. Hizi zote ni jitihada za kuhakikisha kwamba wafugaji wa nchi hii wanapata maeneo mazuri ya kufugia na wanafuga vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala la uvuvi wa bahari kuu. Waheshimiwa Wabunge katika hili msiwe na mashaka, Serikali ya Awamu ya Tano imejipanga vizuri kufanya kazi hiyo na ndiyo maana Shirika la TAFICO tayari limeshafufuliwa, mpango wa biashara umeshaandaliwa wa kununua meli na kuanza shughuli za uvuvi wa bahari kuu. Na kama hiyo haitoshi bandari ya uvuvi tayari upembuzi yakinifu na usanifu wa kina unaendelea na tupo kwenye hatua za mwisho na tayari tuende kwenye hatua za kujenga.

Mheshimiwa Spika, kama hiyo haitoshi, tayari Sheria ya Mamlaka ya Uvuvi Na. 1 ya Mwaka 1998 tumeifuta ili kuleta na kuwavutia watu mbalimbali waliokua wanakwazwa na sheria kuja kuwekeza katika uvuvi wa Bahari Kuu katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Spika, kuna mambo ya makokoro yataisha lini. Kuna changamoto, bidhaa za nyuzi hizi zinapoingia nchini zinakuwa ni halali lakini zinapokuja kutengenezwa, wavuvi wetu wanapokuja kusuka nyavu sasa wanaweza kusuka kokoro; lakini nyavu inapoingia nchini ni halali kama nyavu tu (raw material kwa ajili ya kutengeneza bidhaa. Kwa hiyo, hiyo ni tatizo kubwa na hili limetusababisha Wizara ya Mifugo na Uvuvi kukaa na wenzetu wa TBS pamoja watafiti wetu wa TAFIRI ili kutafuta namna bora ya kusimamia hili eneo. Kwa hiyo, tuna imani hivyo tutafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tatizo lingine la hizi nyavu ni kwamba kila maeneo yana nyavu tofauti ya kuvulia kulingana na aina ya samaki waliopo kwenye eneo hilo. Samaki waliopo Bahari ya Hindi ni tofauti na samaki waliopo Ziwa Tanganyika, ni tofauti na samaki waliopo Ziwa Victoria, kwa hiyo hata nyavu zake nazo pia ni tofauti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hapa kuna maneno mengine yalizungumzwa ya kwamba wananchi wanahitaji maji, hawahitaji ndege. Waheshimiwa Wabunge hivi hayo maji mnaenda kuyajenga bila ya kuwa na fedha? Miundombinu ya ndege inaponunuliwa nchini inawezesha uchumi kukua, mazao yetu ya samaki leo, samaki atavuliwa saa 2 Ziwa Victoria anaenda kuliwa saa 4 Zimbabwe. Samaki atavuliwa hapa Dar es Salaam saa 12 asubuhi kufikia jioni analiwa India; huu ndio uchumi wa nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa unapozungumza kwa ajili ya kujifurahisha kwamba eti wananchi wanahitaji maji hawahitaji ndege, huwezi ukaondoa mahitaji muhimu ya wananchi katika kupatikana kwa ndege. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo hii Ziwa Victoria tunavua kila siku tani 250, kwa hiyo unahitaji ndege za kubeba samaki tani 250 kila siku. Leo samaki wetu hao wanabebwa Uganda, samaki wetu hao wanabebwa Kenya, tungekuwa na ndege zetu – na ndiyo maana Waziri wa Uchukuzi nimemwambia piga, garagaza, ua lazima tununue ndege zetu za kusafirisha mazao yetu. Tani 250 kwa maji moja, hujaenda Tanganyika, hujaenda Bahari ya Hindi.

Mheshimiwa Spika, lakini kama hiyo haitoshi, la mwisho labda ni hili Mawaziri, kwa sababu yanazungumzwa maneno hapa mengine ni vizuri kutolewa clarification. Mtu anasema tu hapa Mawaziri ambao ni wasimamizi wa sera wanafanya mambo ya operation, nadhani alikuwa anazungumza kutofautisha operational na oversight. Lakini tangu lini wewe mtu wa oversight utafanya shughuli zako za oversight bila kwenda kwenye maeneo unayoyasimamia. Ni tangu lini wewe msimamizi utafanya ukiwa ndani mambo ya kisera, unasema nafanya mambo ya kisera unajifungia chumbani, utashindwa kwenda kwenye maeneo ya uvuvi, utashindwa kuonana na wavuvi, utashindwa kwenda kuwaona wafugaji, utashindwa kwenda kwenye maeneo eti wewe unatunga sera. Sera hizi utazitungia ukiwa wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge, ni vizuri kama ukiwa huna la kuchangia unaacha tu, sio kusimama hapa na kupoteza muda wa nafasi na muda wako. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Waziri nakuongeza dakika tano. (MakofiVigelegele)

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa ongezeko hilo. Mheshimiwa Spika nataka niweke mambo vizuri hapa; kuna suala la oversight function, kuna suala la operation function. Kama wewe ni oversight utawezaje kuwa oversight bila kukaa na hawa operational? Kama wewe ni oversight utawezaje kufanya kazi yako ya oversight function bila kwenda kwenye operational sight? Haiwezekani! Ni mambo ambayo unazungumza kama huyajui au kama umeambiwa nje unakuja nayo hapa Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninachotaka niwaambie, Serikali ya Awamu ya Tano kama mtu yeyote anatafuta eti kutupotezea uelekeo…

SPIKA: Mheshimiwa Mchungaji Msigwa hoi kabisa.

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Kama mtu yeyote anatafuta kutupoteza uelekeo, kama mtu yeyote anatafuta eti kutukatisha tamaa Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ilishakataa katakata kukatishwa tamaa na mtu yeyote yule. Serikali inayoongozwa na Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ilishakataa katakata kukatishwa tamaa na mtu yeyote. (Makofi/Vigelegele)

MHE. MCH. PETER S. MSIGWA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

WABUNGE FULANI: Aaaaa!

SPIKA: Mheshimiwa Waziri, endelea.

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, ninachotaka kukieleza hapa ni kwamba watu wajue katika taarifa hii ya Kamati kuna mambo makubwa yaliyoelezwa hapa. Nilitegemea Wabunge wakayaona hayo. Leo mapato ya uvuvi…

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, tusikilizane, naomba tusikilizane; mlipokuwa mnawapiga Mawaziri hapa wala hawakusema kitu…

WABUNGE FULANI: Ndiooo!

SPIKA: Sasa wanapojibu naomba na ninyi mtulie, ndiyo kuwa na ngozi ngumu, tulieni. Mheshimiwa Waziri, endelea.

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, Kamati hii imeongea mambo mazuri sana ambayo leo wastani wa makusanyo ya Wizara ya Sekta ya Mifugo na Uvuvi yalikuwa bilioni 21, leo yamefika bilioni 72. Fedha hizi zimeenda kwenye elimu, fedha hizi zimeenda kwenye maji, fedha hizi zimeenda kujenga miundombinu ya maji ya wananchi. Mauzo yetu ya samaki nje ya nchi yameongezeka kutoka bilioni 379 hadi bilioni 691; hiyo ni Serikali ya Dkt. Magufuli imeyafanya hayo. Tulitegemea Mbunge badala ya kwenda kwenye vitu vidogovidogo hivi angesema mambo haya makubwa yaliyofanyika ya kitaifa.

Mheshimiwa Spika, tumepunguza manunuzi ya samaki nje ya nchi. tulikuwa tunanunua samaki nje ya nchi kwa thamani ya bilioni 56 kwa mwaka. Leo tunafika hapa mwaka mzima manunuzi yetu ya samaki nje ya nchi ni milioni 37, fedha hizo ziko hapa kwa Watanzania, bilioni 56 zinaliwa na Watanzania leo, zinaliwa na wavuvi hawa, ni Serikali ya Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, nataka niwathibitishie Watanzania wote na Wabunge kwamba Serikali ya Awamu ya Tano tumejipanga na tutahakikisha kwamba kero zote za Watanzania tunazishughulikia. Tutaenda site moja baada ya nyingine, tutaenda maeneo yote kuhakikisha Tanzania na matatizo ya Watanzania yanaokolewa, kuhakikisha kwamba tunafuta, kuhakikisha kwamba Watanzania ambao wamelia muda mrefu tunafuta machozi yao, tunakwenda kupangusa machozi ya Watanzania wote walioteseka na kunyanyaswa muda mrefu, na tupo kwa ajili ya kufanya hiyo kazi. (Makofi)