Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuchangia siku siku ya leo.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote, nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya. Pia nipongeze taarifa za Kamati zote mbili; mimi ni mjumbe wa Kamati ya Kilimo, Maji na Mifugo, nimpongeze Mwenyekiti wetu na Kamati nzima kwa kazi kubwa na nzuri na ushirikiano mzuri na mkubwa ambao unafanywa na Wizara ambao tunazisimamia. Pia nishukuru Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa taarifa nzuri na kazi kubwa ambayo wamefanya na mabadiliko yote tumeweza kuyaona. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nichangie katika badhi ya maeneo. Nikianza na Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utlii; naomba nitoe maoni machache ambayo yangeweza kuboresha shughuli, najua Kamati itaweza kuyafanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, kuna sheria mbalimbali ambazo tumepitia na tumefanya semina mbalimbali pamoja na Kamati hiyo, sheria ambazo zinakinzana kwenye sekta nzima ya ardhi, maliasili na utalii; kuna sheria za maliasili, lakini pia kuna sheria za ardhi na sheria za mifugo. Ziko sheria tumezibainisha ambazo zinakinzana na hiyo ndiyo unaleta changmoto kubwa na ndiyo inasababisha migogoro mingi. Tukiweza kuziweka vizuri sheria hizi na zisiwe zinakinzana naamini migogoro mingi itakuwa imepungua.

Mheshimiwa Spika, lakini pia, napendekeza kwa upande wa National Haousing, sehemu kubwa siku za nyuma walikuwa kazi zao nyingi wanazi-outsource. Ni vizuri kila jambo wangekuwa wanafanya in house, kwa mfano kutengeneza madirisha ya aluminum wangekuwa na kiwanda chao wenyewe, kama ni kufyatua blocks wafyatue wenyewe yaani shughuli nyingi ziwe in house badala ya kuwa outsource ambapo gharama inakuwa kubwa na faida ndogo. Kwa hiyo, wakifanya kazi nyingi bei za nyumba zitapungua sana na wataweza kuwauzia Watanzania nyumba ambazo zitakuwa na gharama nafuu. Kwa hiyo, hilo jambo ni muhimu kwa upande wa National Housing. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwa upande wa migogoro mbalimbali ya ardhi, tungeomba sasa Kamati itusaidie. Yale yote ambayo Tume iliyoundwa na Mheshimiwa Rais wetu kumaliza ule mgogoro basi yafanyiwe kazi sasa na vile vijiji vitangazwe rasmi ili ile hofu na wananchi kuishi bila kujua hatma yao haswa katika vijiji kwa mfano Jimbo la Babati kuna Vijiji vya Ayamango, Gedamar, Gedejabong na eneo lile ambalo lina tatizo kubwa la WMA basi ingewekwa wazi ili kila mmoja ajue ni nini kimetokea. Jambo hilo likifanyiwa kazi naamini kabisa kwamba migogoro mingi itaisha. Pia kwenye Land Use Plan basi tuweze kuangalia ushirikishwaji katika maeneo mengi ya sekta mbalimbali ili ziendane kwa pamoja.

Mheshimiwa Spika, lakini pia, napendekeza kamati itusaidie, matumizi ya ardhi yanabadilika kila siku na hasa leo tunaangalia Mji kama wa Dodoma, kuna mashamba yako ndani ya Mji huu wa Dodoma hasa ya zabibu na nchi nyingi duniani zinakuwa na mashamba ndani ya miji. Ni vizuri hii sheria ikawekwa la sivyo tutajikuta mashamba yetu ya zazibu ambayo ni eneo pekee Tanzania ambalo tunaweza kupanda zabibu ya uhakika na ambayo ina sifa kubwa duniani itatoweka. Kwa hiyo, jambo hilo pia lizingatiwe, Land Use Plan kwenye miji pia izingatie kulinda mashamba mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikija pia kwenye utalii, naomba Serikali kwa kupitia Kamati ishauri, najua maoni hayo tuliwaletea na mmeyafanyia kazi, lakini kwenye hii bajeti tunayoelekea maeneo mengi, hasa katika maeneo ya hifadhi ambayo yanaingiza fedha za kutosha ambapo zinalisha hizi hifadhi nyingine hasa kwa mfano Tarangire, kuna barabara tatu zinazoingia zingetengenezwa. Tumeomba kwa muda mrefu sasa barabara ile ya Minjingu kuingia getini, ile ya Kibawa Tembo kwenda Sangaiwe na ile ya Babati Mji kwenda kule Mamire zote zingetengewa fedha ili kukuza utalii katika sekta hiyo.

Mheshimiwa Spika, pia Kamati iweze kusaidia kuangalia miradi mbalimbali ambayo inachangiwa na hizi hifadhi katika jamii isiwe miradi ambayo kwa mfano ya kujenga shule au ya kujenga zahanati na kadhalika lakini waangalie mahali ambapo wanaweza kuchangia miradi ambayo itanyanyua uchumi wa watu ili watu wakishakuwa na uchumi mzuri wao wenyewe watajenga hizo zahanati na shule. Kwa hiyo, iwe ni miradi ambayo itanufaisha wananchi wanaokaa jirani na hizi hifadhi. Pia, nipongeze kwamba mahusiano sasa yamekuwa mazuri sana baina ya hifadhi nyingi na wananchi wanaozunguka na usimamizi umeendelea kuwa mzuri.

Mheshimiwa Spika, nikirudi sasa kwenye sekta ya kilimo, niipongeze Wizara ya Kilimo na Wizara ya Mifugo kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wanafanya, lakini pia Wizara ya Maji ambayo Kamati yetu inasimamia. Nishukuru kwamba wamekubali lile ombi letu la kufanya miradi mingi kwa kupitia Force Account. Tumeona Force Account imekuwa na mafanikio makubwa katika sekta ya elimu na sekta ya afya. Sasa hivyohivyo tukitumia kwenye sekta hii ya maji, nina uhakika kwamba tutaona mafanikio makubwa zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi letu kwa kupitia Kamati ni Serikali wakati tunapokuja kwenye bajeti iweze kuondoa kodi kwenye mitambo ya kuchimba maji, mitambo ya kuchimba mabwawa, ili badala ya Serikali kutegemea bajeti yetu ndogo basi sekta binafsi iweze kufanya kazi hiyo. Leo hii bidhaa nyingi ambazo zinatokana na sekta ya kilimo hazina VAT kwa hiyo, hawapati ule msamaha wa capital goods kwa sababu bidhaa zao hazina VAT. Wakiondoa hilo katika sekta ya kilimo watu wengi wataweza kuleta hii mitambo na kutengeneza mabwawa wenyewe na kuanzisha miradi ya umwagiliaji ambayo itakuwa ni kilimo cha uhakika zaidi.

Mheshimiwa Spika, lakini muhimu zaidi ni maoni ambayo pia Kamati imeiomba Serikali na nasisitiza kwamba ilete ile Sheria ya Blue Print Regulatory Reforms mapema kwa sababu bila hiyo sekta nzima hii ya kilimo itaendelea kuwa na changamoto. Tumeainisha kwenye ripoti yetu utaona ada, tozo, ushuru na kodi nyingi kwenye sekta moja tu ndogo ya horticulture hivyohivyo iko katika karibu sekta nzima ya kilimo na mifugo, kuna utitiri wa kodi na tozo na ada mbalimbali ambazo zinafanya bidhaa zetu zinakuwa ghali kuliko bidhaa zinatoka nje. Tunaendelea kuishauri Serikali kwamba ni vizuri bidhaa ambazo tunaagiza kutoka nje kwa mfano matunda na mboga ambazo tuna uwezo wa kuzalisha nchini basi Serikali iweze kuwekeza zaidi. Sehemu kubwa tunachohitaji ni kuwa na mazingira rafiki, siyo lazima Serikali iwekeze fedha, wakiweka mazingira wezeshi basi sekta binafsi itaweza kuchukua fursa hiyo na kuifanyia kazi ili watu wengi zaidi waweze kunufaika na kuzalisha ndani ya nchi na kwa gharama nafuu.

Mheshimiwa Spika, hivyohivyo kwa upande wa mbegu tumeona asilimia 60 ya mbegu tunaagiza kutika nje ya nchi. Ni vizuri sasa Serikali iangalie namna ya kupunguza gharama mbalimbali ambazo zinafanya uzalishaji wa mbegu hizo hapa nchini kuwa wa chini ili tuzalishe wenyewe hapa nchini na fursa hiyo ipo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ni muhimu ni kwamba sekta hii ya kilimo inakua kwa asilimia 4.5 ingawa ni sekta ambayo inaajiri zaidi ya asilimia 80 ya Watanzania lakini kwenye bajeti haipewi umuhimu wake. Tunaomba tuangalie namna ya kuongeza bajeti angalau ifikie asilimia 10. Ndiyo tunakubali kwamba Serikali inasema miradi yote ambayo inatekelezwa mjini iwe ya elimu, afya, maji, barabara, miundombinu, nishati, yote hiyo inachangia kwenye sekta ya kilimo lakini ukichukua budget approved na Bunge na budget disbursed kwa upande wa maendeleo huko vijijini bado haifikii asilimia 10.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ni vizuri ile asilimia 10 ili iweze kufikiwa yote hiyo, tunakubali ni sekta ya kilimo na mifugo kwa mapana yake, ni vizuri budget disbursed ambayo tunapitisha hapa Bungeni, ile approved basi ilingane na asilimia 10 tutaona maendeleo huko kwenye sekta ya kilimo. Kwa sasa hivi bado haijafikia iko kwenye asilimia 8.2, ni vizuri tukahakikisha kwamba hiyo miradi yote tunayosema iko vijijini bajeti hizo ziende kwa sekta zote tutaweza kufanya vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kwa upande wa maji tungeomba Serikali iangalie namna ya kuboresha. Kuna mitambo ya kusafisha maji, water purifiers, wangeweza kuondoa kodi ili gharama za kupata maji safi na salama vijijini iwe ndogo. Pia solar water pumps zikiondolewa kodi watu wengi zaidi watapata maji safi na salama na bajeti kwa upande wa afya ambayo ni zaidi ya shilingi bilioni 30 kwa magonjwa yanayotokana na maji itapungua na watu watakuwa na afya njema na Watanzania wengi wataendelea kupata maji. Serikali inafanya kazi kubwa na nzuri, lakini hizi reforms tunahitaji ziende kwa haraka zaidi kwa wakati mmoja ili tupone haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya hayo, naunga mkono hoja moja kwa moja. (Makofi)