Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika Wizara hii ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi. Kwanza kabisa namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia kuwepo hapa, niishukuru pia familia yangu walitambua umuhimu wa mimi kupata elimu ndiyo maana nikawepo hapa, lakini vile vile naomba nimpongeze Waziri mwenye Wizara husika Mheshimiwa Waziri Ndalichako kwa jitihada zake za kuhakikisha kwamba tunaboresha elimu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naomba nianze kwa kunukuu. Kama tunavyofahamu elimu ni maarifa na maarifa ni maisha. Maana yake jamii ikipata elimu, watoto wakipata elimu ,basi watakuwa na maisha bora. Natambua jitihada za Serikali katika kuboresha elimu tangu uhuru. Kwa mfano, mwaka 1961-1984 kwa falsafa ya Elimu ya Kujitegemea; lakini vile vile Sera ya Elimu mwaka 1995 ambapo Serikali ilikuja na Sera ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi; mwaka 2002-2006 ikaja na MMEM na MMES na mwaka 2014 Sera ya Elimu imeasisiwa, lakini pamoja na jitihada hizo za Serikali bado elimu bora kwa Watanzania na nalenga hasa kundi la watu wenye ulemavu.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimnukuu mtu ambaye ni miongoni wa watu wenye ulemavu ambao wamefanikiwa sana, Bwana Nicolaus James maarufu kwa jina la Nick Vujicic ambaye yeye ni mlemavu kutoka nchini Australia, hana miguu, hana mikono, lakini pamoja na yote hayo mafanikio yake ni makubwa na ni mfano wa kuigwa na walemavu wote duniani kutokana na jitihada zake. Hata hivyo, Bwana Nicolaus James au Nick Vujicic yeye amefanikiwa kutokana na Serikali yake kutambua kwamba kuwa na ulemavu siyo kulemaa, kwa maana hiyo iliboresha miundombinu na kuhakikisha kwamba Bwaba Nicolaus Vujicic anapata elimu, ili elimu ndiyo iwe mtaji katika maisha yake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba sasa nizungumzie changamoto za watu wenye ulemavu na hasa watoto wenye ulemavu kwa hapa nchini Tanzania. Hii sio kwamba kwa nchi hii ya Tanzania tu, ni Afrika yote, lakini kwa sababu mimi ni Mtanzania naomba nizungumzie nchi yetu ya Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumze kwa kusema kwamba; kama familia yangu isingetambua umuhimu wa mimi kupata elimu, leo hii nisingekuwa hapa, lakini walitambua umuhimu wa elimu ndiyo maana leo niko hapa na pengine isingekuwa hivyo, ningekuwa ombaomba mitaani. Kwa maana hiyo, siyo walemavu wote wanaoomba wanapenda, yote hiyo ni kutokana na maisha, ni kutokana na wao kutokupata elimu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kibaya zaidi najiuliza swali; ni kwa nini watoto wengi wenye ulemavu wanatoka katika familia maskini? Hili ndilo ambalo linatukosesha sisi elimu kwa sababu katika familia kama kuna watoto watatu na yupo mtoto mwenye ulemavu, familia itaona ni afadhali iwapeleke watoto wasio na ulemavu ili wakapate elimu na kwa maana hiyo yule mwenye ulemavu anabaki nyumbani. Kwa maana hiyo, huyu ambaye ana ulemavu, asipopata elimu ndiyo tunamuandaa na kumpeleka katika kundi la kuwa ombaomba. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nina furaha kwa sababu mama Ndalichako ni mwananmke na wanasema “uchungu wa mwana, aujuaye mzazi” na hasa mama! Wewe ni mama! Nakuomba kwa moyo wangu wote, angalia watoto wenye ulemavu. Waandalie mazingira mazuri ili waweze kupata elimu. (Makofi)
Mheshimiwa naibu Spika, changamoto ni nyingi. Miundombinu sio rafiki kwa maana hiyo hata anapokwenda shule bado ni shida huyu mtoto! Ukienda vijijini watoto wanatembea kilometa saba, kama ni mtoto mwenye ulemavu atawezaje kutembea kilometa saba kwenda kupata elimu? Kwa hiyo hii inakuwa ni changamoto, hawezi kwenda kupata elimu!
Mheshimiwa Naibu Spika, yuko mtoto mmoja aliamua yeye kila siku awe anambeba mdogo wake, kumpeleka shule kwa sababu alijua hii ndiyo njia ya kumsaidia mdogo wake! Lakini alifika mahali kwa sababu yule binti anakua na uzito, alishindwa. Kwa hiyo, yule kijana alishindwa kumsaidia mdogo wake na mdogo wake akaishia hapo hakupata tena elimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda katika shule zetu, mfano watoto wenye ulemavu wasioona, hawa wanahitaji vifaa ambavyo vinawawezesha mfano mashine za braille, katika shule nyingi hakuna hizo mashine. Huyu mtoto ili aweze kupata elimu inakuwa ni vigumu kwake. Naiomba Serikali kuhakikisha kwamba hivi vifaa vinapatikana na kwa sababu Waziri wa Fedha yuko hapa viko vifaa ambavyo ni muhimu vya kupunguziwa kodi au vikaondolewa kodi kabisa ili kuhakikisha watoto wenye ulemavu wanapata elimu! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika vyuo vyetu na vyuo vya ualimu, kwa nini Serikali isione umuhimu wa lugha za alama zikafundishwa ili Walimu wote wanapotoka shule wawe na ufahamu wa lugha hizi za alama, kwa sababu wakijua hivyo, mwanafunzi mwenye uziwi kule kijijini hatakuwa na haja ya kutafuta shule nyingine. Ndiyo maana ukienda hata katika vyuo vikuu ni nadra sana kuwakuta wanafunzi viziwi! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kwa sababu hakuna Walimu wenye utaalam huo. Kwa hiyo, naomba sana Serikali kuhakikisha kwamba mitaala ya lugha za alama inafundishwa Walimu wote waweze kufahamu, lakini pia kuna ubaya gani kuingiza katika syllabus ili hata hawa wanafunzi wengine waweze kuwasiliana kwa sababu watajua kwa kujifunza hizi lugha za alama. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ziko shule za binafsi na hapa Serikali tungeweza pia kuzitumia hizi shule za binafsi kwa kupunguza baadhi ya kodi ili watoto wenye ulemavu na wao wakapata nafasi. Ukimpunguzia kodi, atawachukua watoto, watano, wane; tayari hawa watoto wamepata elimu! Katika vyuo vyetu sio rafiki na hasa vyuo binafsi na hata Chuo Kikuu cha Dar es Salaam chenyewe ukinipeleka hata mimi pale mazingira sio rafiki ili niweze kusoma. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tuhakikishe kwamba vyuo vyetu vyote na hii sheria ipo na nakumbuka mwaka 2013/2014, Waziri Lukuvi wakati huo tukiadhimisha siku ya watu wenye ulemavu duniani pale Iringa, alilizungumzia hili kuhakikisha kwamba majengo yote yanakuwa rafiki. Nashangaa ni kwa nini mpaka leo hii baadhi ya majengo hayaangalii hilo, lakini pia katika Vyuo Vikuu, tunawaandaa vipi hawa wanafunzi katika suala la mikopo? Wengine hawawezi hata kufuatilia. Tuwe na tangazo maalum, tuwaelekeze wanafunzi wanaomaliza elimu ya form six kuhakikisha kwamba wanapotaka kwenda kujiunga utaratibu mzuri umeandaliwa kwa ajili yao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mambo ni mengi, changamoto ni nyingi, lakini nimalizie kwa kusema kwamba; elimu ndiyo ufunguo wa maisha. Ukimwezesha mtoto mweye ulemavu, umemkomboa! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga hoja mkono.